14. Maswahabah waliosimulia Hadiyth kuhusu Kushuka

Hadiyth imesimuliwa vilevile kutoka kwa wengine mbali na Abu Hurayrah.

Naafiy´ bin Jubayr bin Mutw´im ameipokea kutoka kwa baba yake.

Muusa bin ´Uqbah ameisimulia kutoka kwa Ishaaq bin Yahyaa, kutoka kwa ´Ubaadah bin as-Swaamit.

´Abdur-Rahmaan bin Ka´b bin Maalik ameisimulia kutoka Jaabir bin ´Abdillaah.

´Ubaydullaah bin Abiy Raafiy´ ameisimulia kutoka kwa ´Aliy bin Abiy Twaalib.

Shariyk ameisimulia kutoka kwa Abu Ishaaq, kutoka kwa Abul-Ahwasw, kutoka kwa ´Abdullaah bin Mas´uud.

Muhammad bin Ka´b ameisimulia kutoka kwa Fadhwaalah bin ´Ubayd, kutoka kwa Abud-Dardaa’.

Abuz-Zubayr ameisimulia kutoka kwa Jaabir.

Sa´iyd bin Jubayr ameisimulia kutoka kwa Ibn ´Abbaas.

Vilevile imesimuliwa kutoka kwa mama wa Waumini ´Aaishah na Umm Salamah – Allaah awawie radhi wote.

Njia zote hizi zimepokelewa kwa cheni zake za wapokezi katika kitabu chetu kikubwa kwa jina al-Intiswaar.

al-Awzaa´iy amesema: Yahyaa bin Abiy Kathiyr amenihadithia: Abu Salamah ametuhadithia, kutoka kwa Abu Hurayrah aliyesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Kunapopita nusu ya usiku, au theluthi yake, basi Allaah anashuka katika mbingu ya chini na kusema mpaka kupambazuke: ”Kuna mwenye kuomba apewe? Kuna mwenye kuomba aitikiwe? Kuna mwenye kuomba msamaha asamehewe?”

Sa´iyd bin Marjaanah amesimulia kutoka kwa Abu Hurayrah kwa ziada mwishoni mwake inayosema:

”Kisha hunyoosha mikono Yake na kusema: ”Ni nani ambaye anataka kumkopa Ambaye hanyimi wala hadhulumu?”[1]

Abu Haazim amesimulia kutoka kwa Abu Hurayrah, kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), aliyesema:

”Hakika Allaah hushuka katika mbingu ya chini katika ile theluthi ya mwisho na akaita kwa sauti: ”Kuna mwenye kuomba Nimpe? Kuna mwenye kuomba msamaha Nimsamehe?” Hakuna kitu kilicho na roho isipokuwa hufikiwa na ujumbe huo isipokuwa tu majini na watu.” Akasema: ”Hapo ni pale ambapo anawika jogoo, akapiga kelele punda na mbwa akabweka.”

[1] Muslim (758).

  • Mhusika: Imaam Abu ´Uthmaan Ismaa´iyl bin ´Abdir-Rahmaan as-Swaabuuniy (afk. 449)
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-us-Salaf wa Aswhaab-il-Hadiyth, uk. 206-212
  • Imechapishwa: 06/12/2023