Ndugu zangu! Ingawa umemalizika mwezi wa Ramadhaan lakini itambulike kuwa matendo ya muumini hayamalizika kabla ya yeye kufa. Allaah (´Azza wa Jall) amesema:
وَاعْبُدْ رَبَّكَ حَتَّىٰ يَأْتِيَكَ الْيَقِينُ
“… na mwabudu Mola wako mpaka kikufikie kifo.”[1]
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ حَقَّ تُقَاتِهِ وَلَا تَمُوتُنَّ إِلَّا وَأَنتُم مُّسْلِمُونَ
“Enyi walioamini! Mcheni Allaah ukweli wa kumcha na wala msife isipokuwa nyinyi ni waislamu.”[2]
Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:
“Anapokufa mja ndipo matendo yake hukatika.”
Kwa hivyo kifo ndio kimefanywa kuwa kikomo cha kukatika kwa matendo. Ingawa imekatika funga ya Ramadhaan hata hivyo muumini hakatishi ´ibaadah ya swawm. Swawm bado ni yenye kuendelea kusuniwa mwaka mzima. Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Ayyuub al-Answaariy (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:
“Yule atakayefunga Ramadhaan kisha akaifuatishia [siku] sita za Shawwaal, basi anakuwa kama amefunga mwaka mzima.”
Kuna swawm nyingine ambayo ni kufunga siku tatu kila mwezi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema juu yake:
“Kufunga siku tatu kila mwezi na Ramadhaan moja hadi nyingine hiyo ni swawm ya mwaka mzima.”
Ameipokea Ahmad na Muslim.
Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):
“Ameniusia kipenzi mwandani wangu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mambo matatu” ambapo akataja moja wapo “kufunga siku tatu kila mwezi.”
Bora zaidi siku tatu hizo iwe yale masiku meupe; tarehe 13, 14 na 15. Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema:
“Ee Abu Dharr! Utapofunga siku tatu katika mwezi basi funga kumi na tatu, kumi na nne na kumi na tano.”
Ameipokea Ahmad na an-Nasaa´iy katika “as-Swahiyh” yake.
Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliulizwa kuhusu swawm ya siku ya ´Arafah ambapo akasema:
“Inasamehe mwaka uliopita na mwaka ujao.”
Aliulizwa kuhusu kufunga ´Aashuuraa´ ambapo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:
“Inasamehe mwaka uliopita.”
Aliulizwa kuhusu kufunga siku ya jumatatu ambapo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:
“Hiyo ni siku niliyozaliwa na siku niliyotumilizwa au kuteremshiwa.”
Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliulizwa:
“Ni swawm ipi ambayo ni bora baada ya mwezi wa Ramadhaan?” Akasema: “Swawm bora baada ya mwezi wa Ramadhaan ni funga ya mwezi wa Allaah Muharram.”
al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) aliyesimulia:
“Sijapatapo kumuona Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akikamilisha mwezi wowote isipokuwa mwezi wa Ramadhaan. Sijapatapo kumuona akifunga kwa wingi mwezi wowote kama Sha´baan.”
Imekuja katika tamko jengine:
“Alikuwa akiufunga isipokuwa siku chache tu.”
Amesimulia tena (Radhiya Allaahu ´anhaa):
“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akijitahidi kufunga jumatatu na alkhamisi.”
Wameipokea watano isipokuwa Abu Daawuud ambaye yeye ameipokea kupitia kwa Usaamah bin Zayd.
Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:
“Matendo hudhihirishwa siku ya jumatatu na alkhamisi na kwa hivyo napenda matendo yangu yaonyeshwe hali ya kuwa nimefunga.”[3]
Ameipokea at-Tirmdhiy.
[1] 15:99
[2] 03:102
[3] Dhaifu lakini kuna nyingine inayoitolea ushahidi na kuipa nguvu. Imethibiti katika “as-Swahiyh” ya Muslim kwamba matendo yanaonyeshwa kila siku ya jumatatu na alkhamisi.
- Muhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
- Tarjama: Firqatunnajia.com
- Marejeo: Majaalis Shahr Ramadhwaan, uk. 226-228
- Imechapishwa: 01/04/2024
Mshirikishe mwenzako:
- Click to share on Telegram (Opens in new window)
- Click to share on WhatsApp (Opens in new window)
- Click to print (Opens in new window)
- Click to email a link to a friend (Opens in new window)
- Click to share on Facebook (Opens in new window)
- Click to share on Twitter (Opens in new window)
- Click to share on Pocket (Opens in new window)