Miongoni mwa sifa za kipekee za kumi la mwisho ni kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akifanya I´tikaaf ndani yake. I´tikaaf ni kule kulazimiana na msikiti kwa ajili ya kupata muda wa kumtii Allaah (´Azza wa Jall). Ni Sunnah iliyothibiti kwa mujibu wa Qur-aan na Sunnah. Allaah (´Azza wa Jall) amesema:
وَلَا تُبَاشِرُوهُنَّ وَأَنتُمْ عَاكِفُونَ فِي الْمَسَاجِدِ
“Na wala msichanganyike nao hali ya kuwa nyinyi ni wenye kukaa I’tikaaf misikitini.”[1]
Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifanya I´tikaaf na Maswahabah wakafanya I´tikaaf pamoja naye na baada yake. Abu Sa´iyd al-Khudriy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia:
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikaa I´tikaaf katika yale masiku kumi ya mwanzo ya Ramadhaan, kisha akakaa I´tikaaf katika masiku kumi ya katikati kisha akasema: “Nilifanya I´tikaaf katika kumi la mwanzo nikiutafuta usiku huu, kisha nikafanya katika kumi la katikati. Halafu nikajiwa na kuambiwa: “Unapatikana katika lile kumi la mwisho. Kwa hivyo yule anayependa miongoni mwenu kufanya I´tikaaf basi afanye I´tikaaf.”
Ameipokea Muslim.
al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) aliyesimulia:
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akikaa I´tikaaf katika kumi la mwisho la Ramadhaa mpaka alipofishwa na Allaah (´Azza wa Jall) kisha wakafanya I´tikaaf wakeze baada yake.”
al-Bukhaariy amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwake huyohuyo tena aliyesimulia:
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akifanya I´tikaaf katika kila Ramadhaan siku kumi. Ulipofika ule mwaka aliyofishwa akakaa I´tikaaf siku ishirini.”
Anas (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia:
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akifanya I´tikaaf zile siku kumi za mwisho za Ramadhaan. Akaacha kukaa I´tikaaf kwa muda wa mwaka mzima. Ulipofika mwaka uliofuata akakaa I´tikaaf siku ishirini.”
Ameipokea Ahmad na at-Tirmidhiy ambaye ameisahihisha.
´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia:
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa anapotaka kukaa I´tikaaf anaswali Fajr kisha ndio anaingia mahali pake pa I´tikaaf. ´Aaishah akamuomba idhini na akampa idhini na kumtengenezea hema. Hafswah akamwambia ´Aaishah amuombee idhini na akafanya hivo na akamtengenezea hema. Wakati Zaynab alipoona hivo akaamrisha afanyiwe hema ambapo akatengenezewa. Wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipoyaona mahema hayo akasema: “Nini hivi?” Wakasema: “Ni jengo la ´Aaishah, Hafswah na Zaynab.” Ndipo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Kipi kimekupelekeeni kufanya hivo; yaondosheni nisiyaone.” Yakaondoshwa na I´tikaaf ikaachwa kufanywa ndani ya Ramadhaan mpaka akafanya I´tikaaf katika kumi la mwanzo la Shawwaal.”
Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim katika upokezi mmoja.
Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:
“Sijui kutoka kwa mwanachuoni yeyote tofauti ya kwamba I´tikaaf ni Sunnah.”
[1] 02:187
- Muhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
- Tarjama: Firqatunnajia.com
- Marejeo: Majaalis Shahr Ramadhwaan, uk. 155-157
- Imechapishwa: 10/03/2024
Mshirikishe mwenzako:
- Click to share on Telegram (Opens in new window)
- Click to share on WhatsApp (Opens in new window)
- Click to print (Opens in new window)
- Click to email a link to a friend (Opens in new window)
- Click to share on Facebook (Opens in new window)
- Click to share on Twitter (Opens in new window)
- Click to share on Pocket (Opens in new window)