Muulizaji: Tumeona waandishi wengi, au wanafunzi ambao wameathirika na mfumo wa wanachuoni wa Hadiyth, wameathirika na mfumo wake.

al-Albaaniy: Mfumo wake ni upi? Ana mfumo?

Muulizaji: Kuathirika kwa mfumo wa kitabu cha Abul-A´laa al-Mawduudiy “al-Adaalah al-Ijtimaaiyyah” na “at-Taswiyr al-Fanniy fiyl-Qur-aan”. (Vyote viwili ni vitabu vya Sayyid Qutwub)

al-Albaaniy: Ule ni mfumo wa uandishi na sio mfumo wa kielimu.

Muulizaji: Kuna mfumo maalum katika Takfiyr kama kuwafanyia Ummah mzima Takfiyr. Hili linapatikana na khaswa katika kitabu “al-Adaalah al-Ijtimaaiyyah”. Hili limetajwa ikiwa ni pamoja na mwandishi wa kitabu “al-I´laam”, az-Zarkiy. Ametaja hili kuhusu mtu huyu na jinsi amvyowafanyia Ummah mzima Takfiyr. Vijana wengi wameathirika na mfumo huu. Vijana wengi hivi sasa wanalingania katika vitabu vyake na maoni yake. Unasemaje juu ya hilo?

al-Albaaniy: Ninaonelea kuwa mtu huyu alikuwa ni mjinga na inatosha. Nini zaidi unachotaka? Kama unataka nimfanyie Takfiyr, mimi sio katika wanaofanya hivo na wewe sio katika wanaofanya hivo. Ninashuhudia na wewe. Inatosheleza kwa Muislamu mwadilifu na asiyekuwa na kundi kumpa kila mwenye haki haki yake. Allaah (Ta´ala) Amesema:

وَلَا تَبْخَسُوا النَّاسَ أَشْيَاءَهُمْ

“Wala msipunje watu vitu vyao.” (07:85)

Mtu huyu alikuwa ni mwandishi tu. Alikuwa ni mwenye shauku juu ya Uislamu aliokuwa akiufahamu. Lakini mtu huyu kwanza hakuwa ni mwanachuoni na kitabu chake “al-Adaalah al-Ijtimaaiyyah” ni katika vitabu vyake vya kwanza. Alipokiandika alikuwa ni mwandishi tu na hakuwa mwanachuoni. Lakini uhakika ni kwamba aliboreka kiasi kikubwa gerezani na kuandika baadhi ya vitabu kwa njia ya ki-Salafiy. Ninaitakidi kuwa gereza inawalea na kuwaamsha baadhi ya watu. Inatosheleza kuandika anwani isemayo “Laa ilaaha illa Allaah – mfumo wa uhai.” Lakini ikiwa hatofautishi kati ya Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah na Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah, haina maana ya kwamba havifahamu na anafanya yote mawili kuwa ni kitu kimoja. Hapana, haina maana ya kwamba sio msomi na mwanachuoni na kwamba hawezi kuleta ibara kwa njia ya Kishari´ah iliyotajwa katika Qur-aan na Sunnah. Hili linatokamana na kwamba hakuwa ni mwanachuoni.

Muulizaji: Je, araddiwe?

al-Albaaniy: Ndio, araddiwe kwa njia ya utulivu na sio kwa hamasa. Araddiwe. Ni wajibu. Radd juu ya kosa haikuwekewa mpaka kwa mtu mmoja au wengi. Inahusiana na kila mwenye kukosea. Kila mwenye kukosea wakati anapofundisha Uislamu kwa Bid´ah na mambo ya kuzua yanayokosa msingi katika Qur-aan, Sunnah, Salaf wetu waliotangulia na maimamu wane, anatakiwa kuraddiwa. Lakini haina maana tufanye uadui dhidi yake au tukasahau kuwa ana mazuri yake. Inatosheleza kuwa ni Muislamu na ni mwandishi wa Kiislamu ambaye anaufahamu Uislamu kwa njia yake na alikufa kwa ajili ya Da´wah yake. Waliomuua ilikuwa ni maadui wa Uislamu. Ama kwamba alikuwa amepinda sana au kidogo katika Uislamu, ninatuhumiwa na al-Ikhwaan al-Muslimuun wa ndani kumfanyia Takfiyr Sayyid Qutwub na kwamba nimewaelekeza baadhi ya watu kwamba anazungumza kwa Wahdat-ul-Wujuud katika baadhi ya vitabu vyake. Wakati huo huo sikanushi ya kwamba alikuwa ni Muislamu na uamsho kwa Uislamu na vijana wa Kiislamu na kwamba alikuwa anataka kuunyoosha Uislamu na nchi ya Kiislamu. Hata hivyo alifanya hilo kwa njia ya kimakosa.

Muulizaji: Je, mtu atahadharishe dhidi ya vitabu vyake?

al-Albaaniy: Watahadharishwe wale wasiokuwa na ufahamu sahihi wa Uislamu.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://alalbany.net/fatawa_view.php?id=6824
  • Imechapishwa: 22/04/2015