12 – Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Swawm ni ngao. [Mfungaji] asizungumze maneno machafu na wala asipige kelele.” Imekuja katika upokezi mwingine: “Asifanye ujinga. Mtu akimtukana au akamgombeza, basi amwambie: “Mimi nimefunga. Mimi nimefunga.”[1]

Kuna maafikiano juu yake.

Hadiyth hii ni dalili juu ya kwamba mfungaji anatakiwa kuchunga swawm yake na kujiepusha na mambo yanayokinzana na swawm. Hayo yanakuwa kwa kujipamba na tabia njema na kujiweka mbali na zile tabia mbaya ili aitekelezee swawm yale matunda yake yanayotakiwa na impelekee katika msamaha ilioahidiwa.

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yule asiyeacha maneno ya uongo, kuyatendea kazi na ujinga, basi Allaah hana haja kwa yeye kuacha chakula na kinywaji chake.”[2]

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Swawm ni ngao.”

ni yale yanayokukinga kutokana na yale unayoogopa. Maana yake ni kwamba swawm inamlinda mtu kutokamana na madhambi ulimwenguni. Akiwa na kinga ya madhambi basi huko Aakhirah atakuwa na kinga ya Moto. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Swawm ni ngao ya Moto kama ngao ya mmoja wenu vitani.”[3]

Hii ni dalili ya wazi kabisa juu ya ubora wa swawm.

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“[Mfungaji] asizungumze maneno machafu… “

Ni kuzungumza maneno mabaya. Wakati mwingine husemwa hivo na kukakusudiwa kujamiiana na kukidhi matamanio. Amesema (Ta´ala):

أُحِلَّ لَكُمْ لَيْلَةَ الصِّيَامِ الرَّفَثُ إِلَىٰ نِسَائِكُمْ

“Mmehalalishiwa usiku wa swawm kujamiiana na wake zenu.”[4]

Wanazuoni wengi wamesema kuwa makusudio katika Hadiyth hii ni kuzungumza maneno machafu. Allaah ndiye mjuzi zaidi.

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… wala asipige kelele.”

Ni kupiga fujo.

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Asifanye ujinga.”

Makusudio ya ujinga hapa ni kinyume na upole. Kwa msemo mwingine ni kwamba asifanye kitu katika matendo ya wajinga kama kupiga kelele, upumbavu na mengineyo.

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Aseme: “Mimi nimefunga.”

Bi maana mtu akizozana naye au akamtukana basi hatangamani naye kama alivofanya. Bali anasema:

“Mimi nimefunga.”

Pengine yule mpinzani wake akakomeka kumpiga vita na kumtukana akitambua kuwa hatamshinda kwa sababu amefunga.

Swawm inayokubalika kikweli ni ile funga kwa njia ya mtu kujizuilia kutokamana na madhambi, mdomo kutokamana na uwongo na maneno machafu, tumbo kutokamana na chakula na kinywaji, tupu kutokamana na jimaa na kuchanganyikana na wanawake.

Swawm ni masomo ya kimalezi inayofunza upole, subira na ukweli na pia inahimiza tabia njema na ubora wa maneno na matendo. Mfungaji hapigi kelele, hafanyi upuuzi  na wala hakasiriki. Hazungumzi uwongo. Bali kuongea kwake ni kwa kumtaja Allaah na kunyamaza kwake ni kufikiri [uumbaji wa Allaah]. Wakati wa swawm ni wenye thamani zaidi kuliko kuutumia katika maangamizi haya ambao unaathiri thawabu za swawm au kuondosha uhakika wake.

Ee Allaah! Tuongoze njia za amani, tuokoe kutokamana na viza kwenda katika nuru, tuepushe na machafu yenye kuonekana na yaliyofichikana, tubarikie katika masikizi yetu, maono yetu, nguvu zetu, wake zetu na watoto wetu. Tusamehe sisi, wazazi wetu na waislamu wote.

[1] al-Bukhaariy (1894) na Muslim (1151).

[2] al-Bukhaariy (6057). Tazama maneno ya Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah juu ya maana yake katika “Minhaaj-us-Sunnah” (05/197-198).

[3] an-Nasaa´iy (04/167), Ibn Maajah (1639), Ahmad (26/205), Ibn Khuzaymah (03/193) na Ibn Hibbaan (08/409). Cheni ya wapokezi wake ni Swahiyh. Ameisahihisha Ibn Khuzaymah na Ibn Hibbaan. Inatiliwa nguvu na Hadiyth ya Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh).

[4] 02:187

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Mukhtaswar Ahaadiyth-is-Swiyaam, uk. 36-38
  • Imechapishwa: 24/04/2022