98. Kulikuwa kuna faida gani ya Qur-aan na Sunnah?

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

Ikiwa wanafalsafa hawa wenye kujikakama ndio wanazungumza ´Aqiydah ya wajibu ambayo wameijenga juu ya akili  pamoja na kutupilia mbali kile kinachofahamishwa na Qur-aan na Sunnah ima kwa dalili ya wazi kabisa au udhahiri umeonyesha hivo, basi ingelikuwa ni uongofu zaidi na ni manufaa zaidi kuwaacha watu bila ya Qur-aan na Sunnah. Bali kutokana na msingi wa ´Aqiydah yao uwepo wa Qur-aan na Sunnah ilikuwa ni madhara matupu.

MAELEZO

Ikiwa haki iko pamoja na hawa Jahmiyyah na wadogo wao, wanaosema kuwa Allaah hana majina wala sifa na kwamba Yeye ni dhati tupu, sambamba na hayo ndani ya Qur-aan na Sunnah kumejaa majina na sifa za Allaah, basi ingelikuwa bora zaidi ni kuwaacha watu bila Qur-aan na Sunnah. Kwa sababu kwa mujibu wa fikira hii ni kuwa Mitume hawakuja na uongofu wowote – na kwamba uongofu uko katika maneno ya watu hawa. Basi kuna faida gani ya vitabu vya kiungu? Kuna faida gani ya kutumilizwa Mitume? Ingelikuwa ni bora kuwaacha watu wakazitegemea akili na fikira zao. Haya ndivo inavopelekea ´Aqiydah yao. ´Aqiydah yao inapelekea kwamba ulimwengu hauna haja ya Mtume wala Kitabu, kwa sababu akili na fikira zao zinawatosha. Bali uwepo wa Qur-aan na Sunnah unawadhuru tu watu kwa sababu, kwa mujibu wa ´Aqiydah yao, vinawapotosha. Kwa mujibu wa watu hawa ni kuwa Qur-aan na Sunnah haikusema ´Aqiydah sahihi waziwazi. Kwa hivyo Qur-aan na Sunnah vimekuja kupotosha, na kwamba haki ni katika kule kuzifuata akili, watu wa mijadala, wanafalsafa na watu wa mantiki.

  • Muhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaa al-Hamawiyyah, uk. 143-144
  • Imechapishwa: 01/09/2024