Halafu Mitume Wake ni wakweli na ni wenye kusadikishwa… – Ni wajibu kwa kila yule ambaye ´ibaadah ni yenye kumuwajibikia kuwasadikisha. Hawakuleta chochote kutoka kwa Allaah isipokuwa ni cha kweli. Kwa hivyo wao ni wakweli na ni wenye kusadikishwa. Lililo la wajibu kwa kila yule ambaye ´ibaadah ni yenye kumuwajibikia kuwasadikisha na kutendea kazi yale waliyokuja nayo. Kila Ummah unatakiwa utendee kazi yale yaliyoletwa na Mtume wao. Mtume wa Ummah huu ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ni wajibu kwao kufuata yale aliokuja nayo na kunyenyekea Shari´ah yake. Amesema (Ta´ala):

وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا

“Na lolote lile analokupeni Mtume basi lichukueni, na lolote lile analokukatazeni, basi acheni.” (59:07)

قُلْ يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُمْ جَمِيعًا

“Sema: “Hakika mimi ni Mtume wa Allaah kwenu nyinyi nyote.” (07:158)

Ni wajibu kwa kila ambaye ´ibaadah ni yenye kumuwajibikia kufuata zile hukumu ambazo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekuja nazo. Sawa hukumu hizo ziwe zinahusiana na mambo ya kufanya au ya kuacha.

Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja vilevile na yale aliyoelezea juu ya majina na sifa za Allaah. Ni wajibu kumsadikisha katika hayo na kuamini majina na sifa zote alizoelezea juu ya Allaah. Mtu aamini pasi na kufananisha. Badala yake mtu anatakiwa aamini na wakati huo huo amtakase Allaah na kushabihiana na viumbe Vyake na iwe ni utakaso usiokuwa ndani yake na ukanushaji. Kwa ajili hiyo ndio maana amesema (Rahimahu Allaah):

“… tofauti na wale wanaosema juu Yake yale wasioyajua.”

Hawa ni wale makafiri na wajinga. Kwa ajili hii ndio maana ameitakasa nafsi Yake kwa yale waliyosema waongo pale aliposema (Ta´ala):

سُبْحَانَ رَبِّكَ رَبِّ الْعِزَّةِ عَمَّا يَصِفُونَ وَسَلَامٌ عَلَى الْمُرْسَلِينَ وَالْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ

“Ametakasika Mola wako Mola Mtukufu kutokana na yote wanayoelezea na amani iwe juu ya Mitume na himidi zote ni za Mola wa walimwengu.” (37:181-182)

Amejihimidi Mwenyewe kwa sababu Yeye ni mkamilifu katika dhati Yake, majina na sifa Zake. Akasema:

وَالْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ

“Na himidi zote ni za Mola wa walimwengu.”

Vilevile amejitakasa Mwenyewe kwa yale waliyosema wale wenye kwenda kinyume na Mitume miongoni mwa maadui zao pale aliposema:

سُبْحَانَ رَبِّكَ رَبِّ الْعِزَّةِ عَمَّا يَصِفُونَ

“Ametakasika Mola wako Mola Mtukufu kutokana na yote wanayoelezea.”

Bi maana yale ambayo maadui wa Allaah wanamuelezea kwayo katika makafiri ambapo wamemnasibishia mwana, mke na mshirika. Yote haya ni batili. Kwa ajili hiyo ndio maana amejitakasa Mwenyewe. Hakujichukulia mke wala mtoto.

Hakika Yeye (Subhaanah) yupekee na ndiye Mwenye kukusudiwa na hana mshirika. Yeye ndiye Mungu wa haki. Amesema (Ta´ala):

وَإِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ ۖ لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الرَّحْمَـٰنُ الرَّحِيمُ

“Na Mungu wenu ni Allaah Mungu Mmoja Pekee, hapana mungu wa haki ila Yeye. Mwingi wa Rahmah, Mwenye kurehemu.” (02:163)

Halafu akawasalia Mitume kutokana na usalama wa yale mapungu na aibu walizokanusha pale aliposema:

وَسَلَامٌ عَلَى الْمُرْسَلِينَ

Na amani iwe juu ya Mitume.”

Amefanya hivi kwa sababu Mitume wamejisalimisha kwa Allaah kutokana na yale aliyowaeleza juu Yake na wakanyenyekea Kwake na hatimaye wakawafikishia watu. Wao wako salama na wamesalimishwa, ni wakweli na wamesadikishwa. Kisha akajihimidi Nafsi Yake pale aliposema:

وَالْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ

“Na himidi zote ni za Mola wa walimwengu.”

kutokana na ukamilifu wa dhati, sifa na matendo Yake (Subhaanahu wa Ta´ala). Yeye ana himdi kamilifu.

  • Mfasiri: Firqatunnajia.com