Ndugu wapendwa! Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنَّ الَّذِينَ يَتْلُونَ كِتَابَ اللَّـهِ وَأَقَامُوا الصَّلَاةَ وَأَنفَقُوا مِمَّا رَزَقْنَاهُمْ سِرًّا وَعَلَانِيَةً يَرْجُونَ تِجَارَةً لَّن تَبُورَ لِيُوَفِّيَهُمْ أُجُورَهُمْ وَيَزِيدَهُم مِّن فَضْلِهِ ۚ إِنَّهُ غَفُورٌ شَكُورٌ

“Hakika wale wanakisoma Kitabu cha Allaah na wakasimamisha swalah na wakatoa sehemu katika yale Tuliyowaruzuku kwa siri na dhahiri wanataraji biashara isiyoenda patupu ili [Allaah] awalipe ujira wao kikamilifu na awazidishie kutokana na fadhilah Zake; hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kupokea shukurani.”[1]

Kuna usomaji wa Qur-aan aina mbili:

1- Usomaji wa kihukumu. Ni kule kusadikisha khabari zake na kutekeleza hukumu zake kwa kutekeleza amri zake na kujiepusha na makatazo yake. Tutayazungumzia haya katika kikao kingine – Allaah akitaka.

2- Usomaji wa kimatamshi. Ni kule kuisoma. Kumepokelewa maandiko mengi juu ya fadhilah zake ima Qur-aan yote, Suurah au Aayah maalum. al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) aliyeeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mbora wenu ni yule mwenye kujifunza Qur-aan na akaifundisha wengine.”

al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) aliyeeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kuisoma Qur-aan kwa usanifu yuko pamoja na Malaika mbinguni. Na yule mwenye kuisoma na anataabikataabika na ni nzito kwake anapata ujira mara mbili.”

Ujira mara mbili moja ni kwa sababu ya usomaji na ujira mwingine ni kwa ajili ya ule uzito msomaji anapata.

al-Bukhaariy na Muslim wamepotea kupitia kwa Abu Muusa (Radhiya Allaahu ´anh) aliyesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mfano wa muumini ambaye anasoma Qur-aan ni kama mfano wa ndimu[2]; harufu yake ni nzuri na harufu yake ni nzuri. Na mfano wa muumini ambaye hasomi Qur-aan ni kama mfano wa tende; isiyokuwa na harufu na ladha yake ni nzuri.”

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Umaamah (Radhiya Allaahu ´anh) aliyesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Isomeni Qur-aan kwani itakuja siku ya Qiyaamah hali ya kuwa ni yenye kuwaombea watu wake.”

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa ´Uqbah bin ´Aamir (Radhiya Allaahu ´anh) aliyeeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kwa nini asirauke mmoja wenu asubuhi kwenda msikitini akajifunza au akasoma Aayah mbili kutoka katika Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall) ni bora kwake kuliko ngamia wawili, [Aayah] tatu ni bora kwake kuliko [ngamia] watatu, [Aayah] nne ni bora kwake kuliko [ngamia] wanne na juu ya idadi zake katika ngamia.”

 Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) aliyeeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hawatokusanyika watu katika nyumba miongoni mwa nyumba za Allaah wakikisoma Kitabu cha Allaah na wakikidurusu kati yao, isipokuwa wanateremkiwa na utulivu, rehema huwafunika na Malaika huwazunguka na Allaah huwataja kwa wale walioko Kwake.”

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ipatilizeni Qur-aan! Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko mikononi Mwake kwamba ni yenye kuponyoka haraka zaidi kuliko ngamia kwenye kamba yake.”

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Asiseme mmoja wenu kwamba amesahau Aayah kadhaa na kadhaa. Bali amesahaulishwa.”

Ameipokea Muslim.

Hilo ni kwa sababu maneno yake “nimeshau” linaweza kuleta hisia ya mtu kutojali kile alichohifadhi katika Qur-aan mpaka akasahau.

´Abdullaah bin Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yule mwenye kusoma herufi moja kutoka katika Kitabu cha Allaah ana ujira mmoja na jema moja linalipwa mara kumi mfano wake. Simaanishi kuwa “Alif Laam Miym” kwamba ni herufi moja. Bali “Alif” ni herufi moja, “Laam” ni hefuri nyingine na “Miym” ni herufi nyingine.”

Ameipokea at-Tirmidhiy[3].

´Abdullaah bin Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwa kusema:

“Hakika Qur-aan hii ni karamu ya Allaah. Hivyo basi kubalini karamu Yake kadri na muwezavyo. Hakika Qur-aan hii ni kamba ya Allaah madhubuti, nuru ya wazi, dawa yenye kunufaisha, kinga kwa yule atakayeshikamana nayo, uokozi kwa yule atakayeifuata ambaye hatopotea akapondoka, hatoenda kombo akanyooshwa, maajabu yake hayamaliziki na haichoshi kwa kuirudiarudia sana. Isomeni! Hakika Allaah ni mwenye kuwalipa ujira kila herufi kwa kumi mfano wake. Simaanishi kuwa “Alif Laam Miym” kwamba ni herufi moja. Bali “Alif” ni herufi moja, “Laam” ni hefuri nyingine na “Miym” ni herufi nyingine.”

Ameipokea al-Haakim.

Ndugu wapendwa! Hizi ndio fadhilah za kuisoma Qur-aan. Ujira huyu ni kwa yule mwenye kutafuta ujira na radhi kutoka kwa Allaah. Inahusiana na ujira mkubwa kwa kitendo kidogo. Mkoseshwa ni yule atayezembea kwayo na mla khasara ni yule atayepitwa na faida yake pindi ataposhindwa kuisoma. Fadhilah hizi ni zenye kuienea Qur-aan nzima.

[1] 35:29-30

[2] Ni tunda fulani mfano wa ndimu.

[3] Amesema kuwa Hadiyth ni nzuri na Swahiyh na geni kwa njia hii. Wako baadhi ya wanachuoni waliokuja nyuma ambao wameisahihisha kwa kuishilia kwa Swahabah ´Abdullaah.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majaalis Shahr Ramadhwaan, uk. 31-35
  • Imechapishwa: 20/04/2020