Mara nyingi hedhi ya mwanamke hukatika wakati anaposhika mimba. Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) amesema:

“Mwanamke yajulikana kuwa ameshika mimba kwa kule damu yake kukatika.”

Mwanamke mwenye mimba akipata damu pamoja na machungu kwa siku mbili au tatu kabla ya kuzaa, basi hiyo ni nifasi. Hata hivyo haizingatiwi kuwa ni nifasi ikiwa ataipata kipindi kirefu kabla ya kuzaa au kipindi kifupi kabla ya kuzaa lakini bila ya machungu. Je, ni katika damu ya hedhi ilio na hukumu kama ya hedhi au ni damu isiyokuwa na maana isiyokuwa na hukumu kama ya hedhi? Wanachuoni wametofautiana katika hili. Kauli sahihi ni kwamba ni damu ya hedhi ikiwa inatokamana na hedhi ya kawaida ya mwanamke. Kwa sababu damu ambayo huwa inamtoka mwanamke asli huwa ni hedhi maadamu hakujathibitishwa kinyume chake. Isitoshe hakuna katika Qur-aan na Sunnah dalili inayoonesha kuwa mwanamke mwenye mimba hawezi kupata hedhi. Hii ni kauli ya madhehebu ya Maalik na ash-Shaafi´iy ambayo imechaguliwa na Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah ambaye amesema:

“al-Bayhaqiy amesimulia kuwa ni moja katika kauli ya Ahmad. Bali imesemekana kuwa alirejea katika kauli hii.”[1]

Kujengea juu ya hili yanathibiti kwa mwanamke mwenye mimba aliye na hedhi yale yenye kuthibiti kwa mwanamke asiyekuwa na mimba aliye na hedhi isipokuwa katika hali tatu:

1- Talaka. Ni haramu kumtaliki mwanamke wakati wa eda [katika twahara uliyomwingilia na] wakati yuko na hedhi. Hata hivyo si haramu kumtaliki mwanamke mjamzito. Kumtaliki mwanamke asiyekuwa na mimba wakati wa hedhi yake ni jambo linaloenda kinyume na Kauli Yake (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ إِذَا طَلَّقْتُمُ النِّسَاءَ فَطَلِّقُوهُنَّ لِعِدَّتِهِنَّ وَأَحْصُوا الْعِدَّةَ

“Ee Nabii! Mtakapowataliki wanawake, basi watalikini katika wakati wa eda [twahara na si katika hedhi au katika twahara mliyowaingilia].” (65:01)

Pamoja na hivyo ni jambo lisiloenda kinyume nayo akimtaliki mwanamke mwenye mimba wakati yuko na hedhi. Kwa sababu mwenye kumtaliki mwenye mimba anachofuata ni eda yake inayoisha kwa kule kuzaa kwake na haijalishi kitu sawa akiwa na hedhi au akiwa twahara pindi anapoachika. Kwa ajili hiyo ndio maana sio haramu kumtaliki mwanamke mwenye mimba baada tu ya kufanya jimaa tofauti na mwanamke asiyekuwa na mimba.

2- Eda ya mwanamke mwenye mimba aliye na hedhi haiishi tofauti na mwanamke mwenye hedhi asiyekuwa na hedhi. Eda ya mwanamke mwenye mimba inaisha kwa kuzaa, sawa akiwa na hedhi au hapana. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَأُولَاتُ الْأَحْمَالِ أَجَلُهُنَّ أَن يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ

“Na wenye mimba muda wao [wa eda] watakapozaa mimba zao.” (65:04)

[1] al-Ikhtiyaaraat, uk. 35

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ad-Dimaa’ at-Twabiy´iyyah lin-Nisaa’ http://www.ibnothaimeen.com/all/books/article_16961.shtml
  • Imechapishwa: 30/10/2016