18 – Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Nilisafiri pamoja na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Ramadhaan na yule mwenye kufunga hakumkosoa yule ambaye hakufunga na yule ambaye hakufunga hakumkosoa yule ambaye amefunga.”[1]

Kuna maafikiano juu yake.

Hadiyth hii ni dalili juu ya kwamba msafiri yuko na khiyari kati ya kufunga akiona yuko na nguvu za kufanya hivo au kufungua akiona kufanya hivo ndio kunamfanya kuwa na nguvu na baadaye atalipa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwakubalia Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) juu ya yote mawili. Kukubali kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni hoja. Jambo hili ni miongoni mwa wepesi wa Shari´ah na sifa zote njema anastahiki Allaah. Amesema (Ta´ala):

وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ

”Na atakayekuwa mgonjwa au safarini basi [atimize] idadi katika siku nyinginezo. Allaah anakutakieni mepesi na wala hakutakieni magumu.”[2]

Ruhusa ya kufungua inategemea safari na sio ule ugumu. Kwa mfano akisafiri kwa ndege basi inafaa kwake kula kwa sababu ni msafiri ambaye ameacha mji wake.

Maandiko yamefahamisha kuwa msafiri swawm ikimtia uzito mkubwa basi itaharamika kwake kufunga. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipofikiwa na khabari – pindi alipokuwa katika vita vya Ufunguzi – kwamba swawm imekuwa ngumu kwa watu, basi aliitisha maji baada ya alasiri akanywa na huku watu wakimtazama. Akasema pindi alipoambiwa kuwa baadhi ya watu wameendelea kufunga:

“Hao ndio waasi. Hao ndio waasi.”[3]

Lakini ikiwa funga inamtia uzito usiokuwa mkubwa, bora kwake ni kula. Hilo ni ktuokana  na maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hakika Allaah anapenda ziendewe ruhusa Zake kama anavochukia kuendewa maasi Yake.”[4]

Imekuja katika Hadiyth nyingine:

“Hakika Allaah anapenda ziendewe ruhusa Zake kama anavopenda yaendewe maamrisho Yake.”[5]

Ikiwa swawm haimtii uzito basi atafanya kile ambacho ni rahisi zaidi kwake. Yakilingana basi itakuwa ni bora zaidi kufunga kutokana na kitendo cha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Isitoshe kufanya hivo ndio haraka zaidi kuitakasa dhimma yake na kuchangamfu zaidi kwake akifunga na wengine.

Kuhusu mgonjwa, akiweza kufunga pasi na madhara wala uzito atalazimika kufunga. Vinginevyo atakula kutokana na kuenea kwa maneno Yake (Ta´ala):

وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ

”Na atakayekuwa mgonjwa au safarini basi [atimize] idadi katika siku nyinginezo. Allaah anakutakieni mepesi na wala hakutakieni magumu.”[6]

Maradhi yakizuka katikati ya mchana ilihali amefunga na ikawa vigumu kukamilisha siku yake, basi itafaa kwake kufungua sehemu yoyote ile ya mchana kwa kupatikana udhuru unaomruhusu kufungua.

Kuhusu mtumzima asiyeweza kufunga anatakiwa badala yake kumlisha masikini kwa kila siku itakayompita. Inapokuja katika  chakula anapewa khiyari kati ya kukigawa kwa wale masikini awatakao. Kila mmoja atampa Mudd ya ngano nzuri. Kiwango cha Mudd ni gramu 563. Chaguo jengine ni kwamba anaweza kupika chakula na akawaalika wale masikini kwa kiwango cha yale masiku ambayo hakufunga. Hilo ni kutokana na yale yaliyopokelewa kutoka kwa Anas (Radhiya Allaahu ´anh):

“Kwamba kuna mwaka alidhoofika kufunga ambapo akatengeneza bakuli la Thariyd na akawaalika masikini thelathini na akawashibisha.”[7]

Ikiwa mzee amefikia ule umri wa kuchanganyikiwa na ameondokewa na jambo la kupambanua mambo, basi hahitajii kufunga wala kulisha chakula. Kwa sababu mzee huyu ´ibaadah si zenye kumuwajibikia. Ikiwa kuna wakati fulani anaweza kupambanua mambo, basi atalazimika kufunga katika kile kipindi cha kupambanua kwake mambo pasi na kile kipindi cha kuchanganyikiwa kwake[8] – na Allaah ndiye mjuzi zaidi.

“Ee Allaah! Hakika sisi tunajilinda kwa ridhaa Yako kutokamana na hasira Zako, msamaha Wako kutokamana na adhabu Yako na naomba ulinzi Kwako kutokamana na Wewe. Hatuwezi kukusifu vile Unavostahiki Wewe ni kama vile Ulivyojisifu Mwenyewe. Tunakuomba utuongoze katika matendo mema na tabia njema – kwani hakika hakuna anayeongoza katika nzuri yazo isipokuwa Wewe. Pia utuepushe na tabia mbaya – kwani hakika hakuna anayeepusha katika mbaya yazo isipokuwa Wewe, utusamehe sisi, wazazi wetu na waislamu wote.

[1] al-Bukhaariy (1947) na Muslim (1121).

[2] 02:185

[3] Muslim (1114).

[4] Ahmad (10/112), Ibn Khuzaymah (950) na Ibn Hibbaan (06/451).

[5] Ibn Hibbaan (08/333) na at-Twabaraaniy katika ”al-Kabiyr” (11881).

[6] 02:185

[7] ´Abdur-Razzaaq (7570), Ibn Abiy Shaybah (07/533), ad-Daaraqutwniy (02/207) na wengineo. Cheni ya wapokezi wake ni Swahiyh na iliyothibiti. Tazama “Sharh-ul-´Umrah” Kitaab-us-Swiyaam (02/260).

[8] Tazama ”Majaalis Ramadhwaan”, uk. 28 ya Shaykh Muhammad bin ´Uthaymiyn.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Mukhtaswar Ahaadiyth-is-Swiyaam, uk. 51-53
  • Imechapishwa: 28/04/2022