Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

67 – Allaah ametakasika kutokamana na mipaka, malengo (الغايات), nguzo (الأركان), viungo vya mwili na zana (الأدوات).

MAELEZO

Haya matamshi yametajwa kwa ujumla. Ikiwa anakusudia mipaka iliyoumbwa, basi Allaah ametakasika kutokamana na mipaka na kukita ndani ya viumbe. Na ikiwa anakusudia mipaka ambayo haikuumbwa na ujuu, ni kitu kilichothibiti kwa Allaah (Jalla wa ´Alaa) kwamba yuko juu. Allaah hatakaswi kutokana na ujuu, kwa sababu ni kweli Yuko juu. Katika hali hii mipaka wala pande zilizoumbwa sio mambo muhimu.

Malengo ni tamko la ujumla pia; inaweza kuwa na maana ya haki na inaweza pia kuwa na maana ya batili. Ikiwa kwa neno malengo (الغايات) anakusudia hekima ya Allaah kuwaumba viumbe na kwamba amewaumba kwa malengo, ni kitu cha haki. Lakini inasemwa hekima na si (الغايات). Allaah (Ta´ala) amesema:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ مَا أُرِيدُ مِنْهُم مِّن رِّزْقٍ وَمَا أُرِيدُ أَن يُطْعِمُونِ

“Sikuumba majini na wana Aadam isipokuwa waniabudu. Sitaki kutoka kwao riziki yoyote na wala Sitaki wanilishe.”[1]

Na kama anakusudia kuwahitajia viumbe, ni ukanushaji sahihi. Allaah (´Azza wa Jall) hakuwaumba viumbe kwa sababu anawahitaji, kwa sababu Yeye ni mkwasi kutokamana na walimwengu.

Nguzo, viungo vya mwili na zana ni matamshi ya ujumla. Ikiwa anakusudia sifa za Allaah za kidhati kama mfano wa uso na mikono, ni haki na kuzikanusha ni batili. Na kama anakusudia kukanusha viungo vya mwili vinavyofanana na viungo vya mwili vya viumbe, basi ni kweli kwamba Allaah ametakasika kutokamana na vitu hivyo. Kwa msemo mwingine matamshi hayo yanaweza kupambanuliwa ifuatavyo:

1 – Ikiwa mtunzi anakusudia kukanusha sifa za Allaah (Ta´ala) za kidhati kama vile uso na mikono na sifa nyinginezo za kidhati zilizothibiti Kwake (Subhaanahu wa Ta´ala), ni batili.

2 – Ikiwa mtunzi anakusudia kumtakasa Allaah kutokamana na kufanana na viungo vya mwili vya viumbe, ni haki. Allaah ametakasika kutokamana na vitu hivyo. Kwa sababu hakuna kiumbe chochote kinachofanana Naye, si katika dhati, majina wala sifa Zake.

Matamshi yaliyotajwa na mtunzi yametajwa kwa njia ya ujumla. Hata hivyo yanatakiwa kufasiriwa kwa njia sahihi kwa sababu (Rahimahu Allaah) alikuwa ni katika Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah na alikuwa ni katika maimamu. Haiwezekani akawa amekusudia maana mbaya. Anachokusudia ni maana nzuri. Ndio maana ingelikuwa vyema kama angeyapambanua na kuyabainisha na asiyataje kwa ujamla namna hii.

[1] 51:56

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Mukhtaswarah ´alaal-´Aqiydah at-Twahaawiyyah, uk. 86-88
  • Imechapishwa: 23/01/2023