Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

66 – Yule asiyeacha ukanushaji na ufananishaji, atapotea na wala hatopatia matakaso yoyote. Kwani hakika Mola wetu (Jalla wa ´Alaa) ni Mwenye kusifika kwa sifa za upweke. Hakuna kiumbe chochote kama Yeye.

MAELEZO

Kama tulivyotangulia kusema ni lazima kuwa kati na kati, kati ya kukanusha na kati ya kufananisha. Upande mmoja mtu hatakiwi kuchupa mipaka katika kumtakasa Allaah mpaka mwishowe ikampelekea kumkanushia Allaah sifa Zake, kama walivofanya Mu´attwilah. Upande mwingine mtu hatakiwi kuchupa mipaka katika kuthibitisha mpaka akamfananisha Allaah na viumbe Wake. Mtu anatakiwa kuwa wastani; amthibitishie Allaah yale Yeye Mwenyewe na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wamemthibitishia pasi na kushabihisha wala kumpigia mfano, pasi na kukanusha wala kumfanyia namna. Hii ndio njia ilionyooka na ya kati na kati. Hakuna anayeshabihiana na Allaah (Sunhaanah), hakuna anayelingana Naye wala hakuna aliye sawa Naye.

Allaah amepwekeka katika sifa Zake na hana mshirika yeyote. Hana mshirika inapokuja katika uola Wake, kupwekeka Kwake katika kuabudiwa wala katika majina na sifa Zake. Yeye ni Mmoja wa pekee katika sifa zote hizi.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Mukhtaswarah ´alaal-´Aqiydah at-Twahaawiyyah, uk. 85-86
  • Imechapishwa: 23/01/2023