03. Kinga ya mwenye kupatwa na msiba dhidi ya shaytwaan

Allaah amefanya yale maneno yanayosema yule aliyepatwa na msiba “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea” kuwa ni pahali pa kukimbilia kwa wale wenye misiba na kinga kwa wale waliopewa mtihani dhidi ya shaytwaan ili asimpe yule aliyepatwa na msiba fikira mbaya na akahamasisha yaliyotulia na akatoa yale yaliyofichikana.

Pindi yule aliyepewa msiba atapokimbilia maneno haya yaliyo na kheri na baraka, anakuwa ni mwenye kumthibitishia Allaah haki yake pekee ya kuabudiwa na haki ya mmiliki wakati anaposema “Sisi ni wa Allaah”. Pindi anaposema “Na Kwake ndiko tutakorudi” anathibitisha kuwa Allaah ndiye atakayechukua uhai wetu kisha atuhuishe. Hapa kunapatikana imani ya kuamini Ufufuliwaji baada ya kufa. Vilevile kunapatikana imani ya kuamini kwamba Allaah ndiye muamuzi wa mwanzo na kwamba kila kitu kitarejea Kwake huko Aakhirah. Ni katika kuwa na yakini. Allaah ndiye anayaendesha mambo yote. Hakuna makimbilio yoyote Kwake isipokuwa kupitia Kwake.

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Umm Salamah (Radhiya Allaahu ´anhaa) ambaye amesimulia kuwa alimsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

“Hakuna muislamu yoyote anayesibiwa na msiba na akasema “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea. Ee Allaah! Nilipe kwa msiba wangu na unipe kilicho bora kuliko hicho” isipokuwa inakuwa hivyo.”

Muslim amepokea vilevile kupitia kwa Umm Salamah ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mtapohudhuria kwa mgonjwa au maiti basi semeni yaliyo mazuri, kwani hakika Malaika huitikia “Aamiyn” kwa yale mnayoyasema.” Pindi Abu Salamah alipofariki nikamwendea Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kumwambia: “Ee Mtume wa Allaah! Abu Salamah amefariki.” Akasema: “Ee Allaah! Nisamehe mimi na yeye na unipe kilicho bora baada yake.” Nikasema hivo na Allaah akanipa aliye bora kuliko yeye; Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”

Mtu anaweza kufikia manzilah ya juu na thawabu nyingi endapo atasema “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea” wakati wa msiba, kama itavyotajwa katika Hadiyth ya Abu Muusa. Ndipo Allaah awaambie Malaika:

“Mja wangu amesema nini?” Waseme: “Amekuhimidi na kusema “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea”.” Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) aseme: “Mjengeeni mja Wangu nyumba Peponi na ipeni jina “Nyumba ya himidi”.”

Tumeshasema kwamba yule mwenye kusema “Sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutarejea” wakati wa msiba, basi anafikia baraka na rehema na ni mmoja katika walioongozwa. Maneno ya ´Umar “Ni neema iliyoje ya mambo mawili yanayochukua nafasi!” inahusiana na baraka na rehema na “Ni neema iliyoje ya nyongeza!” inahusiana na uongofu na Allaah ndiye anajua zaidi.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 11-12
  • Imechapishwa: 09/10/2016