13. Maana sahihi ya kutafuta ukatikati na njia (الوسيلة)

Ukatikati na njia (الوسيلة) maana yake ni utiifu na ukaribu. Kilugha maana yake ni kitu chenye kufikisha katika malengo. Kitu chenye kufikisha katika radhi na mapenzi ya Allaah ni njia ya kumwendea. Huu ndio ukati kati uliowekwa kwenye Shari´ah katika maneno Yake (Ta´ala):

وَابْتَغُوا إِلَيْهِ الْوَسِيلَةَ

“Tafuteni Kwake njia.” (05:35)

Lakini kuhusu waliopinda na wapumbavu wanasema kuwa ukatikati ni kuweka kati yako wewe na Allaah mawalii, watu wema au wafu ili wakukurubishe kwa Allaah:

مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ

“Hatuwaabudu isipokuwa kwa lengo la kutukurubisha kwa Allaah ukaribu.” (39:03)

Hivi ndivyo wanavyofasiri “ukatikati na njia” wapumbavu hawa. Wanaonelea kuwa unatakiwa kuweka mkatikati kati yako wewe na Allaah anayekutambulisha kwa Allaah, kukufikishia mahitaji yako na kuelezea juu yako. Ni kana kwamba Allaah (Jalla wa ´Alaa) Mwenyewe hajui au ni bakhili ambaye hatoi isipokuwa baada ya mkatikati huyu kumnga´ang´ania – ametakasika Allaah (Jalla wa ´Alaa) na yale wanayoyasema! Wanawapaka watu mchanga wa machoni na kuwaambia kuwa Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ يَدْعُونَ يَبْتَغُونَ إِلَىٰ رَبِّهِمُ الْوَسِيلَةَ أَيُّهُمْ أَقْرَبُ

“Hao wanaowaomba [wao wenyewe] wanatafuta kwa Mola wao njia [na] kumkurubia kadri wanavyoweza… “

Wanasema kuwa hii ni dalili inayoonyesha kuwa kuweka wakatikati mbele ya Allaah katika viumbe ni kitu kimewekwa katika Shari´ah kwa sababu Allaah amewasifu wale wenye kufanya hivo. Katika Aayah nyingine imekuja:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَابْتَغُوا إِلَيْهِ الْوَسِيلَةَ

“Enyi mlioamini! Mcheni Allaah na tafuteni Kwake njia.” (05:35)

Wanasema eti Allaah ametuamrisha kufanya ukatikati wa kumfikia na ukatikati maana yake ni kuweka wakatikati na watetezi. Namna hii ndivyo wanayapotosha maneno kuyaondosha mahali pake stahiki. Ukatikati unaokubalika kwa mujibu wa Qur-aan na Sunanh ni utiifu unaokurubisha kwa Allaah kwa njia ya mtu kufanya Tawassul kwa majina na sifa Zake (Subhaanahu wa Ta´ala). Hii ndio njia na ukatikati unaokubalika katika Shari´ah.

Kuhusu kufanya Tawassul kwa Allaah kupitia viumbe, ni jambo limekatazwa na ni ukatikati wa kishirki. Isitoshe ndio uliyofanywa na washirikina hapo kale:

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنفَعُهُمْ وَيَقُولُونَ هَـٰؤُلَاءِ شُفَعَاؤُنَا عِندَ اللَّـهِ

“Na wanaabudu asiyekuwa Allaah ambao [hawawezi] kuwadhuru na wala kuwanufaisha na wanasema: “Hawa ni waombezi wetu mbele ya Allaah.”” (10:18)

وَالَّذِينَ اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ إِنَّ اللَّـهَ يَحْكُمُ بَيْنَهُمْ فِي مَا هُمْ فِيهِ يَخْتَلِفُونَ ۗ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي مَنْ هُوَ كَاذِبٌ كَفَّارٌ

“Na wale wanaowafanya wengine badala Yake kuwa walinzi [wakisema]: “Hatuwaabudu isipokuwa kwa lengo la kutukurubisha kwa Allaah ukaribu.” Hakika Allaah atahukumu kati yao katika yale yote waliyokhitilafiana nayo. Hakika Allaah hamwongoi aliye muongo, kafiri.” (39:03)

Hii ndio shirki ileile ya watu wa kale na waliokuja nyuma. Hata kama wataita kuwa ni njia na ukatikati si jengine isipokuwa ni shirki na sio ukatikati aliyouweka Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) katika Shari´ah. Allaah kamwe hakufanya shirki iwe ni njia ya kumfikia. Badala yake ni kuwa shirki inamuweka mtu mbali kabisa na Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala):

إِنَّهُ مَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدْ حَرَّمَ اللَّـهُ عَلَيْهِ الْجَنَّةَ

“Hakika mwenye kumshirikisha Allaah bila shaka Allaah atamharamishia Pepo.” (05:72)

Ni vipi basi shirki itakuwa ni njia ya kumfikia Allaah? Allaah ametakasika na yale wanayoyasema!

Kinacholengwa katika Aayah ni kwamba inafahamisha kuwa kuna washirikina wenye kuwaabudu watu wema. Allaah amebainisha hilo na kwamba wale wanaowaabudu ni waja wahitaji na kwamba:

يَبْتَغُونَ إِلَىٰ رَبِّهِمُ الْوَسِيلَةَ

“… wanatafuta kwa Mola wao njia [na] kumkurubia…

Bi maana wanajikurubisha Kwake kwa kumtii:

أَيُّهُمْ أَقْرَبُ

“.. kadri wanavyoweza… “

Bi maana wanashindana kwa ajili ya Allaah (Jalla wa ´Alaa) kupitia ´ibaadah kwa sababu wanamuhitajia Allaah:

وَيَرْجُونَ رَحْمَتَهُ وَيَخَافُونَ عَذَابَهُ

“… na wanataraji rehema Zake na wanakhofu adhabu Yake… “

Ambaye hali yake imeshakuwa namna hii hastahiki kuwa mungu anayeombwa na kuabudiwa pamoja na Allaah (´Azza wa Jall).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Qawaa´id al-Arba´ah, uk. 27-28
  • Imechapishwa: 18/08/2022