05. Picha zinazofaa na zilizo haramu

Suala la tatu: Pasi na kujali jibu moja kati ya hayo mawili, je, katazo linahusu kutengeneza baadhi ya vitu bila vingine?

Tayari tumetangulia kutaja kwamba al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kwamba Ibn ´Abbaas amesema:

“Ikiwa ni lazima ufanye, basi tengeneza miti na vitu visivyo na roho.”

Hii inafahamisha kwamba inajuzu kutengeneza picha za vitu visivyo na roho, mfano wa milima, mabonde, mbingu na ardhi, miti na mfano wa hivyo. Kitu kinachotilia mkazo kwamba katazo hili linahusu tu picha za wanyama ni maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth ya Ibn ´Umar iliyotangulia:

”Fufueni mlivyoviumba!”

Kwa sababu changamoto ya kufufua na kuwabebesha watengeneza picha jukumu la kupuliza roho katika maumbo waliyoyatengeneza haifai isipokuwa pale maumbo hayo ni ya viumbe vilivyo na uhai, si ya viumbe visivyo hai. Mfano wa hilo ni ile iliyotangulia katika Hadiyth nyingine ya Ibn ´Abbaas kwa tamko lisemalo:

“Yeyote atakayetengeneza picha, basi Allaah atamuadhibu kwayo siku ya Qiyaamah mpaka apulize roho ndani yake, kitu ambacho hatoweza kukifanya.”

  • Muhusika: Imaam Muhammad bin ´Aliy ash-Shawkaaniy (afk. 1250)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Hukm-ut-Taswwiyr, uk. 27-28
  • Imechapishwa: 06/05/2026