53. Swawm na swalah ambao mchana au usiku wao unarefuka sana

Swali 53: Kipi wafanye wale ambao mchana wao unakuwa kwa masaa ishirini na moja? Je, wakadirie yale masaa ya funga? Kipi wafanye wale ambao mchana wao unakuwa mfupi sana? Kadhalika ambao mchana wao unaendelea kwa miezi sita na usiku wao unaendelea kwa miezi sita[1]?

Jibu: Wale ambao wana usiku na mchana kwa muda wa masaa ishirini na nne basi wanatakiwa kufunga katika kile kipindi cha mchana. Ni mamoja mchana ukawa mfupi au mrefu. Hayo yatawatosha na himdi zote njema anastahiki Allaah. Haijalishi kitu hata kama mchana wao ni mfupi. Ama kuhusu wale ambao mchana na usiku wao unaendelea kama mfano miezi sita basi wanatakiwa kukadiria swawm na swalah viwango vyake, kama alivyoamrisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika siku ya ad-Dajjaal ambayo itakuwa ni kama mwaka, vivyo hivyo ile siku ambayo itakuwa kama mwezi na wiki. Basi watatakiwa kukadiria swalah kiwango chake.

Baraza la wanazuoni wakuu Saudi Arabia wamelidurusu suala hili na wakatoa  maamuzi nambari. 61 tarehe 12/04/1398 kama ifuatavyo:

:الحمد لله، والصلاة والسلام على رسوله وآله وصحبه وبعد

Imewasilishwa barua kwa baraza la wanazuoni wakuu katika kikao cha kumi na mbili kilichofanyika Riyaadh katika siku za mwanzo za mwezi wa Rabiy´ al-Aakhir katika mwaka wa 1398 kutoka kwa muheshimiwa na mkuu wa jumuiya ya Raabitwat-ul-´Aalams-il-Islaamiy huko Makkah al-Mukarramah nambari. 555 tarehe 16/01/1398 inayojumuisha yale yaliyoelezwa katika mazungumzo ya raisi wa jumuiya ya Kiislamu ilioko katika mji wa Malmö nchini Uswidi ambayo inatufahimisha kwamba nchi za Skandinavia inarefuka michana yake wakati wa msimu wa joto na inafupika wakati wa msimu wa baridi kutokana na nafasi yake ya kijiografia kama ambavo mikoa yake ya kaskazini wakati wa kiangazi jua halizami kabisa na kinyume chake wakati wa majira ya baridi. Waislamu wanaoishi humo wanauliza namna ya kukata swawm na kujizuilia katika Ramadhaan na vivyo hivyo namna ya kudhibiti nyakati za swalah katika miji hii. Sambamba na hilo muheshimiwa anatarajia kutolewe fatwa juu ya hayo ili awape zawadi kwayo.”

Baraza liliwasilishiwa yale yaliyotayarishwa na al-Lajnah ad-Daaimah lil-Buhuuth-il-´Ilmiyyah wal-Iftaah na tuna mengine ya kusema kuhusu wanazuoni juu ya maudhui haya. Baada ya kuyasoma, kuyadurusu na kuyajadili kikao kimepitisha yafuatayo:

1 – Ambaye anaishi katika mji ambao kunapambanuka usiku kutokamana na mchana kwa kuchomoza alfajiri na kuzama kwa jua, ingawa mchana wake unarefuka sana wakati wa majira ya joto na unafupika wakati wa majira ya baridi, basi analazimika kuswali zile swalah tano ndani ya nyakati zake zinazotambulika ki-Shari´ah. Hayo ni kutokana na ueneaji wa maneno Yake (Ta´ala):

أَقِمِ الصَّلَاةَ لِدُلُوكِ الشَّمْسِ إِلَىٰ غَسَقِ اللَّيْلِ وَقُرْآنَ الْفَجْرِ ۖ إِنَّ قُرْآنَ الْفَجْرِ كَانَ مَشْهُودًا

“Simamisha swalah jua linapopinduka hadi kiza cha usiku na Qur-aan ya alfajiri. Hakika Qur-aan ya alfajiri ni yenye kushuhudiwa.”[2]

إِنَّ الصَّلَاةَ كَانَتْ عَلَى الْمُؤْمِنِينَ كِتَابًا مَّوْقُوتًا

“Kwani hakika swalah kwa waumini ni fardhi iliyowekwa nyakati maalum.”[3]

Vilevile kutokana na yale yaliyothibiti kutoka kwa Buraydah (Radhiya Allaahu ´anh) kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba bwana mmoja alimuuliza kuhusu nyakati za swalah ambapo akamwambia:

“Swali pamoja nasi.” – bi maana siku hizi mbili – “Wakati jua lilipopondoka akamwamrisha Bilaal ambapo akaadhini, kisha akamwamrisha akasimamisha Dhuhr, kisha akamwamrisha akasimamisha ´Aswr ilihali jua limenyanyuka juu jeupe pepe, kisha akamwamrisha akasimamisha Maghrib wakati jua lilipozama, kisha akamwamrisha akasimamisha ´Ishaa wakati yalipozama mawingu [mekundu] na kisha akamwamrisha akasimamisha Fajr wakati ilipochomoza alfajiri. Ilipokuwa siku ya pili akaichelewesha Dhuhr na akapenda kuicheleweshe na akaswali ´Aswr na jua limepanda ambapo akaichelewesha juu ya ile iliokutwa na akaswali Maghrib kabla ya kupotea mawingu [mekundu] na akaswali ´Ishaa baada ya kupita theluthi ya usiku na akaswali Fajr pindi ulipodhihiri mwanga wa mchana halafu akasema: “Yuko wapi anayeuliza wakati wa swalah?” Bwana yule akasema: “Mimi hapa, ee Mtume wa Allaah.” Akasema:

“Wakati wa swalah zenu ni baina ya kile mlichoona.”[4]

 Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

´Abdullaah bin ´Amr al-´Aaswr (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

 “Wakati wa Dhuhr ni pale linapopinduka jua na kikawa kivuli cha mtu ni sawa na urefu wake muda wa kuwa haijaingia ´Aswr, wakati wa ´Aswr ni pale jua halijakuwa manjano, wakati wa swalah ya Maghrib ni muda wa kuwa mawingu hayajapotea, wakati wa swalah ya ´Ishaa ni mpaka nusu ya usiku katikati, wakati wa swalah ya Subh ni pale kunapochomoza alfajiri muda wa kuwa halijachomoza jua. Jua likichomoza basi jizuilieni kuswali. Kwani hakika huchomoza kati ya pembe za shaytwaan.”[5]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Zipo Hadiyth nyenginezo zinazooanisha nyakati za swalah tano kimaneno na kimatendo. Hakujatofautishwa kati ya urefu wa mchana na ufupi wake, urefu wa usiku na ufupi wake maadamu nyakati za swalah ni zenye kupambanuka kwa zile alama alizozibainisha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haya ni kuhusiana na kuanisha nyakati zao za swalah.

Kuhusu kuanisha nyakati za funga zao za mwezi wa Ramadhaan, basi ni lazima kwa wale wote ambao ´ibaadah ni yenye kuwawajibikia kila siku kujizuilia na kula, kunywa na vifunguzi vyengine kuanzia pale alfajiri inapoingia mpaka kuzama kwa jua katika miji yao muda wa kuwa mchana unapambanuka na usiku katika miji yao na jumla ya muda wao ukawa ni masaa ishirini na nne. Ni halali kwao kula, kunywa, kufanya jimaa na mfano wake katika kile kipindi cha usiku wao peke yake ijapo ni kitambo kifupi. Hakika Shari´ah ya Uislamu ni yenye kuwaenea watu wote katika miji yote. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِۖ ثُمَّ أَتِمُّوا الصِّيَامَ إِلَى اللَّيْلِ

“Kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu weupe wa alfajiri katika weusi wa usiku. Kisha timizeni swawm mpaka usiku.”[6]

Ambaye atashindwa kukamilisha swawm kutokana na urefu wake, akatambua kutokana na ishara au uzowefu, akatambuzwa na daktari mwaminifu na mwerevu, akawa na dhana yenye nguvu ya kuwa swawm itampelekea yeye kuangamia au akauguwa maradhi makali, itampelekea kuongezeka kwa maradhi yake au kuchelewa kupona kwake, basi atakula na baadaye atalipa yale masiku ambayo aliacha kufunga katika mwezi wowote ambao ataweza kufanya hivo. Amesema (Ta´ala):

وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ

”Na atakayekuwa mgonjwa au safarini basi [atimize] idadi katika siku nyinginezo.”[7]

رَبَّنَا لَا تُؤَاخِذْنَا إِن نَّسِينَا أَوْ أَخْطَأْنَا

“Ee Mola wetu! Usituchukulie pale tutaposahau au tukikosea.”[8]

وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ

“Hakukufanyieni ugumu wowote ule katika dini.”[9]

2 – Ambaye anaishi katika mji ambao jua halizami wakati wa kiangazi na wala jua halichomozi wakati wa baridi au kwa mfano anaishi katika mji ambao mchana wake unaendelea mpaka miezi sita na usiku wake unaendelea mpaka miezi sita, basi analazimika kuswali zile swalah tano ndani ya kila masaa ishirini na nne na akadirie na kuzianishia nyakati zake hali ya kutegemea nchi ilio karibu zaidi na wao ambayo nyakati zake za swalah ni zenye kupambanuka hizi kutokana na zile. Hayo ni kutokana na  yale yaliyothibiti katika Hadiyth ya Israa´ na Mi´raaj ya kwamba Allaah (Ta´ala) ameufaradhishia Ummah huu swalah khamsini kila usiku na mchana. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakuacha kuendelea kumwomba Mola Wake wepesi mpaka akasema:

“Ee Muhammad! Ni swalah tano kila mchana na usiku ambapo kila swalah inayo [thawabu] kumi. Hivyo inakuwa swalah khamsini… “[10]

Vilevile kutokana na yale yaliyothibiti kutoka katika Hadiyth ya Twalhah bin ´Ubaydillaah (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesimulia:

“Kuna bwana mmoja kutoka katika watu wa Najd alikuja kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hali ya kuwa nywele zake ziko timtim, tunasikia sauti yake iliokuwa juu na wala hatuelewi kile anachokisema mpaka akasogea karibu na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tahamaki akauliza kuhusu Uislamu ambapo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

“Swalah tano wakati wa mchana na usiku.” Akauliza: “Je, kuna kingine kinachonilazimu mbali na hizo?” Akasema: “Hapana, isipokuwa ukipenda kujitolea… “[11]

Pia kutokana na yale yaliyothibiti kwa Anas (Radhiay Allaahu ´anh) ambaye amesema:

“Tulikuwa tukichukizwa kumuuliza Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) chochote. Tulikuwa tukipendekezwa aje mtu kutoka katika watu wa mashamba mwerevu akimuuliza na sisi huku tusikie. Akaja mtu mmoja katika watu wa mashamba akasema: “Ee Muhammad! Ametujia mjumbe wako ambapo akadai ya kwamba Allaah amekutumiliza.” Akajibu: “Amesema kweli.” Mpaka aliposema: “Mjumbe wako amedai kuwa tunalazimika kuswali swalah tano katika mchana na usiku wetu.” Akasema: “Amesema kweli.” Akasema: “Naapa kwa Yule aliyekutumiliza! Je, Allaah ndiye amekuamrisha haya?” Akajibu: “Ndio.”

Kadhalika imethibiti ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwaeleza Maswahabah zake juu ya al-Masiyh ad-Dajjaal ambapo wakasema: “Atakaa ardhini kwa muda gani?” Akasema: “Siku arobaini; siku ya kwanza itakuwa kama mwaka, siku ya pili itakuwa kama mwezi, siku ya tatu itakuwa kama wiki na siku nyenginezo zilizobakia zitakuwa kama masiku yenu.” Kukasemwa: “Ee Mtume wa Allaah! Ile siku ambayo itakuwa kama mwaka itatutosha kuswali swalah ya siku moja?” Akasema: “Hapana, zikadirieni kiwango chake.”[12]

Ile siku ya kwanza ambayo itakuwa kama mwaka hakuizingatia kama siku moja ambayo itatosha kuswali swalah tano. Bali amewajibisha kuswali swalah tano ndani ya kila masaa ishirini na nne na akawaamrisha wazigawe kwa mujibu wa nyakati zake kwa kuzingatia vipimo vya muda ambavyo viko kati ya nyakati zake katika siku ya kawaida ndani ya nchi zao.

Kwa hiyo ni lazima kwa waislamu katika nchi inayolengwa kuanisha nyakati za swalah na wapambanue nyakati za swalah humo hali ya kutegemea ule mji ambao uko karibu zaidi na wao ambao usiku unatofautiana na mchana na kunatambulika humo nyakati za swalah tano kutokana na zile alama zinazokubalika katika Shari´ah kila ndani ya masaa ishirini na nne.

Vivyo hivyo wanalazimika kufunga funga ya Ramadhaan. Pia ni lazima kwao wakisie swawm zao kwa njia ya kwamba waainishe wakati wa kuanza na kumalizika kwa mwezi, wakati wa kuanza na kumalizika kwa swawm. Wafanye hivo kila siku mwanzoni na mwishoni mwa mwezi, kuchomoza na kuzama kwa mwezi kila siku kutokana na mji ambao uko karibu zaidi na wao ambao usiku unatofutiana na mchana na mkusanyiko wake uwe masaa ishirini na nne kutokana na yale yaliyotangulia katika Hadiyth ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusu al-Masiyh ad-Dajjaal na akawaelekeza Maswahabah zake namna ya kuanisha nyakati za swalah. Kwa vile katika hayo hakuna tofauti ya swawm na swalah.

Swalah na amani ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad, kizazi chake na Maswahabah zake.

Kibaar-ul-´Ulamaa´.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (15/292-300).

[2] 17:78

[3] 04:103

[4] Muslim (613).

[5] Muslim (612).

[6] 02:187

[7] 02:185

[8] 02:286

[9] 22:78

[10] Muslim (1162).

[11] al-Bukhaariy (46) na Muslim (11).

[12] Muslim (2937).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Musaafir, uk. 70-77
  • Imechapishwa: 25/05/2022