Ibn Abiyd-Dunyaa amepokea kupitia kwa Abu Khaliyfah al-´Abadiy aliyesema:

“Mwanangu alifariki na nikahuzunika kiasi kikubwa mpaka nikashindwa kulala. Ninaapa kwa Allaah kwamba nililala usiku mzima peke yangu kitandani na kumfikiria mwanangu. Tahamaki nikasikia sauti kutoka upande wa mlango wa nyumba ikisema: “as-Salaam ´alaykum wa Rahmatullaah, Abu Khaliyfah!” Nikajibu: “Wa ´alaykumus-Salaam wa Rahmatullaah.” Nikasikia woga kweli kweli na kutaka ulinzi kwa Allaah kisha nikasoma mwishoni mwa Aal ´Imraan mpaka nilipofikia:

وَمَا عِندَ اللَّـهِ خَيْرٌ لِّلْأَبْرَارِ

“Na vilivyoko kwa Allaah ni bora kabisa kwa wale wema.” 3:198

Sauti ile ikasema: “Abu Khaliyfah!” Nikajibu: “Nakuitikia.” Sauti ile ikasema: “Hivi kweli unataka nini? Unataka katika maisha yako kuwa na mwanao peke yake pasi na watu wengine? Wewe ni mtukufu zaidi kwa Allaah kuliko Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)? Hata na yeye mwanaye Ibraahiym alifariki na akasema: “Macho hutokwa na machozi na moyo huingiwa na huzuni na wala hatusemi isipokuwa yale yenye kumridhisha Muumba.” Wataka nini wewe? Unataka mtoto wako asife ilihali viumbe wote watatoweka? Unataka nini? Unataka kumuudhi Allaah kwa kuviendesha viumbe Wake? Ninaapa kwa Allaah kama kusingelikuwa mauti basi ardhi isingeliwaenea na kwamba wasingelinufaika na maisha kama isingelikuwa maliwazo.” Kisha sauti ile ikasema: “Unahitajia kitu?” Nikasema: “Kwani wewe ni nani – Allaah akurehemu?” Akajibu: “Ni mmoja katika majirani wako majini.”

al-Hasan al-Baswriy ameeleza namna ambavyo kuna mtu alihuzunika kwa kufa mtoto wake na akamshtakia al-Hasan. al-Hasan akamwambia: “Ilikuwa ikitokea [wakati mwingine] kumkosa mwanao?” Akasema: “Ndio. Kuwa kwake mbali kulikuwa ni zaidi ya kuwepo kwake.” al-Hasan akasema: “Mchukulie kama yuko mbali. Hakuwahi kuwa mbali na wewe kwa njia inayopelekea katika kheri kama hii.” Mtu yule akasema: “Abu Sa´iyd! Umenisahilishia huzuni wangu juu ya mwanangu.”

Salamah amesema:

“Pindi mvulana wa ´Umar bin ´Abdil-´Aziyz alipofariki alimfunua uso wake na kusema: “Allaah akurehemu, ee mwanangu! Nilifurahi pindi ulipozaliwa na niliishi maisha ya furaha na wewe. Hata hivyo hakuna siku nina furaha kama hii ya leo. Ninaapa kwa Allaah utakuja kumwita baba yako Peponi.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 79-80
  • Imechapishwa: 14/10/2016