60- Ni haramu kuwaswalia, kuwaombea msamaha na rehema makafiri na wanafiki[1]. Hilo ni kutokana na maneno ya Allaah (Tabaarak wa Ta´ala):

وَلَا تُصَلِّ عَلَىٰ أَحَدٍ مِّنْهُم مَّاتَ أَبَدًا وَلَا تَقُمْ عَلَىٰ قَبْرِهِ ۖ إِنَّهُمْ كَفَرُوا بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَمَاتُوا وَهُمْ فَاسِقُونَ

”Wala kamwe usimswalie yeyote miongoni mwao akifa na wala usisimame kaburini kwake [kwa ajili ya kumuombea]; kwani hakika wao wamemkanusha Allaah na Mtume Wake na wakafa hali wao ni mafasiki.”[2]

Sababu ya kuteremka kwa Aayah ni yale aliyopokea ´Abdullaah bin ´Umar na baba yake, na mtiririko ni wake, ambaye amesema:

“Wakati alipofariki ´Abdullaah bin Ubay bin Saluul Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliitwa kwa ajili yake ili amswalie. Pindi Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliposimama nikamsogelea [mpaka nikamsimamia usawa na kifua chake] [nikamshika nguo zake] nikasema: “Ee Mtume wa Allaah! Unamswalia [adui wa Allaah?] Ibn Ubay bin Saluul ilihali amesema hivi na hivi siku fulani na fulani? Nikawa namhesabia maneno yake[3]. [Je, Allaah hakukukataza kuwaswalia wanafiki?]

اسْتَغْفِرْ لَهُمْ أَوْ لَا تَسْتَغْفِرْ لَهُمْ إِن تَسْتَغْفِرْ لَهُمْ سَبْعِينَ مَرَّةً فَلَن يَغْفِرَ اللَّـهُ لَهُمْ

[“Waombee msamaha au usiwaombee msamaha, hata ukiwaombea msamaha mara sabini, basi Allaah hatowasamehe.”[4]]

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akatabasamu na akasema:

“Nimepewa khiyari, ee ´Umar! Pindi alipokithirisha akasema: “Nimepewa khiyari nikachagua hilo. [Nimeambiwa:

اسْتَغْفِرْ لَهُمْ أَوْ لَا تَسْتَغْفِرْ لَهُمْ إِن تَسْتَغْفِرْ لَهُمْ سَبْعِينَ مَرَّةً فَلَن يَغْفِرَ اللَّـهُ لَهُمْ

[“Waombee msamaha au usiwaombee msamaha, hata ukiwaombea msamaha mara sabini, basi Allaah hatowasamehe.”]

Lau ningejua kuwa endapo nitazidisha mara sabini atasamehewa basi ningezidisha juu yake. [Akasema: “Hakika yeye ni mnafiki[5]] Akasema: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamswalia[6]. [na tukaswali pamoja naye] [akatembea (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pamoja naye na akasimama juu ya kaburi lake mpaka alipomaliza kuzikwa.] Kisha akaondoka na hakukaa isipokuwa kitambo kidogo mpaka kukateremka Aayah ya kujitenga mbali:

وَلَا تُصَلِّ عَلَىٰ أَحَدٍ مِّنْهُم مَّاتَ أَبَدًا

”Wala kamwe usimswalie yeyote miongoni mwao akifa… “

mpaka:

وَهُمْ فَاسِقُونَ

“… hali wao ni mafasiki.”

[Amesema: “Baada ya hapo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakumswalia mnafiki na wala hakusimama kwenye kaburi lake mpaka alipomfisha Allaah]. Baadaye nikaja kushangazwa na ujasiri wangu kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) siku ile]. Allaah na Mtume Wake ndio wanajua zaidi.”

Ameipokea al-Bukhaariy (03/177-08/280), an-Nasaa´iy (01/279), at-Tirmidhiy (03/117,118), Ahmad (nambari. 95) kutoka kwa ´Umar. Ziada ya kwanza, ya pili, ya tatu, ya tano, ya nane na ya tisa ni ya Ahmad na at-Tirmidhiy ambaye ameisahihisha. Ziada za mwisho ni za al-Bukhaariy isipokuwa ya sita ambayo ni ya Muslim na ya al-Bukhaariy kupitia kwa Ibn ´Umar. Ziada ya pili ni ya at-Twabariy kama ilivyo katika “al-Fath”.

Kisha akaitoa al-Bukhaariy (07/268,270 – 10/218), Muslim (07/116 – 08/120, 121), an-Nasaa´iy (01/269), at-Tirmidhiy (03/118, 119), Ibn Maajah (01/464, 465), al-Bayhaqiy (03/402), Ahmad (4680) kupitia kwa Ibn ´Umar. Juu yake kuna katika ziada ya pili na ya sita.

al-Musayyib bin Hazn (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza:

“Wakati Abu Twaalib alipotaka kukata roho alikuja Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamkuta Abu Jahl, ´Abdullaah bin Abiy Umayyah na al-Mughiyrah. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Ee ami yangu! [Hakika wewe ni mtu mwenye haki kubwa zaidi kwangu na mwenye wema na msaada zaidi kwangu. Hakika wewe una haki kubwa sana kwangu kuliko baba yangu. [Sema ´hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Allaah`. Ni neno ambalo nitakutolea ushahidi kwalo mbele ya Allaah.” Abu Jahl na ´Abdullaah bin Abiy Umayyah wakasema: “Ee Abu Twaalib! Hivi kweli unataka kuipa mgongo dini ya ´Abdul-Muttwalib? Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaendelea kumtangazia na akimrudia na [wao[7]] wakimrudia maneno hayo. Mpaka dakika ya mwisho Abu Jahl akasema: “Yeye yuko juu ya dini ya ´Abdul-Muttwalib na akakataa kutamka ´hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Allaah`[8]. [Akasema: “Lau si kuchelea kusakamwa na Quraysh – wakasema kwamba kilichompelekea katika hayo ni dhiki – basi ningekufurahisha! Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Ninaapa kwa Allaah kwamba nitakuombea msamaha muda wa kuwa sijakatazwa juu yako. Waislamu wakawa wanawaombea msamaha wafu wao waliokufa wakiwa ni washirikina] Ndipo Allaah (´Azza wa Jall) akateremsha:

مَا كَانَ لِلنَّبِيِّ وَالَّذِينَ آمَنُوا أَن يَسْتَغْفِرُوا لِلْمُشْرِكِينَ وَلَوْ كَانُوا أُولِي قُرْبَىٰ مِن بَعْدِ مَا تَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُمْ أَصْحَابُ الْجَحِيمِ

“Haimpasi Nabii na wale walioamini kuwaombea msamaha washirikina japokuwa ni jamaa zao wa karibu baada ya kuwabainikia kwamba wao ni watu wa Motoni.” (09:113)

Allaah akaiteremsha pia juu ya Abu Twaalib. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

إِنَّكَ لَا تَهْدِي مَنْ أَحْبَبْتَ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يَهْدِي مَن يَشَاءُ ۚ وَهُوَ أَعْلَمُ بِالْمُهْتَدِينَ

”Hakika wewe huwezi kumwongoza umpendaye, lakini Allaah humwongoza amtakaye; Naye ndiye mjuzi zaidi ya waongokao.”[9]

al-Bukhaariy (03/173 – 07/154 – 08/274, 410, 411), Muslim, an-Nasaa´iy (01/286), Ahmad (05/433), Ibn Jariyr katika “Tafsiyr” yake (11/27) na mtiririko ni wake na pia Muslim. Ziada ya pili ni yake katika baadhi ya misingi kama alivyotaja al-Haafidhw kutoka kwa al-Qurtwubiy. Upokezi wa al-Bukhaariy na wengineo zinaitolea ushahidi kwa maana yake.

Pia kisa kimepokelewa katika Hadiyth ya Abu Hurayrah kwa ufupi kwa Muslim, at-Tirmidhiy (04//159) ambaye ameonelea kuwa ni nzuri. Kwa wawili hao ipo hiyo ziada ya tatu, al-Haakim (02/335, 336) ambaye ameisahihisha na adh-Dhahabiy akaafikiana naye. Kwao ipo ziada ya kwanza ambayo pia iko kwa Ibn Jariyr kutoka katika Hadiyth ya Sa´iyd bin al-Musayyib ambayo katika cheni ya wapokezi wake kuna Swahabah anayekosekana. Lakini hata hivyo inayo hukumu ya kuunganika kwa cheni ya wapokezi wake kwa sababu yeye ndiye ameipokea Hadiyth kutoka kwa al-Musayyib bin al-Hazn ambaye ni baba yake.

Kisa kimepokelewa pia kupitia kwa Jaabir. Ameipokea al-Haakim pia ambaye ameisahihisha na adh-Dhahabiy akaafikiana naye.

Ipo ziada ya nne ambayo iko kwa Ibn Jariyr ambayo kuna Swahabah anayekosekana katika cheni ya wapokezi wake kutoka kwa Mujaahid, na kutoka kwa ´Amr bin Diynaar.

´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Nilimsikia bwana mmoja akiwaombea msamaha wazazi wake wawili ilihali ni washiirkina ambapo nikasema: “Hivi unawaombea msamaha wazazi wako ilihali ni washirikina?” Akasema: “Je, Ibraahiym si alimuombea msamaha baba yake ilihali ni mshirikina?” Nikamtajia kitendo hicho Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ndipo kukateremshwa:

مَا كَانَ لِلنَّبِيِّ وَالَّذِينَ آمَنُوا أَن يَسْتَغْفِرُوا لِلْمُشْرِكِينَ وَلَوْ كَانُوا أُولِي قُرْبَىٰ مِن بَعْدِ مَا تَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُمْ أَصْحَابُ الْجَحِيمِ

“Haimpasi Nabii na wale walioamini kuwaombea msamaha washirikina japokuwa ni jamaa zao wa karibu baada ya kuwabainikia kwamba wao ni watu wa Motoni.” (09:113)

Ameipokea an-Nasaa´iy (01/286), at-Tirmidhiy (04/120) ambaye ameifanya kuwa nzuri. Pia ameipokea Ibn Jariyr (11/28), al-Haakim (02/335), Ahmad (771, 1085) na mtiririko ni wake. Cheni ya wapokezi wake ni nzuri. al-Haakim amesema:

“Ni yenye cheni ya wapokezi Swahiyh” na adh-Dhahabiy ameafikiana naye.

Msamaha huu ndio ule ambao umeelezewa na Allaah mwishoni mwa Suurah “Ibraahiym”  juu yake:

رَبَّنَا اغْفِرْ لِي وَلِوَالِدَيَّ وَلِلْمُؤْمِنِينَ يَوْمَ يَقُومُ الْحِسَابُ

“Mola wetu! Nisamehe na wazazi wangu wawili na waumini siku itakayosimama hesabu.” (14:41)

Wanachuoni wa tafsiri ya Qur-aan wametaja kwamba du´aa hii kutoka kwake ilikuwa baada ya kufariki kwa baba yake na baada ya kuhama kwake kwenda Makkah ili hilo liende sawa na mtiririko wa Aayah ambazo zimekuja mwishoni mwake hiyo Aayah iliyotajwa hapo. Kujengea juu ya haya kule kubainikiwa kwake kulikotajwa katika Aayah ya kumuombea msamaha kunatakikana pia kuwe baada ya kufariki kwa baba yake. Hayo yalikuwa kwa kutambulishwa na Allaah. Ibn Abiy Haatim ametaja, kwa cheni ya wapokezi Swahiyh, kama alivosema as-Suyuutwiy katika “al-Fataawaa” (02/419) kutoka kwa Ibn ´Abbaas ambaye amesimulia:

“Ibraahiym aliendelea kumuombea baba yake mpaka alipokufa. Alipokufa ndipo ikabainika kwake kwamba ni adui wa Allaah. Kuanzia hapo hakumuombea tena msamaha.”

an-Nawawiy (Rahimahu Allaah) amesema katika “al-Majmuu´” (05/144, 258):

“Kumswalia kafiri na kumuombea du´aa ya msamaha ni haramu kwa andiko la Qur-aan na kwa maafikiano.”

Kutokana na hayo utatambua makosa ya baadhi ya waislamu hii leo ambapo wanawaombea du´aa ya rehema na kuwaombea radhi baadhi ya makafiri. Hayo yanafanyika kwa wingi kutoka kwa baadhi ya watu wa magazeti na majarida. Hakika mimi nimemsikia mmoja katika waarabu wanaojulikana akimuombea rehema Staaliyn, ambaye ni mkomunisti ambaye yeye na madhehebu yake, ni katika maadui wakubwa zaidi dhidi ya dini. Hayo aliyafanya katika kalima ya raisi ambaye punde ameashiriwa katika mnasaba wa kufa kwa mtu aliyetajwa ambayo ilirushwa redioni. Hakuna mshangao kutokana na mtu kwa sababu pengine hukumu kama hii inaweza kuwa si yenye kutambulika kwake. Kilicho mshangao ni kwa baadhi ya walinganizi wa Kiislamu kutumbukia katika jambo kama hilo ambapo amesema katika kijitabu chake:

“Allaah amrehemu Bernard…. “

Nimepewa khabari na baadhi ya watu ninaowaamini kwamba mmoja katika Mashaykh alikuwa akimswalia mmoja katika wanaokufa katika pote la Ismaa´iyliyyah Baatwiniyyah pamoja na kwamba yeye anaonelea kuwa sio waislamu. Kwa sababu watu hao hawaonelei kuwepo kwa swalah, hajj na wanamwabudu mtu. Pamoja na hayo anawaswalia kwa njia ya unafiki na kujikombakomba kwao. Allaah ndiye mwenye kushtakiwa na ndiye mwenye kutakwa msaada.”

[1] Ni wale wanaoficha ukafiri na wanadhihirisha Uislamu. Si vyenginevyo ukafiri wao unabainika kutokana na yale maneno yao pindi wanazitia kasoro baadhi ya hukumu za Kishari´ah, kuonyesha kuwa ni mbaya na wakidai kuwa zinapingana na akili na zile tararibu za watu walizonazo. Hakika Mola wetu (Tabaarak wa Ta´ala) ameashiria juu ya uhakika huu pale aliposema:

أَمْ حَسِبَ الَّذِينَ فِي قُلُوبِهِم مَّرَضٌ أَن لَّن يُخْرِجَ اللَّـهُ أَضْغَانَهُمْ وَلَوْ نَشَاءُ لَأَرَيْنَاكَهُمْ فَلَعَرَفْتَهُم بِسِيمَاهُمْ ۚ وَلَتَعْرِفَنَّهُمْ فِي لَحْنِ الْقَوْلِ ۚ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ أَعْمَالَكُمْ

”Je, wanadhania wale ambao nyoyoni mwao mna maradhi kwamba Allaah hatafichua chuki zao? Na lau Tungelitaka, basi tungelikuonyesha hao, pasi na shaka ungeliwatambua kwa alama zao na pasi na shaka utawatambua kwa namna ya msemo wao. Na Allaah anajua matendo yao.” (47:29-30)

Mfano wa wanafiki hawa ni wengi katika zama zetu hizi. Allaah ndiye mwenye kutakwa msaada.

[2] 09:84

[3] Anaashiria kwa hayo katika mfano wa maneno Yake:

لَا تُنفِقُوا عَلَىٰ مَنْ عِندَ رَسُولِ اللَّـهِ حَتَّىٰ يَنفَضُّوا

”Msitoe mali kwa ajili ya walioko kwa Mtume wa Allaah mpaka watokomee mbali.” (63:07)

Vilevile maneno Yake:

يَقُولُونَ لَئِن رَّجَعْنَا إِلَى الْمَدِينَةِ لَيُخْرِجَنَّ الْأَعَزُّ مِنْهَا الْأَذَلَّ

”Wanasema: ”Tutakaporudi al-Madiynah, basi mtukufu zaidi atamfukuza aliye dhalili.” (63:08)

[4] 09:80

[5] al-Haafidhw Ibn Hajar (Rahimahu Allaah) amesema katika ”al-Fath” (08/270):

”´Umar alikata kauli kwamba ni mnafiki kutokana na yale yenye kuonekana katika hali zake. Si vinginevyo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakuyachukua maneno yake na badala yake akamswalia ili kuendana naye juu ya hukumu ya Uislamu, kutendea kazi uinje wa hukumu, kumkirimu mtoto wake ambaye uzuri wake ulikuwa ukifahamika, pia kuwavuta jamaa zake na pia kwa ajili ya kuzuia madhara. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mwanzoni mwa jambo alikuwa akivumilia maudhi ya washirikina, akisamehe na kuachilia bure. Kisha akaamrishwa kuwapiga vita washirikina. Ndipo msamaha kwake kukaendelea kwa yule mwenye kudhihirisha Uislamu ijapo undani wake ni wenye kupingana na jambo hilo kwa ajili ya manufaa ya kuunga na kutowakimbiza watu mbali naye. Kwa ajili hiyo amesema:

“Watu wasije kuzungumza kuwa Muhammad anawaua Maswahabah zake.”

Wakati ulipofunguliwa mji wa Makkah,washirikina wakaingia ndani ya Uislamu na  makafiri wakawa wachache na wanyonge ndipo akaamrishwa kuwafichua wanafiki na kuwachukulia juu ya hukumu ya nguvu ya haki na khaswa hayo yalikuwa kabla ya kuteremka kwa makatazo ya wazi kuwaswalia wanafiki na mengineyo ambayo aliamrishwa katika kuwafichukua. Kwa pitisho hili utata unakuwa ni wenye kuondoka kutokana na yale yaliyotokea katika kisa hiki kwa himdi za Allaah (Ta´ala).

[6] Alimswalia baada ya kuingizwa ndani ya shimo lake na akatolewa ndani yake kwa amri yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Alimvika kanzu yake kama itavyokuja katika masuala ya 94.

[7] Bi maana Abu Jahl na Ibn Abiy Umayyah.

[8] Katika Hadiyth hii kuna kwamba sababu ya kuteremka kwa Aayah sio sababu iliyotajwa katika Hadiyth ilio kabla yake. Hakuna kugongana kati ya mawili hayo kwa kuwa inafaa kuwepo sababu zaidi ya moja ya kuteremka kwa Aayah. Hayo yametokea katika Aayah nyingi tu. al-Haafidhw ameyasapoti haya katika “al-Fath” (08/412).

[9] 28:56

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 120-124
  • Imechapishwa: 13/08/2020