Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Muumini mwenye nguvu anapendwa zaidi na Allaah kuliko muumini dhaifu – na kwa wote wawili kuna kheri. Pupia yale yanayokunufaisha na mtake msaada Allaah (´Azza wa Jall) na wala usishindwe. Ukifikwa na jambo basi usisemi ´Lau ningefanya kadhaa basi ingelikuwa kadhaa na kadhaa`. Badala yake sema:

قَدَر الله و ما شاء فعل

“Makadirio ya Allaah na Anayotaka huwa.”

Kwani hakika “Lau” inafungua matendo ya shaytwaan.”[1]

Huenda mtu akauliza ni chumo lipi ambalo ni aula na bora zaidi? Wanachuoni wametofautiana juu ya hilo. Wako ambao wamefadhilisha kilimo na mambo ya shamba, wengine wakafadhilisha biashara na wengine wakafadhilisha kazi za mikono na wengineo. Kila mmoja amelata hoja zake. Lakini Hadiyth hii ndio yenye kutatua mizozo yote, kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Pupia yale yanayokunufaisha.”

Yenye kunufaisha yanatofautiana kwa kutegemea na hali na watu. Wako ambao bora kwao ni kujishughulisha na mambo ya kilimo na shamba, wengine ni biashara na wengine ni kazi za mikono. Kwa hiyo bora ni kile chenye manufaa zaidi. Allaah amsifu na amsalimie yule ambaye amempa maneno yenye mafupi yenye maana pana!

[1] Muslim (2664), Ibn Maajah (79) na Ahmad (8611).

  • Mhusika: Imaam ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bahjatu Quluub-il-Abraar, uk. 39-40
  • Imechapishwa: 26/02/2019