154 –  Aadam bin Abiy Iyaas amesema: Abu Ja´far ar-Raaziy ametuhadithia, kutoka kwa ar-Rabiy´, kutoka kwa Abul-´Aaliyah ambaye amesema kuhusu maneno YAake (Subhaanahu wa Ta´ala):

هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن يَأْتِيَهُمُ اللَّـهُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ وَالْمَلَائِكَةُ

”Je, wanangojea nini isipokuwa Allaah awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika?”

”Malaika watakuja katika vivuli vya mawingu na Allaah atakuja anavyotaka. Ni kama mfano wa maneno Yake (Ta´ala):

وَيَوْمَ تَشَقَّقُ السَّمَاءُ بِالْغَمَامِ وَنُزِّلَ الْمَلَائِكَةُ تَنزِيلًا

”Na Siku ambayo mbingu itafunguka kwa mawingu na Malaika watateremshwa mteremsho mkubwa.”

155 – Abu ´Awaanah amesema: al-Ajlah ametuhadithia: adh-Dhwahhaak bin Muzaahim ametuhadithia:

”Allaah (Ta´ala) atashuka katika fahari na uzuri Wake. Atakuwa na awatakao katika Malaika Wake.”[1]

156 – ´Amr bin Hammaad amesimulia kutoka kwa Asbaatw, kutoka kwa as-Suddiy ambaye amesema:

”Allaah atakuja katika vivuli vya mwingu ambapo mbingu zipasuke, na Malaika watateremka mteremko mkubwa.”

157 – al-Waliyd bin Muslim amesema:

”Nilimuuliza Zuhayr bin Muhammad al-Makkiy kuhusu maneno Yake Allaah (Ta´ala):

هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن يَأْتِيَهُمُ اللَّـهُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ وَالْمَلَائِكَةُ

”Je, wanangojea nini isipokuwa Allaah awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika?”

Akajibu:

”Vivuli vya mawingu vitapambwa kwa yakuti, taji ya vito na peridot.”

158 – ´Abdullaah ad-Dashtakiy amesimulia kutoka kwa baba yake, kutoka kwa ar-Rabiy´ aliyesema kuhusu maneno Yake Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala):

هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن يَأْتِيَهُمُ اللَّـهُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ وَالْمَلَائِكَةُ

”Je, wanangojea nini isipokuwa Allaah awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika?”

”Hiyo ni ile siku ya Qiyaamah. Malaika watawajia katika vivuli vya mawingu, na Mola atakuja vile anavyotaka.”

Katika baadhi ya visomo imekuja:

هَلْ يَنظُرُونَ إِلاَّ أَن يَأْتِيَهُمُ اللّهُ وَالْمَلآئِكَةُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ

“Je, wanangojea nini isipokuwa Allaah na Malaika wawajie katika vivuli vya mawingu?”

Namna hiyo ndio amepokea Abush-Shaykh katika tafsiri yake ya Qur-aan.

159 – Amesema tena: Ahmad bin Yasaar al-Marwaziy amesema katika ”ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah”: Anas bin Abiy Aniysah ar-Rahaawiy ametuhadithia: ´Uthmaan bin ´Abdir-Rahmaan ametuhadithia, kutoka kwa Twalhah bin Zayd, kutoka kwa bwana mmoja, kutoka kwa Ka´b ambaye amesema:

”Kuna milima minne. Kila mlima una lulu inayoangaza yaliyo kati ya Mashariki na Magharibi: Lubnaan, Juudiy, Twur na Jaliyl. Allaah ataiweka kwenye pembe za Yerusalemu. Baada ya hapo aje Mola na ´Arshi Yake na ziwe juu yake.”

Ibn Lahiy´ah amepokea mfano wake kutoka kwa Abu Qubayl, kutoka kwa Ka´b. Njia zote mbili ni nyonge.

160 – Muhammad bin Haatim amesema: Ishaaq bin ´Iysaa ametuhadithia:

”Tulifika kwa ´Abdul-´Aziyz bin Abiy Salamaj al-Maajaashuun tukiwa na Jahmiy anayepina ujio wa Allaah siku ya Qiyaamah. Akasema: ”Ee mwanangu, nini unachopinga?” Akasema: ”Allaah ni mtukufu zaidi kutokana na kushuka namna hiyo.” Akasema: ”Ee mpumbavu! Sio sifa ya Allaah inayobadilishwa, lakini macho yako ndio yamebadilishwa mpaka unamuona  vile unavyotaka wewe.” Jahmiy yule akasema: ”Natubu kwa Allaah.” Akajirejea kutokana na maoni yake.”

161 – Ibn Abiy ´Aruubah amesimulia kutoka kwa Qataadah, kutoka kwa Anas ambaye amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kutaendelea kutupwa ndani ya Moto, na utakuwa ukisema:

هَلْ مِن مَّزِيدٍ

“Je, hakuna ziada yoyote?”[2]

mpaka aje Mola wa walimwengu na aweke unyayo Wake juu yake ambapo utasema. Utavutana na kusema: “Naapa kwa ushindi Wako na ukarimu Wako! Tosha, tosha.”

Mlango huu ni mpana kutoka ndani ya Qur-aan, Sunnah na maneno ya Salaf kuhusu ujio wa Allaah – Ambaye habadiliki na wala hateketei. Tunamwamini na sifa Zake zingine zote zilizopokelewa na tunasimama pale waliposimama watu. Tunamuomba Allaah (Ta´ala) azifanye nyoyo zetu kuwa imara katika kumuamini, majina na sifa Zake.

[1] Jaamiy´-ul-Bayaan (24/40).

[2] 50:30

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy (afk. 748)
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Arba´iyn fiy Swifaati Rabb-il-´Aalamiyn, uk. 158-164
  • Imechapishwa: 11/06/2024