Mbora kati ya hawa wanne ni Abu Bakr, kisha ´Umar, kisha ´Uthmaan kisha ´Aliy. Ibn ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Tulikuwa tukitoa mapendekezo kati ya watu katika zama za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambapo tunamchagua Abu Bakr, kisha ´Umar bin al-Khattwaab kisha ´Uthmaan bin ´Affaan.”[1]

Ameipokea al-Bukhaariy.

Abu Daawuud amepokea:

“Tulikuwa tukisema, ilihali Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) bado yuko hai: “Mbora wa Ummah huu baada ya Mitume wake ni Abu Bakr, kisha ´Umar kisha ´Uthmaan.” at-Twabaraaniy amezidisha katika upokezi: “Khabari hizo zinamfikia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wala hazikatai.””[2]

Sikupata tamko la mtunzi wa kitabu linalozidisha kumtaja ´Aliy bin Abiy Twaalib[3].

Mwenye haki zaidi ya uongozi baada ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni Abu Bakr (Radhiya Allaahu ´anh). Kwa sababu yeye ndiye mbora wao na mtangulizi wao katika Uislamu. Jengine Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimtanguliza mbele kuwaswalisha watu. Isitoshe Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) waliafikiana juu ya kumtanguliza na kumpa kiapo cha usikizi na utiifu. Allaah hawezi kuwafanya wakakusanyika juu ya upotofu.

Anayefuatia katika ubora ni ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh). Kwa sababu yeye ndiye Swahabah bora baada ya Abu Bakr. Isitoshe Abu Bakr alimteua kuwa kiongozi wake.

Kisha anayefuatia ni ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh). Hilo ni kutokana na ubora wake na kutangulizwa na watu wa mashauriano. Nao ndio wale waliotajwa katika mashairi haya:

´Aliy, ´Uthmaan, Sa´d na Twalhah

Zubayr, Dhu ´Awf – watu wa mashauriano

Kisha anayefuata ni ´Aliy. Hilo ni kutokana na ubora wake na watu wa zama zake kukusanyika juu yake.

Wanne hawa ndio makhaliyfah waongofu na wanaoongoza ambao Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema juu yao:

“Jilazimieni na Sunnah zangu na Sunnah za makhaliyfah wangu waongofu na wenye kuongoza baada yangu. Ziumeni kwa magego yenu.”[4]

Amesema tena:

“Uongozi baada yangu utakuwa kwa miaka thelathini.”[5]

Ameipokea Ahmad, Abu Daawuud na at-Tirmidhiy. al-Albaaniy amesema:

“Cheni ya wapokezi wake ni nzuri.”

Uongozi wa mwisho ulikuwa wa ´Aliy. Haya yamesemwa na mtunzi wa kitabu. Ni kana kwamba amefanya uongozi wa al-Husayn ni wenye kumfuata baba yake. Kuna uwezekano vilevile hakuzingatia uongozi wake kwa sababu yeye (Radhiya Allaahu ´anh) alijiuzulu.

[1] al-Bukhaariy katika “Fadhwaa-il-us-Swahaabah” (3655).

[2] al-Bukhaariy (3655) na (3697).

[3] Abu Daawuud (4628), at-Tirmidhiy (3707), Ibn Abiy ´Aaswim katika “as-Sunnah” (1190). Cheni ya wapokezi wake ni Swahiyh. Hayo yamesemwa na al-Albaaniy katika “TAkhriyj-us-Sunnah (02/567).

Kuhusu nyongeza iliyokusudiwa na Shaykh al-´Uthaymiyn inayosema:

“Khabari hizo zinamfikia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wala hazikatai.”

Ni nyonegza Swahiyh iliyothibiti kupitia njia nyingi kwa Ibn Abiy ´Aaswim katika “as-Sunnah” (1194, 1995, 1996, 1997), Ahmad (02/14) na wengineo kwa cheni za wapokezi Swahiyh. Rejea “Takhriyj-us-Sunnah” ya Ibn Abiy ´Aaswim (02/568, 569). Vilevile “Fath-ul-Baariy” (07/16, 17).

[4] Abu Daawuud (4607), at-Tirmidiy (2678), Ahmad (4/126-127), ad-Daarimiy (1/44-45), Ibn Maajah (42-43), al-Haakim (1/95) na wengine. Imaam Ibn Hibbaan, Imaam al-Ajjurriy na Imaam al-Albaaniy (Rahimahumu Allaah) wamesema kuwa ni Swahiyh. Tazama “Swahiyh al-Jaamiy´ as-Swaghiyr” (2/344) ya Imaam al-Albaaniy (Rahimahu Allaah).

[5] Abu Daawuud (4646), at-Tirmidhiy (2226), Ahmad (5/221), at-Twabaraaniy katika “al-Kabiyr” (6444), al-Hakiym (3/145) na wengineo.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ta´aliyq mukhtaswar ´alaa Lum´at-il-I´tiqaad, uk. 141-143
  • Imechapishwa: 14/12/2022