[21] Yule mwenye kunyanyua sauti yake mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kunachelea juu yake kuporomoka matendo yake. Amesema (´Azza wa Jall):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَرْفَعُوا أَصْوَاتَكُمْ فَوْقَ صَوْتِ النَّبِيِّ وَلَا تَجْهَرُوا لَهُ بِالْقَوْلِ كَجَهْرِ بَعْضِكُمْ لِبَعْضٍ أَن تَحْبَطَ أَعْمَالُكُمْ وَأَنتُمْ لَا تَشْعُرُونَ

“Enyi walioamini! Msizinyanyue sauti zenu juu ya sauti ya Mtume na wala msiseme naye kwa sauti ya juu kama mnavyosemezana wenyewe kwa wenyewe kwa sauti za juu, yasije yakaporomoka matendo yenu nanyi hamhisi.”[1]

Akawafunza adabu namna wanavyotakiwa kuwa pindi wanapomzungumzisha na kuzungumza na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Akasema:

لَّا تَجْعَلُوا دُعَاءَ الرَّسُولِ بَيْنَكُمْ كَدُعَاءِ بَعْضِكُم بَعْضًا

“Msifanye wito wa Mtume baina yenu kama wito wa nyinyi kwa nyinyi.”[2]

Msisemi: ”Ee Ahmad! Ee Muhammad! Ee Abul-Qaasim!” Badala yake semeni: “Ee Mtume wa Allaah! Ee Nabii wa Allaah!” Allaah (´Azza wa Jall) amesema:

لِّتُؤْمِنُوا بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَتُعَزِّرُوهُ وَتُوَقِّرُوهُ وَتُسَبِّحُوهُ بُكْرَةً وَأَصِيلًا

“Ili mumwamini Allaah na Mtume Wake na mumtukuze na mumheshimu na mumsabihi asubuhi na jioni.”[3]

Amewaamrisha kumuadhimisha yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kama ambavyo Yeye kamuadhimisha na kumtukuza mbele ya Mitume wengine wote kwa vile anamsemesha:

يَا أَيُّهَا الرَّسُولُ بَلِّغْ مَا أُنزِلَ إِلَيْكَ مِن رَّبِّكَ

“Ee Mtume! Fikisha yale yaliyoteremshwa kwako kutoka kwa Mola wako.”[4]

Sambamba na hilo amewasemesha Mitume kwa majina yao: “Ee Aadam!”, “Ee Nuuh!”, “Ee Ibraahiym!”, “Ee Muusa!” na “Ee ´Iysaa!” Amesema:

وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا

“Kile anachokupeni Mtume basi kichukueni na anachokukatazeni basi kiacheni.”[5]

Amefanya maamrisho na makatazo yake kuwa na nafasi kama ya Qur-aan. Kadhalika akamkusanyia sifa mbili miongoni mwa sifa Zake na akasema:

لَقَدْ جَاءَكُمْ رَسُولٌ مِّنْ أَنفُسِكُمْ عَزِيزٌ عَلَيْهِ مَا عَنِتُّمْ حَرِيصٌ عَلَيْكُم بِالْمُؤْمِنِينَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ

“Hakika amekujieni Mtume anayetokana na jinsia yenu nyinyi wenyewe. Yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni, anakuhangaikieni na kwa waliomuamini ni mpole na mwenye huruma.”[6]

Hakuwahi kuapa kwamba yeyote ni Mtume isipokuwa yeye. Amesema:

وَالْقُرْآنِ الْحَكِيمِ إِنَّكَ لَمِنَ الْمُرْسَلِينَ عَلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ

“Naapa kwa Qur-aan yenye hekima. Hakika wewe ni miongoni mwa Mitume. Uko juu ya njia iliyonyooka.”[7]

Vilevile amesema:

لَعَمْرُكَ إِنَّهُمْ لَفِي سَكْرَتِهِمْ يَعْمَهُونَ

“Naapa kwa umri wako hakika wao walikuwa katika ulevi wao wanatangatanga kwa upofu.”[8]

Ameeleza kwamba Ibraahiym amesema:

وَلَا تُخْزِنِي يَوْمَ يُبْعَثُونَ

“Usinihizi siku watakayofufuliwa.”[9]

Halafu akamjibu juu ya hilo. Hata hivyo ameyasema haya juu ya Mtume wetu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pasi na yeye kuanza kumuomba:

يَوْمَ لَا يُخْزِي اللَّـهُ النَّبِيَّ وَالَّذِينَ آمَنُوا مَعَهُ

“Siku ambayo Allaah hatomfedhehesha Nabii na wale walioamini pamoja naye.”[10]

Muusa amesema:

قَالَ رَبِّ اشْرَحْ لِي صَدْرِي

“Akasema: “Mola wangu nikunjulie kifua changu.”[11]

Allaah akamjibu juu ya hilo na akasema:

قَدْ أُوتِيتَ سُؤْلَكَ يَا مُوسَىٰ

“Umekwishapewa ombi lako, ee Muusa.”[12]

Hata hivyo alisema kumwambia Mtume wetu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

أَلَمْ نَشْرَحْ لَكَ صَدْرَكَ

“Je, kwani hatukukupanulia kifua chako kukubainishia?”[13]

Amemsamehe madhambi yake pamoja na kuyaficha na wakati huohuo amesamehe madhambi ya wengine pamoja na kuyaweka wazi. Amesema:

وَعَصَىٰ آدَمُ رَبَّهُ فَغَوَىٰ ثُمَّ اجْتَبَاهُ رَبُّهُ فَتَابَ عَلَيْهِ وَهَدَىٰ

“Aadam akamuasi Mola wake akapotoka kisha Mola wake akamteua akapokea tawbah yake na akamwongoza.”[14]

Amesema kumwambia Daawuud:

وَظَنَّ دَاوُودُ أَنَّمَا فَتَنَّاهُ فَاسْتَغْفَرَ رَبَّهُ وَخَرَّ رَاكِعًا وَأَنَابَ فَغَفَرْنَا لَهُ ذَٰلِكَ ۖ وَإِنَّ لَهُ عِندَنَا لَزُلْفَىٰ وَحُسْنَ مَآبٍ

“Daawuud akahisi kwamba Tulimpa mtihani, basi akamuomba Mola wake msamaha na akaanguka chini kusujudu na akatubia. Hivyo tukamsamehe hayo na hakika yeye bila shaka ana Kwetu makurubisho na marejeo mazuri.”[15]

Vilevile amesema:

وَلَقَدْ فَتَنَّا سُلَيْمَانَ وَأَلْقَيْنَا عَلَىٰ كُرْسِيِّهِ جَسَدًا ثُمَّ أَنَابَ

“Hakika Tulimpa mtihani Sulaymaan na tukamtupia juu ya kiti chake mwili kisha akarejea.”[16]

Pia amesema:

وَذَا النُّونِ إِذ ذَّهَبَ مُغَاضِبًا فَظَنَّ أَن لَّن نَّقْدِرَ عَلَيْهِ فَنَادَىٰ فِي الظُّلُمَاتِ أَن لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا أَنتَ سُبْحَانَكَ إِنِّي كُنتُ مِنَ الظَّالِمِينَ

“Dhan-Nuun alipoondoka hali ya kuwa ameghadhibika akadhani kwamba hatutamdhikisha, akaita katika kiza kwamba: “Hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Wewe, kutakasika kutokamana na mapungufu ni Kwako! Hakika mimi nilikuwa miongoni mwa madhalimu.”[17]

Amesema kumwambia Mtume wetu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

لِّيَغْفِرَ لَكَ اللَّـهُ مَا تَقَدَّمَ مِن ذَنبِكَ وَمَا تَأَخَّرَ

“Ili Allaah akusamehe yale yaliyotangulia katika madhambi yako na yale yanayofuatia.”[18]

Hakuyataja madhambi hayo. Kadhalika amesema:

أَلَمْ نَشْرَحْ لَكَ صَدْرَكَ وَوَضَعْنَا عَنكَ وِزْرَكَ الَّذِي أَنقَضَ ظَهْرَكَ

“Je, kwani hatukukupanulia kifua chako kukubainishia na Tukakuondolea mzigo [madhambi] wako ambao ulithakilisha mgongo wako?”[19]

Hata hivyo hakutaja mzigo huo.

[1] 49:02

[2] 24:63

[3] 48:09

[4] 05:67

[5] 59:07

[6] 09:128

[7] 36:02-04

[8] 15:72

[9] 26:87

[10] 66:08

[11] 20:25

[12] 20:36

[13] 94:01

[14] 20:121-122

[15] 38:24-25

[16] 38:34

[17] 21:87

[18] 48:02

[19] 94:01-03

  • Mhusika: Imaam Abul-Husayn Muhammad bin Abiy Ya´laa al-Hanbaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Kitaab-ul-I´tiqaad, uk. 41-42
  • Imechapishwa: 26/02/2019