10. Sunnah inahusiana tu na kufuata na kuacha matamanio

Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) amesema:

“Haifahamiki kwa akili wala matamanio. Inahusiana tu na kufuata na kuacha matamanio.”

Bi maana Sunnah inafahamika kwa mapokezi na sio kupitia akili wala matamanio. Ikiwa unataka Sunnah na unataka kuongozwa basi unachotakiwa ni kujifunza na kusoma. Unapojiwa na Sunnah basi unatakiwa kuielewa. Itumie akili yako kuweza kuifahamu:

“Yule ambaye Allaah anamtakia kheri basi humpa ufahamu akaielewa dini.”[1]

Kuzungumza bila ya dalili kutoka kwenye Qur-aan na Sunnah ni kuzungumza juu ya Allaah pasi na elimu:

قُلْ إِنَّمَا حَرَّمَ رَبِّيَ الْفَوَاحِشَ مَا ظَهَرَ مِنْهَا وَمَا بَطَنَ وَالْإِثْمَ وَالْبَغْيَ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَأَن تُشْرِكُوا بِاللَّـهِ مَا لَمْ يُنَزِّلْ بِهِ سُلْطَانًا وَأَن تَقُولُوا عَلَى اللَّـهِ مَا لَا تَعْلَمُونَ

“Sema: “Hakika Mola wangu ameharamisha machafu, yaliyodhihirika na yaliyofichika na dhambi [aina zote] na ukandamizaji bila ya haki. Na [ameharamisha] kumshirikisha Allaah kwa ambayo hakukiteremshia mamlaka na kuzungumza juu ya Allaah yale ambayo hamyajui.”[2]

Muislamu anatakiwa kushikamana na dalili inapokuja katika mambo ya ´Aqiydah, ´ibaadah, mambo ya halali na haramu. Kuhusiana na mambo ya kidunia fanya uwezalo:

“Hakika nyinyi ni wajuzi zaidi wa mambo ya dunia yenu.”[3]

Msingi ni kuwa mambo yote ya kidini ni haramu mpaka kinyume chake kithibitishwe katika Shari´ah. Pale tu utakapoanza kutumia akili zako katika dini ya Allaah  basi utakuwa ni mwenye kufuata matamanio yako na utakuwa ni mwenye kuzungumza juu ya Allaah pasi na elimu. Hii ndio aina kubwa ya dhambi. Wakati mwingine inaweza kuwa hata kubwa zaidi kuliko shirki, kama alivyoashiria hilo Ibn-ul-Qayyim wakati alipokuwa akifafanua Aayah hii na kusema:

“Ameyagawa madhambi katika ngazi nne. Ameanza kwa madogo mpaka kwenda katika makubwa.”[4]

Dhambi kubwa ni kuzungumza juu ya Allaah pasi na elimu. Ni kubwa kuliko shirki kwa sababu ndani yake kunaingia shirki na mambo mengine yote. Shirki si jengine isipokuwa ni matunda ya maneno ya watu wa batili na wapotevu. Kwa hivyo tahadharini sana kuzungumza juu ya dini ya Allaah kwa matamanio na usiache ukadanganyika na akili zenu na busara na uelewa wenu. Uelewa wote unapatikana katika dalili. Haya ndio yalikuwa matendo ya Maswahabah na Taabi´uun. Haya ndio ambayo Imaam Ahmad amesema hapa:

“Inahusiana tu na kufuata na kuacha matamanio.”

Ina maana ya kwamba usiache akili na matamanio yakashinda dini ya Allaah. Inahusiana tu na kufuata na kuacha matamanio kwa ajili ya Allaah, Mola wa walimwengu.

[1] al-Bukhaariy (71) na Muslim (1037).

[2] 07:33

[3] Muslim (2363).

[4] I´laam-ul-Muwaqqi´iyn (1/138).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Usuwl-is-Sunnah, uk. 372-373
  • Imechapishwa: 23/07/2017