Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kuridhika kwa moyo na macho ni kutokana na Allaah (´Azza wa Jall), ilihali kuridhia kwa mkono na ulimi inatokana na shaytwaan.”[1]

Imesihi kwamba Abu Maalik al-Ash´ariy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mambo manne katika Ummah wangu ni miongoni mwa mambo ya kipindi cha kikafiri na hawatoyaacha; kujifakhari kwa koo, kutukaniana nasaba, kuinasibisha mvua kwa nyota na kuomboleza.”[2]

Vilevile amesema:

“Mwanamke mwenye kuomboleza ikiwa hakutubia kabla ya kufa kwake, basi atafufuliwa siku ya Qiyaamah na huku akiwa amevishwa nguo ya shaba iliyoyeyuka na kanzu ya ukoma.”[3]

Ameipokea Muslim.

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwanamke yeyote mwenye kuomboleza anayekufa kabla ya kutubia, basi Allaah atamvisha nguo ya shaba ambapo amsimamishe mbele ya watu siku ya Qiyaamah.”[4]

Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwanamke mwenye kuomboleza atatoka ndani ya kaburi akiwa timtim na mwenye vumbi. Atakuwa amevaa nguo ya juu ya fedheha na vazi la nje ya laana. Atakuwa mwenye kuweka mkono wake juu ya kichwa huku akisema ´Ole wangu!` na huku Malaika akiitikia ´Aamiyn! Aamiyn!`. Kisha fungu lake juu ya yote hayo iwe Moto.”[5]

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Hakika wanawake hawa wenye kuomboleza siku ya Qiyaamah watakuwa safu mbili ndani ya Moto; safu moja upande wa kuliani mwao na safu nyingine upande wa kushotoni mwao. Wataomboleza juu ya wakazi wa Motoni kama wanavyobweka mijibwa.”

Abu Sa´iyd al-Khudriy (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amemlaani mwanamke anayeombolea na mwanamke anayesikiliza.”[6]

 Imesihi kutoka kwa ´Abdullaah bin Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Si katika sisi yule anayejipiga mashavu, akapasua nguo na akaita wito wa kipindi kabla ya kuja Uislamu.”[7]

[1] Ahmad (1/238) na (1/335). Swahiyh kwa mujibu wa Ahmad Shaakir.

[2] Muslim (934), Ahmad (5/342), Ibn Maajah (1581) na al-Haakim (1/383).

[3] Muslim (934).

[4] Abu Ya´laa (1577).

[5] Ibn-un-Najjaar (42454).

[6] Abu Daawuud (3128). Dhaifu kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “Dhwa´iyf Sunan Abî Daawuud” (3128).

[7] al-Bukhaariy (1297) na Muslim (927).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bard-ul-Akbaad ´inda Faqd-il-Awlaad, uk. 117-121
  • Imechapishwa: 28/08/2023