75. ´Aqiydah ya Ibn ´Abdil-Wahhaab juu ya wakeze Mtume

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Nawatakia radhi mama wa waumini waliotwahirishwa na kila ovu.

MAELEZO

Shaykh anawatakia radhi mama wa waumini; wakeze Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wao ni mama wa waumini katika cheo na heshima na si katika nasaba. Inahusiana katika cheo na heshima. Vilevile Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni baba wa waumini katika cheo na si katika nasaba:

مَّا كَانَ مُحَمَّدٌ أَبَا أَحَدٍ مِّن رِّجَالِكُمْ

“Hakuwa Muhammad baba wa yeyote miongoni mwa wanaume wenu.”[1]

Bi maana katika nasaba. Kwa sababu hapa wanajibiwa wale wenye kusema kuwa Zayd bin al-Haarithah ni mwana wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ndipo Allaah akakataa hili. Lakini hiyo haina maana kwamba si baba yao katika cheo katika kutukuzwa. Amesema (Ta´ala):

وَأَزْوَاجُهُ أُمَّهَاتُهُمْ

“Wake zake ni mama zao.”[2]

Katika kisomo kingine:

وهو أب لهم

 “Na yeye ni baba yao.”

Bi maana katika cheo na kutukuzwa.

Kuhusu wao kwamba ni mama wa waumini ni kwa andiko la Qur-aan linalosomwa mpaka siku ya Qiyaamah:

وَأَزْوَاجُهُ أُمَّهَاتُهُمْ

“Wake zake ni mama zao.”

Hiyo ina maana kwamba haijuzu kwa yeyote kuwaoa baada ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa sababu wao ndio wakeze Peponi:

وَمَا كَانَ لَكُمْ أَن تُؤْذُوا رَسُولَ اللَّـهِ وَلَا أَن تَنكِحُوا أَزْوَاجَهُ مِن بَعْدِهِ أَبَدًا ۚ إِنَّ ذَٰلِكُمْ كَانَ عِندَ اللَّـهِ عَظِيمًا

“Haiwapasi kwenu kumuudhi Mtume wa Allaah na wala kuwaoa wake zake baada yake kamwe. Hakika jambo hilo mbele ya Allaah ni kubwa mno.”[3]

Wao wameharamishwa juu ya Ummah kwa sababu ndio wakeze dunaini na Aakhirah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Inatosha hiyo kuwa ni utukufu kwao. Jengine ni kwamba wamebeba elimu na Shari´ah waliyowafikishia Ummah. Wameibeba kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wana fadhilah na utukufu (Radhiya Allaahu ´anhunna).

[1] 33:40

[2] 33:06

[3] 33:53

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh ´Aqiydat-il-Imaam Mujaddid Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab, uk. 109-110
  • Imechapishwa: 19/05/2021