Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

83 – Tunaona kufaa kuswali nyuma ya kila mwema na muovu katika wale wanaoswali kuelekea Qiblah.

MAELEZO

Dalili juu ya hilo ni matendo ya Maswahabah, jambo ambalo limebainishwa katika maelezo ya Ibn Abiyl-´Izz, na inatosha kama dalili. Isitoshe Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Watakuswalisheni. Wakipatia, basi ni kwa manufaa yenu na wao, na wakikosea, ni kwa manufaa yenu na ni dhidi yao.”[1]

Ameipokea al-Bukhaariy, Ahmad na Abu Ya´laa.

Kadhalika zipo dalili zingine nyingi juu ya kuwaswalia swalah ya jeneza anayekufa miongoni mwao[2].

Kuhusu Hadiyth inayosema ”Swali nyuma ya kila mwema na movu, na swali kila nyuma ya mwema na muovu”, cheni yake ya wapokezi ni dhaifu, kama nilivyoashiria katika maelezo ya Ibn Abiyl-´Izz[3]. Hakuna dalili yoyote inayoonyesha kutosihi kuswali nyuma ya mtenda dhambi. Hadiyth isemayo ”Wafanyeni maimamu wenu ni wale wabora wenu” cheni yake ya wapokezi ni dhaifu mno, kama nilivyohakikisha hilo katika ”adh-Dhwa´iyfah”[4]. Na kama ingelikuwa sahihi, basi isingelifahamisha kuwa ni lazima kuwafanya maimamu katika wale wabora, khaswa ikiwa wameteuliwa na yule mtawala. Endapo Hadiyth isemayo ”Mtenda dhambi hamwongozi muumini” ingelikuwa Swahiyh, basi ingelikuwa ni dalili ya wazi juu ya kutosihi uimamu wake, lakini haisihi pia, kama nilivyobainisha katika ”Jumu´ah” na ”Irwaa’-ul-Ghaliyl”[5].

[1] al-Bukhaariy (694) na Ahmad (8497).

[2] Tazama “Ahkaam-ul-Janaa’iz”, uk. 79

[3] Nimebainisha udhaifu wake katika “Dha´iyf Sunan Abiy Daawuud” (97) na “Irwaa’-ul-Ghaliyl” (527).

[4] Tazama “adh-Dhwa´iyfah” (1822).

[5] Tazama  ”Jumu´ah” na ”Irwaa’-ul-Ghaliyl” (591).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah – Sharh wa Ta´liyq, uk. 74-75
  • Imechapishwa: 07/10/2024