07. Kidesuri ni wanawake kuonyesha nyuso na mikono yake

Baada ya Allaah narudisha fadhilah hizi za uzindushi kwa Haafidhw Abul-Hasan bin Qattwaan al-Faasiy (Rahimahu Allaah)[1] na kitabu chake chenye thamani na kisicho na kifani ”an-Nadhwar fiy Ahkaam-in-Nadhwar”. Wakati nilipokuwa naandika utangulizi wa chapa hii mpya wa kitabu nilisoma yafuatayo:

”Desturi tunayokusudia hapa ni ada ya wale walioteremkiwa na Qur-aan, wakaifikisha Shari´ah kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), wakakutana na uzungumzishwaji na wale waliolazimiana na desturi hiyo kutoka kwao. Haihusiani na ada ya wanawake na wengineo wenye kuonyesha miili na sehemu zao za siri zisizotakiwa kuonekana.”[2]

Ibn ´Abbaas, Maswahabah wengine, wanafunzi wa Maswahabah na wafasiri wa Qur-aan wanaashiria desturi hiyo wanapofasiri Aayah:

إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا

“… isipokuwa yale yanayodhihirika… “

Bi maana ile ada ambayo ilikuwa inatambulika na wakakubaliwa kwayo wakati iliposhuka Aayah hiyo. Kwa hivyo haijuzu kupingana na tafsiri yao kwa tafsiri ya Ibn Mas´uud ambaye hakufuatwa na yeyote. Hilo ni kutokana na sababu mbili:

1 – Ametaja nguo kwa kuachia. Hakuna mwingine aliyesema hivo. Tafsiri hiyo inakusanya pia ile nguo ya ndani ambayo yenyewe pia ni mapambo. Kwa hivyo alichokusudia ni ile jilbaab tu ambayo huonekana wakati mwanamke anapotoka nje ya nyumba yake.

2 –  Hata kama baadhi ya watu wenye msimamo mkali wataishabikia tafsiri yake, haiendani na sehemu iliyobaki ya Aayah:

وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ

“Na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao, baba zao, baba za waume wao… ”

Mapambo ya kwanza ndio mapambo ya pili. Kwa mujibu wa kiarabu yanapokaririwa maneno kwa njia ya uhakika basi kunakusudiwa hichohicho. Mambo yakishakuwa hivo basi baba na wengine waliotajwa katika Aayah itafaa kwao kuona ile nguo ya ndani peke yake. Ndio maana Abu Bakr al-Jasswaasw (Rahimahu Allaah) amesema:

”Tafsiri ya Ibn Mas´uud ya kwamba Aayah inakusudia zile nguo haina maana yoyote. Inatambulika kuwa Aayah imetaja mapambo, kinachokusudiwa ni viungo ambavyo mapambo yako juu yake. Je, huoni kuwa inafaa kwake kuonyesha vito vyake mbele ya wanamme muda wa kuwa hakuvivaa? Kwa ajili hiyo ikajulikana makusudio ni vile viungo vya mwili ambavyo mapambo yanakuwa juu yake. Amesema baada ya hapo:

وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ

“Na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao, baba zao, baba za waume wao… ”

Kinachokusudiwa ni viungo vya mwili ambavyo mapambo yanakuwa juu yake. Kuifasiri Aayah kuwa ni zile nguo hakuna maana yoyote, kwa sababu hiyo italeta maana kwamba kutazama nguo zake anapokuwa amezivaa ni kama kuzitazama wakati anapokuwa hakuzivaa.”[3]

[1] adh-Dhahabiy amemweleza kwa kusema:

”Shaykh, Imaam, ´Allaamah, Haafidhw, mkosoaji, msomaji Qur-ana,  Qaadhiy…” (Siyar A´laam-in-Nubalaa’ (22/306))

[2] an-Nadhwar fiy Ahkaam-in-Nadhwar (2/14 – muswada).

[3] Ahkaam-ul-Qur-aan (3/316).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Jilbaab-ul-Mar-ah al-Muslimah, uk. 52-54
  • Imechapishwa: 04/09/2023