Ibn Abiy Haatim amepokea katika Tasfiyr yake kutoka kwa Khaalid bin Yaziyd, kutoka kwa ´Iyaadhw bin ´Uqbah ambaye mtoto wake Yahyaa alifariki. Wakati aliposhuka kwenye kaburi lake mtu mmoja akamwambia: “Ninaapa kwa Allaah kwamba alikuwa ni kiongozi wa jeshi. Tarajia malipo kwa Allaah.” Baba yake akasema: “Ni kipi chenye kunizuia kutarajia malipo? Alikuwa ni pambo la dunia hii na hivi sasa ni katika yale mema yenye kubaki.”

Mtu huyu alikuwa ni mwenye subira, mwenye kuridhia maamuzi ya Allaah na mwenye kutarajia thawabu za Allaah. Ni uzuri uliyoje ulivyokuwa uelewa wake? Ni uzuri uliyoje alivyojipa pole mwenyewe?

Thaabit ameeleza kuwa pindi ´Abdullaah bin Mutwarrif alipofariki baba yake Mutwarrif alitoka hali ya kuwa amevaa vizuri na mwenye kujitia mafuta. Watu walipomuona hivyo wakamsirikia na kusema: “Hivi kweli umekuja namna hii na isitoshe hali ya kujipaka mafuta ilihali mwanao ´Abdullah amefariki?” Akajibu: “Nijizike kwa ajili ya hilo ilihali Mola Wangu ameniahidi zawadi kwa ajili ya hilo na kila zawadi ninaipenda zaidi kuliko dunia nzima. Allaah (Ta´ala) amesema:

الَّذِينَ إِذَا أَصَابَتْهُم مُّصِيبَةٌ قَالُوا إِنَّا لِلَّـهِ وَإِنَّا إِلَيْهِ رَاجِعُونَ أُولَـٰئِكَ عَلَيْهِمْ صَلَوَاتٌ مِّن رَّبِّهِمْ وَرَحْمَةٌ ۖ وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُهْتَدُونَ

“Wale ambao unapowafika msiba husema: “Hakika sisi ni wa Allaah na hakika sisi Kwake ni wenye kurejea.” – [wafikishie ya kwamba] hao zitakuwa juu yao barakah kutoka kwa Mola wao na rahmah; na hao ndio wenye kuongoka.” 02:156-157

Je, nijizike baada ya haya?”

Muhammad bin Khalaf amesema:

“Ibraahiym al-Harbiy alikuwa na mtoto mwenye miaka kumi na moja wakati alipofariki. Mtoto huyo alikuwa amehifadhi Qur-aan amechota sehemu kubwa ya elimu. Nilipokuja kwa ajili ya kumpa pole akasema: “Nilikuwa napenda mwanangu afe.” Nikamwambia: “Ee Abu Ishaaq! Wewe ni msomi wa duniani. Vipi unaweza kusema namna hii kwa mtoto ambaye ulimfunza sana Hadiyth na Fiqh?” Akajibu: “Ndio. Nimeota usingizini kuwa Qiyaamah kimefika. Niliona watoto wameshika mabakuli ya maji na wakiwakaribisha watu maji hayo. Siku hiyo ilikuwa ni siku yenye joto sana. Nikamwambia mtoto mmoja: “Naomba kunywa kwenye maji haya.” Mtoto yule akanitazama: “Baba yangu si wewe.” Nikamwambia: “Kwani nyinyi ni kina nani?” Mtoto yule akasema: “Sisi ni wale watoto waliokufa katika ule mwaka wa kwanza na tukawaacha wazazi wetu. Tunakutana nao na kuwanywesha maji.” Akasema: “Kwa ajili hii ndio maana nilipenda afe.”

Ibn ´Asaakir amepokea kwa mlolongo wa wapokezi wake kupitia kwa Suhayl bin al-Handhwalah al-Answaariy – ambaye alikuwa hawezi kupata mtoto – aliyesema:

“Mimi kupata mtoto akafariki, kama kuharibika kwa mimba, na halafu nikawa na subira na kutarajia malipo nakupenda zaidi kuliko kupata dunia nzima na vilivyomo ndani yake.”

Ibn-ul-Handhwalah alikuwa ni mmoja katika wale waliokula kiapo cha usikivu na utiifu kumpa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) chini ya mti.

Ibn ´Asaakir amepokea tena kuwa mtoto wa ´Iyaadhw bin ´Uqbah alikuwa katika hali ya umaututi pindi ´Iyaadhw alipokuwa amefasiri nje ya mji. Mama wa yule mtoto akamwambia mwanaye: “Lau Abu Wahb angelikuwa hapa basi angelifurahi.” Wakati ´Iyaadhw bin ´Uqbah alipokuwa katika hali ya kukata roho akamwambia kaka yake Abu ´Ubayd: “Umeshinda. Nilitarajia utakufa kabla yangu ili nipate kuwa na subira kwa kufa kwako na kutarajia malipo.”

Abu Muslim al-Khawlaaniy amesema:

“Napenda zaidi kupata mtoto ambaye ataangaliwa na Allaah mpaka atapofikia kuwa kijana na nikampenda zaidi na baada ya hapo Allaah akamchukua kutoka kwangu kuliko kupata dunia nzima na vilivyomo ndani yake.”

Abul-Hasan al-Madaainiy amesema:

“´Umar bin ´Abdil-´Aziyz alifika kwa mmoja katika watoto wake ambaye alikuwa katika uchungu wa umauti. Akamuuliza: “Unaionaje hali yako?” Akajibu: “Unanielewa kuwa katika haki.” Akasema: “Ee mwanangu! Mimi napenda zaidi wewe uwe katika mzani wangu kuliko mimi kuwa katika mzani wako.” Mtoto yule akamjibu kwa kumwambia: “Ee babangu! Mimi napendelea zaidi kile unachokipenda kuliko ninachokipenda.”

Thaabit al-Bunaaniy amesema:

“Silah bin Ushaym alikuwa ametoka vitani yeye akiwa pamoja na mwanaye. Akamwambia: “Ee mwanangu! Sogea mbele upambane uuawe ili niweze kutarajia malipo kwa subira nitayokuwa nayo. Akafanya hivo akapambana mpaka akauawa. Baada ya hapo baba yake akasogea na akauawa. Pindi wanawake walipokusanyika mke wake Mu´aadhah al-´Adhriyyah akasema: “Ikiwa mmekuja kwa ajili ya kunipongeza karibuni. Ikiwa mmekuja kwa lengo lingine lisilokuwa hilo rudini.”

Kathiyr bin Tamiym ad-Daariy amesema:

“Nilikuwa nimekaa na Sa´iyd bin Jubayr pindi mtoto wake ´Abdullaah alipokuja. Mtoto huyo alikuwa na elimu. Sa´iyd bin Jubayr akasema: “Ninajua kilicho bora kwake.” Wakasema: “Ni kipi?” Akasema: “Afe ili nitarajie malipo kwa subira nitayokuwa nayo.”

´Umar bin Maymuun bin Mahraan amesema:

“Mimi na baba yangu tulitufu kwenye Ka´bah. Tahamaki akakutana na mwanaume mtumzima ambaye alimkumbatia. Mzee yule alikuwa na mvulana wa rika yangu. Baba yangu akamwambia: “Huyu ni nani?” Akasema: “Mwanangu.” Baba yangu akamuuliza: “Wewe ni mwenye kuridhika naye kiasi gani?” Akasema: “Ee Abu Ayyuub! Hakuna sifa nzuri hata moja isipokuwa ninamuona nayo isipokuwa moja peke yake.” Baba yangu akasema: “Ipi hiyo?” Akasema: “Nataka afe kabla yangu ili niweze kulipwa kwa ajili yake.” Kisha wakatengana. Nikamuuliza baba yangu mzee yule alikuwa ni nani. Akasema: “Mak-huul.”

Kikusudiwacho ni kwamba hali kama hii ni kubwa na tukufu kwa yule anayetaka kufikwa na misiba na kufurahi kwayo kwa kuzingatia thawabu zake. Hakuna anayelitaka hilo mpaka baada ya kujua ni nguvu na subira gani alionayo mtu. Pindi mtu anapodai jambo basi anatakiwa mara nyingi ahakikishe madai hayo. Suhnuun (Rahimahu Allaah) alikuwa akisema: “Nimeridhika na yale yote Uliyonipangia. Nijaribu kwa yale yote unayotaka.” Ndipo Allaah akamjaribu akawa hawezi kukojoa. Hakuweza kusubiri. Alikuwa akienda kwa watoto na kuwaambia: “Muombeeni du´aa ami yenu mwongo.”

Njia kamilifu ni maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Msitamani kukutana na adui na muombeni Allaah afya.”

Tambua ya kwamba ikiwa nia ya mtu kwa mtoto kumkosa au kumbakiza ni nzuri, basi analipwa malipo makubwa kwa nia zote mbili. Hakika ya matendo yanalipwa kutegemea na nia. Imethibiti kuwa ´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Hakuna mke, wala mali wala mtoto isipokuwa mimi nataka kuwaambia “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea”. Isipokuwa tu ´Abdullaah bin ´Umar ambaye nataka abaki kati ya watu.”

Kinachotilia nguvu hilo ni yale yaliyothibiti katika “as-Swahiyh” ya Muslim ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Pindi mwanaadamu anapofariki basi matendo yake yote hukatika isipokuwa vitu vitatu; swadaqah yenye kuendelea, elimu yenye kunufaisha au mtoto mwema mwema mwenye kumuombea du´aa.”

Katika Hadiyth iliyopokelewa kupitia kwa Anas imekuja:

“Mambo saba mtu huenda nayo baada ya kufa… “

Moja katika mambo hayo akataja:

“… au akaacha mtoto mwenye kumuombea msamaha baada ya kufa kwake.”

´Abdullaah bin ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) aliitwa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa ni mtu mwema au mja mwema.

Ni jambo lisilokuwa na shaka kwamba bora ni mtu aendelee kulipwa baada ya kufa kwake kuliko thawabu kukatika baada ya kufa kwake. Hakika mja ni mwenye haja kubwa ya matendo mema baada ya kufa kwake. Kwa kufa matendo yote yanakatika isipokuwa tu yale Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliyoyataja. Kwa ajili hiyo ndio maana mimi naelewa kuwa lililo bora ni mtu kupata watoto kwa sababu wataendelea kueshi. Lakini kwa vile watu hawa walikuwa na imani yenye nguvu kwelikweli kwenye nyoyo zao na kusadikisha mipango na makadirio ya Allaah, ndio maana wakawa wamesema mambo uwazi. Uhalisia wa mambo sio watu wengi wanaosubiri kwa mitihani na Allaah ndiye anajua zaidi.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 31-36
  • Imechapishwa: 14/10/2016