13. Dalili ya nne kwamba yule asiyeswali sio kafiri

Fungu la nne: Dalili zilizofungamanishwa na hali ambayo yule mwenye kuacha swalah anapewa udhuru. Mfano wa Hadiyth hiyo ni ile iliyopokelewa na Ibn Maajah kupitia kwa Hudhayfah bin al-Yamaan (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye ameeleza kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Uislamu utanyakuliwa mbali kama jinsi mtindo kwenye nguo unavyonyakuliwa mbali mpaka pale si swalah, swawm, kichinjwa wala swadaqah havitofanyiwa kazi. Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall) kitanyanyuliwa katika usiku mmoja na hakuna hata Aayah moja itayobaki ardhini. Kutabaki kundi la watu. Wazee wanaume na wanawake watasema: “Tumewakuta baba zetu wakisema ‘hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah’ na sisi tunasema hali kadhalika.” Swilah akasema: “‘hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah’ itawafaa nini ikiwa hawajui si swalah, swawm, kichinjwa wala swadaqah?” Hudhayfah akampa mgongo ambapo akamkariria mara tatu. Hudhayfah akamgeukia na kumwambia: “Ee Swilah! Itawaokoa kutokamana na Moto!” Alisema hivo mara tatu.”[1]

Watu hawa ambao shahaadah imewaokoa kutokamana na Moto wamepewa udhuru kwa kutotendea kazi Shari´ah za Kiislamu kwa sababu walikuwa si wenye kuzijua. Watafanya kile wanachokiweza. Hali zao zinafanana na wale wenye kufa kabla ya Shari´ah kufaradhishwa au kabla ya kuwahi kuzitendea kazi. Mfano wa mtu huyo ni kama yule mwenye kufa baada tu ya kutamka shahaadah au akasilimu katika nchi ya kikafiri na akafa kabla ya kutambua Shari´ah.

Kwa kufupisha ni kwamba maoni haya hayawezi kukabiliana na dalili zinazotumiwa na wale wenye kusema kuwa yule asiyeswali ni kafiri. Wale wenye kuonelea kuwa sio kafiri ima wanatumia dalili ambazo ni dhaifu na si sahihi, si hoja kabisa, dalili za kijumla ambazo zimefungamanishwa kwa njia ya kwamba hazihusiani na kuacha swalah, dalili zilizofungamanishwa na hali ambayo anapewa mtu udhuru kwa kuacha swalah au kwa dalili zenye kuenea zinazofanywa maalum na Hadiyth zenye kuthibitisha kuwa asiyeswali ni kafiri.

[1] Ibn Maajah (4121). Ni Swahiyh kwa mujibu wa Albaaniy katika ”Swahiyh Sunan Ibn Maajah” (3/326).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Hukm Taarik-is-Swalaah, uk. 15-16
  • Imechapishwa: 22/10/2016