Allaah (Jalla wa ´Alaa) katika Qur-aan ametaja ´Mola` baadhi ya sehemu na ametaja vilevile ´Mungu` sehemu zingine. Kwa mfano Suurah “an-Naas” anasema (Subhaanahu wa Ta´ala):

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ قُلْ أَعُوذُ بِرَبِّ النَّاسِ مَلِكِ النَّاسِ إِلَـٰهِ النَّاسِ

“Kwa Jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu. Sema: “Najilinda na Mola wa watu. Mfalme wa watu. Mungu wa watu.”” (114: 01-03)

Ni ipi tofauti kati ya Mola wa watu na Mungu wa watu? Je, yana maana moja? Basi ingelikuwa maneno yamejirudi. Je, yana maana mbili tofauti? Ni wajibu kujua tofauti kati ya hayo mawili. Ni mara nyingi neno ´Mola` linatajwa. Kama mfano wa maneno Yake (Ta´ala):

قُلْ مَن رَّبُّ السَّمَاوَاتِ السَّبْعِ وَرَبُّ الْعَرْشِ الْعَظِيمِ سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ

“Sema: “Nani Mola wa mbingu saba na Mola wa ´Arishi kubwa?” Watesema: “Ni ya Allaah.” (23:86-87)

Neno ´Mola` na ´Mungu` yamekariri. Nini maana ya kila limoja katika hayo mawili?

Mola maana yake ni yule mwenye kuwalea viumbe Wake kwa neema Zake na kuwatunuku riziki. Inahusiana na malezi ya kimwili kwa kuwaruzuku na kuwalisha na malezi ya kiroho kwa Wahy na elimu yenye manufaa na kuwatuma Mitume.

Miongoni mwa maana za Mola ni yule anayemiliki mbingu na ardhi. Mola wa kitu ni yule mwenye kukimiliki na kukiendesha. Miongoni mwa maana za Mola vilevile ni mrekebishaji anayeyarekebisha mambo na kuyazuia kutokamana na yale yanayoyaharibu. Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ndiye ambaye anasilihi kulimwengu huu na kuupanga kwa vile yanavopelekea matakwa na hekima Yake (Subhaanahu wa Ta´ala).

Kuhusu Mungu maana yake ni yule mwenye kuabudiwa. Ni neno linalotokamana na uabudiwaji. Kwa hiyo Mungu maana yake ni yule mwenye kuabudiwa. Mungu haina maana kwamba ni Mola. Bali maana yake ni muabudiwaji. Uungu (Ilaahiyyah) ni ´ibaadah. Uugu (Ulh) ni kupenda. Kwa kuwa Yeye (Subhanaahu wa Ta´ala) anapendwa na waja Wake waumini, wanamwogopa, wanamtarajia na wanajikurubisha Kwake. Hii ndio maana ya Mungu. Kwa hiyo kumepata kubainika tofauti kati ya maana ya ´Mola` na maana ya ´Mungu` na kwamba hayana maana moja. Mwenye kusema kuwa yana maana moja basi amekosea.

Wanachuoni wanasema kuwa yanapotajwa yote mawili Mola inakuwa na maana yake na Mungu inakuwa na maana yake. Pindi linapotajwa limoja ndani yake kunaingia maana ya lingine. Lakini yakitajwa pamoja – kama ilivyokuja katika Suurah “an-Naas” – Mola inakuwa na maana yake na Mungu inakuwa pia na maana yake nyingine. Ni kama mfano wa neno ´fakiri` na ´masikini`. Yanapotajwa kwa pamoja, kama katika maneno Yake (Ta´ala):

إِنَّمَا الصَّدَقَاتُ لِلْفُقَرَاءِ وَالْمَسَاكِينِ

“Hakika swadaqah [zakaah] ni kwa ajili ya mafakiri na masikini.” (09:60)

fakiri inakuwa na maana yake na masikini inakuwa na maana yake. Fakiri ni yule asiyekuwa na kitu kabisa. Kuhusu masikini ni yule aliye na baadhi ya vitu vyenye kumtosha. Masikini ana hali ya afadhali kidogo kuliko fakiri.

Kadhalika ni kama neno ´Uislamu` na ´imani`. Kunapotajwa Uislamu na imani kwa pamoja Uislamu inakuwa ni yale matendo ya dhahiri na imani ni yale matendo ya ndani, kama ilivyokuja katika Hadiyth ya Jibriyl (´alayhis-Salaam) alipomwambia:

“Nieleze kuhusu Uislamu?” Akasema: “Uislamu ni kuhushudia ya kwamba ´hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah`, kusimamisha swalah, kutoa zakaah, kufunga Ramadhaan, kuhiji Nyumba ukiweza kuiendea.” Muslim (08), at-Tirmidhiy (2610), an-Nasaa´iy (4990), Abu Daawuud (4695), Ibn Maajah (63) na Ahmad (01/27).

Ameufasiri kwa nguzo za dhahiri. Akamuuliza tena:

“Nieleze kuhusu imani?” Akasema: “Imani ni kumuamini Allaah, Malaika Wake, Vitabu Vyake, Mitume Wake, siku ya Mwisho na kuamini Qadar kheri na shari yake.” Muslim (08), at-Tirmidhiy (2610), an-Nasaa´iy (4990), Abu Daawuud (4695), Ibn Maajah (63) na Ahmad (01/27).

Akaifasiri kwa yale matendo ya ndani yaliyomo kwenye moyo. Hapa ni pale ambapo yote mawili yatatajwa kwa pamoja. Katika hali hii kila moja linakuwa na maana yake. Kunapotajwa moja katika hayo basi kunaingia pia na lile lingine.

Kuanzia hapa tunapata kuelewa vilevile tofauti iliyopo kati ya Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah.

Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah ni kutambua ya kwamba Allaah ndiye Muumbaji, Mruzukaji, Muhuishaji na Mfishaji. Kwa msemo mwingine ni kule kuyatambua matendo ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala).

Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah maana yake ni waja kumpwekesha Allaah katika matendo yao ambayo wanajikurubisha kwayo Kwake katika yale matendo aliyoyaweka katika Shari´ah. Hii ndio maana ya Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah. Kuna tofauti kati ya Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah.

Maadamu tumejua maana ya Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah tunarudi katika hali ya washirikina waliotumiwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Walikuwa wakikubali aina ya Tawhiyd ya kwanza, Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah, lakini hata hivyo haikuwaingiza katika Uislamu. Bali Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwazingatia kuwa ni makafiri na washirikina na akawapiga vita ilihali ni wenye kukubali Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Wao waliikubali Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na wakakanusha Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah. Walipotakwa wampwekeshe Allaah kwa ´ibaadah na waache kuyaabudu masanamu walisema:

أَجَعَلَ الْآلِهَةَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا ۖ إِنَّ هَـٰذَا لَشَيْءٌ عُجَابٌ

“Amewafanya waungu wote kuwa ni mungu Mmoja? Hakika hili ni jambo la ajabu mno.” (38:05)

Hapa ilikuwa baada ya yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwaambia waseme ´hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah`. Walielewa kuwa maana yake ni kutomuabudu mwengine asiyekuwa Allaah hali ya kuwa hana mshirika yoyote. Walikuwa na masanamu na waungu wengine wengi ambao walikuwa hawako tayari kuwaacha na badala yake kukomeka na kumuabudu Allaah. Hawakuwa wenye kuridhia hilo na ndio maana wakakataa na kusema:

أَجَعَلَ الْآلِهَةَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا ۖ إِنَّ هَـٰذَا لَشَيْءٌ عُجَابٌ

“Amewafanya waungu wote kuwa ni mungu Mmoja? Hakika hili ni jambo la ajabu mno.” (38:05)

Tunatakwa kumuabudu Allaah peke yake na kuacha kumuabudu al-Laat, al-´Uzzaa, Manaat, Habl na masanamu mengine? Hili ni jambo walilokuwa wanaona kuwa haliingii akilini mwao:

مَا سَمِعْنَا بِهَـٰذَا فِي الْمِلَّةِ الْآخِرَةِ

“Hatukusikia haya katika mila ya mwisho.” (38:07)

Bi maana mila za mababu zao. Huku ni kutumia hoja kwa yale waliyokuwemo mababu zao. Ni hoja yenye kulaaniwa iliokuwa ikitumiwa na nyumati zilizokuwa hapo kabla pale wanapoitwa kumuabudu Allaah pekee. Hata Fir´awn na yeye alisema:

فَمَا بَالُ الْقُرُونِ الْأُولَىٰ

”Basi ni vipi hali ya karne za awali?” (20:51)

Walipoelewa maana ya ´hapana mungu isipokuwa Allaah` wakashangazwa na hili na kulipinga na wakausiana kuitupilia mbali. Katika Aayah nyingine anasema (Subhaanahu wa Ta´ala) kuhusu wao:

إِنَّهُمْ كَانُوا إِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا اللَّـهُ يَسْتَكْبِرُونَ وَيَقُولُونَ أَئِنَّا لَتَارِكُو آلِهَتِنَا لِشَاعِرٍ مَّجْنُونٍ

“Hakika wao walipokuwa wakiambiwa: “Hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah” wanatakabari na husema: “Je, hivi kweli tuache miungu yetu kwa ajili ya mshairi mwendawazimu?”” (37:35-36)

Haya yanabainisha maana ya ´hapana mungu isipokuwa Allaah` kikamilifu, kuiweka wazi na kukata mizozo. Hapa kuna Radd kwa wale waliokosea maana ya ´hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah`. Katika vitabu vya wanachuoni wa falsafa wanasema kuwa ´hapana mungu isipokuwa Allaah` maana yake ni hakuna muumbaji, mruzukaji na muweza wa kuumba isipokuwa Allaah. Hii ndio ´Aqiydah yao pia. Kwa mujibu wao hii ndio maana ya mungu. Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) anasema:

“Mjuzi kabisa katika wao anasema kuwa mungu ni yule mwenye kuweza kuumba. Huu ni ujinga mkubwa wa lugha na Shari´ah takasifu. Maana ya mungu ni yule mwenye kuabudiwa. Wao hawakufahamu maana ya mungu. Kwa kuwa maana ya mungu ni yule mwenye kuadhimishwa na mioyo, kunyenyekewa na kujikurubisha kwake.”[1]

Hawakuelewa maana ya mungu. Ndio maana wanaisema ´hapana mungu isipokuwa Allaah` kwa wingi na wana nyuradi wanazozikariri asubuhi na mchana. Pamoja na haya yote wanayaabudu makaburi na wanataka uokozi kutoka kwa asiyekuwa Allaah (´Azza wa Jall). Hawakuelewa maana ya hapana mungu isipokuwa Allaah na kwamba inawataka kuacha kuyaabudu makaburi na vyengine asiyekuwa Allaah katika masanamu, miti na mawe na kwamba wakiisema inawalazimu kuacha kuabudu mizimu. Kuhusu hawa hapa – yaani washiriina wa leo – wameisema na wakati huo huo wanaabudu asiyekuwa Allaah. Washirikina wa mwanzo ni wajuzi zaidi kuliko hawa. Kwa ajili hii amesema Shaykh [Ibn ´Abdil-Wahhaab]:

“Hakuna kheri kwa mtu ambaye washirikina wajinga ni wajuzi zaidi wa ´hapana mungu isipokuwa Allaah` kuliko yeye.””

[1] Tadmuriyyah, uk. 185-186.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 29-32
  • Imechapishwa: 02/11/2016