08. Mukhtaswari wa hali za anayetokwa na damu ya ugonjwa

Swali 08: Baadhi ya wanawake hawatofautishi kati ya hedhi na damu ya ugonjwa. Damu inaweza kuendelea kumtoka na hivyo akasimamisha swalah kwa kipindi chote cha kutokwa na damu hiyo. Ni ipi hukumu ya hilo?

Jibu: Hedhi ni damu ambayo Allaah amewaandikia wasichana wa Aadam katika kila mwezi  mara nyingi. Hivo ndivo ilivyopokelewa Hadiyth Swahiyh kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Mwanamke anayetokwa na damu ya ugonjwa anazo hali tatu:

1 – Mwanzoni mwake inapotoka. Katika hali hiyo analazimika kujizuilia kutokamana na ile damu anayoona kila mwezi. Kwa msemo mwingine ni kwamba ajizuilie kuswali na kufunga na wala si halali kwa mume wake kumjamii mpaka asafike ikiwa muda kumeshapita siku zisizopungua kumi na tano kwa mtazamo wa maoni ya wanazuoni wengi. Damu ikiendelea kumtoka zaidi ya siku kumi na tano basi mwanamke huyo ni mwenye damu ya ugonjwa. Anatakiwa kujizingatia kuwa ni mwenye hedhi kwa muda wa siku sita au siku saba kwa ajili ya tahadhari zaidi na kuangalia yale yanayowatokea wanawake wanaofanana naye katika wale ndugu. Hapo ni pale ambapo hawezi kutofautisha kati ya damu ya hedhi na damu nyingine.

2 – Lakini kama anaweza kupambanua basi atajizuilia kutokamana na swalah, funga na mume wake kumjamii kwa kipindi chote damu kumtoka iliyopambanuka kwa weusi au kwa harufu mbaya. Baada ya hapo ataoga na kuswali kwa sharti damu hiyo isizidi siku kumi na tano. Hii ni hali ya pili ya mwanamke mwenye damu ya ugonjwa.

3 – Awe na ada inayotambulika. Atakaa kipindi cha ada yake kisha ataoga na kutawadha kwa ajili ya kila swalah pale kunapoingia wakati wa swalah muda wa kuwa bado damu ni yenye kuendelea kumtoka. Mwanamke huyu ni halali kwa mume wake kumjamii mpaka itakapomjilia ada yake katika mwezi mwingine.

Haya ndio mukhtaswari wa yale yaliyopokelewa katika Hadiyth kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusu suala la mwanamke mwenye damu ya ugonjwa. Vilevile yametajwa na Haafidhw Ibn Hajar, ambaye ni mtunzi wa kitabu cha “Buluugh-ul-Maraam” na mtunzi wa “al-Muntaqaa” Ibn Taymiyyah (Rahimahumu Allaah).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa Muhimmah, uk. 08-09
  • Imechapishwa: 10/08/2022