Swali: Tunaishi jangwani na watu wote ni mabedui. Wako wanawake ambao wanavaa mavazi yanayofunika ´Awrah lakini hata hivyo ni mafupi na baadhi ya nyakati ni mafupi. Ni kipi mnachowanasihi watu hao?

Jibu: Hapana shaka kwamba kilicho cha wajibu kwa wanawake hawa ni kujisitiri na kujiweka mbali na mambo ya kudhihirisha mapambo na kuonyesha uzuri. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ وَلَا تَبَرَّجْنَ تَبَرُّجَ الْجَاهِلِيَّةِ الْأُولَى

“Tulizaneni majumbani mwenu na wala msijishauwe kwa kuonyesha mapambo kama walivyojishauwa zama za ujahili.”[1]

Wanachuoni wa tafsiri ya Qur-aan wamesema kuwa maana ya “at-Tabarruj” ni kuonyesha mapambo.

Kwa hiyo ni wajibu  kwa mwanamke awe mwenye kujisitiri na mwenye kuvaa Hijaab mbele yake akiweko mwanamume mmoja au wengi ambao sio Mahram wake na ajitenge mbali na fitina, kama alivosema (Ta´ala) pia katika Suurah “al-Ahzaab”:

وَإِذَا سَأَلْتُمُوهُنَّ مَتَاعًا فَاسْأَلُوهُنَّ مِن وَرَاءِ حِجَابٍ ۚ ذَٰلِكُمْ أَطْهَرُ لِقُلُوبِكُمْ وَقُلُوبِهِنَّ

“Mnapowauliza [wake zake] haja yoyote, basi waulizeni nyuma ya pazia. Hivyo ni utwaharifu zaidi kwa nyoyo zenu na nyoyo zao.”[2]

Hilo ni takasifu zaidi kwenye mioyo ya wanaume na mioyo ya wanawake. Mwanamke anapaswa kuvaa Hijaab na asionyeshe mapambo ili asiwafitishe wengine au yeye akafitinishwa. Amesema (Ta´ala):

وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ

“Na waambie waumini wanawake wainamishe macho yao na wahifadhi tupu zao na wala wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa yale yanayodhihirika; hivyo waangushe khimari zao mpaka vifuani mwao. Na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao, baba zao, baba za waume wao, wana wao wa kiume, wana wa kiume wa waume zao, kaka zao, wana wa kiume wa kaka zao, wana wa kiume wa dada zao… “[3]

Amesema (Ta´ala) katika Suurah “al-Ahzaab”:

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاءِ الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا

“Ee Nabii! Waambie wake zako na mabinti zako – na wanawake [wote] wa Waumini – ya kwamba [nje ya nyumbani] wajiteremshie mavazi yao ya juu; hivyo kunapeleka karibu zaidi watambulikane [kuwa ni wanawake wa heshima] na wasiudhiwe. Na Allaah ni Mwingi wa kusamehe, Mwenye kurehemu.”[4]

Jilbaab ni vazi ambalo mwanamke analiweka juu ya kichwa chake na juu ya mwili wake wote juu ya vazi lake la kawaida hali ya kuwa ni ziada ya sitara na kujitenga mbali na fitina. Hivi ndivo anavotakiwa kufanya mwanamke. Ni mamoja ni mwanamke wa shambani au wa mjini. Ni lazima kwake kushikamana na hukumu za Kiislamu, kujitahidi kufunika viungo vyake visivyotakiwa kuonekana na vazi lake liwe kati na kati; si lenye kubana linaloonyesha saizi ya ´Awrah na wala si pana sana lenye kuonyesha ´Awrah. Linatakiwa liwe kati na kati baina ya hayo. Pamoja vilevile na kufunika kichwa, uso na mikono miwili anapokuwa mbele ya mwanaume wa kando, binamu yake, mume wa dada yake au kaka wa mke wake.

Vivyo hivyo ndani ya swalah yake anapaswa kufunika mwili wake wote mbali na uso tu. Sunnah ni yeye kuuacha wazi ndani ya swalah ikiwa pembezoni mwake hakuna mwanaume ambaye si katika Mahram zake. Kuhusu viganja vya mikono akiviacha wazi hakuna neno na akivifunika ndio bora zaidi. Kuhusu miguu yake ni lazima kuifunika ndani ya swalah kwa mujibu wa japo la wanachuoni wengi na wala haijuzu kuiacha wazi. Kuifunika kunakuwa kwa kuiteremshia kanzu, kuvaa soksi na mfano wake wakati anapotaka kuswali.

[1] 33:33

[2] 33:53

[3] 24:31

[4] 33:59

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (05/298) https://binbaz.org.sa/fatwas/1085/%D8%AD%D9%83%D9%85-%D9%84%D8%A8%D8%B3-%D8%A7%D9%84%D9%85%D8%B1%D8%A7%D8%A9-%D8%A7%D9%84%D9%85%D9%84%D8%A7%D8%A8%D8%B3-%D8%A7%D9%84%D9%82%D8%B5%D9%8A%D8%B1%D8%A9-%D8%A7%D9%88-%D8%A7%D9%84%D8%B6%D9%8A%D9%82%D8%A9
  • Imechapishwa: 27/01/2020