Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

137 – Tunawaamini Malaika wa mauti ambaye amepewa kazi ya kuzitoa roho za walimwengu.

MAELEZO

Allaah (Subhaanah) amesema:

حَتَّىٰ إِذَا جَاءَ أَحَدَكُمُ الْمَوْتُ تَوَفَّتْهُ رُسُلُنَا وَهُمْ لَا يُفَرِّطُونَ

“Mpaka yanapomfikia mmoja wenu kifo, Wajumbe Wetu humfisha, nao hawazembei.”[1]

Bi maana Malaika. Wajumbe wanaweza kuwa katika Malaika na wanaweza kuwa katika watu:

اللَّـهُ يَصْطَفِي مِنَ الْمَلَائِكَةِ رُسُلًا وَمِنَ النَّاسِ ۚ إِنَّ اللَّـهَ سَمِيعٌ بَصِيرٌ

“Allaah anateua wajumbe miongoni mwa Malaika na miongoni mwa watu. Hakika Allaah ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[2]

وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ يَتَوَفَّى الَّذِينَ كَفَرُوا ۙ الْمَلَائِكَةُ يَضْرِبُونَ وُجُوهَهُمْ وَأَدْبَارَهُمْ وَذُوقُوا عَذَابَ الْحَرِيقِ

“Na lau ungeliona pale Malaika wanapowafisha wale waliokufuru wanawapiga nyuso zao na migongo yao [na huku wakiwaambia]: “Onjeni adhabu iunguzayo.”[3]

قُلْ يَتَوَفَّاكُم مَّلَكُ الْمَوْتِ الَّذِي وُكِّلَ بِكُمْ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّكُمْ تُرْجَعُونَ

“Sema: “Atakufisheni Malaika wa mauti ambaye amewakilishwa kwenu, kisha kwa Mola wenu mtarejeshwa.”[4]

Katika baadhi ya Aayah mauti yananasibishwa kwa Malaika, na katika baadhi ya Aayah zingine mauti yananasibishwa kwa Malaika mmoja. Hiyo ni dalili inayofahamisha kuwa Malaika wanaye kiongozi – Malaika wa mauti.

Hakuna yeyote anayebisha kifo, lakini wako baadhi ya watu wanaopinga Malaika wa mauti na wasaidizi wake. Kuwaamini Malaika ni msingi katika misingi ya Uislamu na misingi ya imani iliyothibiti kwa Qur-aan na Sunnah. Yule anayepinga kuwepo kwa Malaika kwa ujumla au Malaika yeyote miongoni mwa Malaika, ni kafiri kwa sababu atakuwa ameipinga nguzo miongoni mwa nguzo za imani.

[1] 6:61

[2] 22:75

[3] 8:50

[4] 32:11

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Mukhtaswarah ´alaal-´Aqiydah at-Twahaawiyyah, uk. 192-193
  • Imechapishwa: 09/12/2024