Himdi zote zinamstahiki Allaah. Tunamhimidi Yeye na kumwomba msaada na msamaha na tunatubia Kwake. Tunajilinda kwa Allaah kutokana na shari ya nafsi zetu na matendo yetu maovu. Yule mwenye kuongozwa na Allaah, basi hakuna wa kumpoteza, na yule anayepotezwa na Allaah, hakuna wa kumwongoza. Ninashuhudia ya kwamba hapana mola mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allaah, hali ya kuwa peke yake hana mshirikina, na ninashuhudia kuwa Muhammad ni mja na Mtume Wake. Swalah na salaam zimwendee yeye, ahli zake, Maswahabah zake na yule mwenye kuwafuata kwa wema mpaka siku ya Qiyaamah.

Amma ba´d:

Damu zinazompata mwanamke ambazo ni hedhi, damu ya ugonjwa na damu ya nifasi ni katika mambo muhimu haja inapelekea kuyabainisha, kujua hukumu zake, kupambanua makosa na usawa kutoka katika maneno ya wanachuoni kuhusu hayo. Utegemezi wa lile litakalopewa nguvu au kudhoofishwa katika hayo itakuwa chini ya kivuli cha Qur-aan na Sunnah. Qur-aan na Sunnah ndio machimbuko mawili ya msingi ambayo kunajengwa juu yake hukumu za Allaah (Ta´ala) ambazo waja Wake wanamuabudu kwazo na akawawajibishia nazo. Jengine ni kwamba kutegemea Qur-aan na Sunnah kuna utulivu wa moyo, kifua kukunjuka, uzuri wa nafsi na kujitakasa na dhimmah. Kisichokuwa Qur-aan na Sunnah kinatakiwa kisimamishiwe hoja na wala hakifanywi kuwa ni hoja. Hakuna hoja isipokuwa katika Maneno ya Allaah (Ta´ala) na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Vilevile hili linahusu maneno ya wanachuoni katika Maswahabah kwa mujibu wa maoni yaliyo na nguvu. Hili ni kwa sharti katika Qur-aan na Sunnah kusiwe kitu kinachoenda kinyume nayo na isiwe ni yenye kupingana na kauli ya Swahabah mwingine. Ikiwa katika Qur-aan na Sunnah kuna kinachoenda kinyume na kauli hiyo, basi ni wajibu kutendea kazi kilichomo katika Qur-aan na Sunnah. Maoni ya Swahabah ikiwa yanapingana na maoni ya Swahabah mwingine, basi moja katika maoni hayo mawili yatatakiwa kupewa nguvu na kuchukua ile ilio na nguvu. Allaah (Ta´ala) amesema:

فَإِن تَنَازَعْتُمْ فِي شَيْءٍ فَرُدُّوهُ إِلَى اللَّـهِ وَالرَّسُولِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ

“Mkizozana katika jambo basi lirudisheni kwa Allaah na Mtume mkiwa mnamwamini Allaah na Siku ya Mwisho.” (04:59)

Huu ni ujumbe mfupi katika yale ambayo haja inapelekea kubainisha damu hizi na hukumu zake. Ujumbe huu una sura zifuatazo:

Sura ya kwanza: Maana ya hedhi na hekima yake

Sura ya pili: Wakati wa hedhi na muda wake

Sura ya tatu: Yanayotokea katika hedhi

Sura ya nne: Hukumu za hedhi

Sura ya tano: Damu ya ugonjwa na hukumu yake

Sura ya sita: Damu ya nifasi na hukumu yake

Sura ya saba: Dawa zinazozuia hedhi au kuileta, na zinazozuia mimba na kuiporomosha

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ad-Dimaa’ at-Twabiy´iyyah lin-Nisaa’ http://www.ibnothaimeen.com/all/books/article_16961.shtml
  • Imechapishwa: 29/10/2016