Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) amesema:

“Himdi zote njema anastahiki Allaah aliyemtuma Mtume Wake kwa uongofu na kwa dini ya haki ili ipate kushinda dini zote na Allaah anatosha kuwa shahidi.

Nashuhudia ya kwamba hakuna mungu mwenye kuabudiwa kwa haki ispokuwa Allaah pekee, hali ya kuwa hana mshirika, kwa kukiri hilo na kumpwekesha Yeye pekee. Nashuhudia vilevile ya kwamba Muhammad ni mja na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kizazi chake na Maswahabah zake.

Ama baada ya hayo;

MAELEZO

Amemtuma Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa uongofu na dini ya haki. Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُونَ

“Yeye ndiye Aliyemtuma Mtume Wake kwa mwongozo na dini ya haki ili aidhihirishe juu ya dini zote, japo watakirihika washirikina.” (09:33)

Uongofu ni elimu yenye manufaa na maelezo ya kweli. Haya ndio huitwa kuwa ni uongofu. Dini ya haki ni zile Shari´ah zilizonyooka na adilifu inapokuja katika amri na makatazo. Allaah amemtuma (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa elimu yenye manufaa na matendo mema na Shari´ah iliyonyooka barabara. Amefanya hivo ili iweze kushinda dini zengine zote kutokana na ule uongofu aliyomtumwa kwao. Allaah anatosha kuwa ni shahidi kwa jambo hili kubwa.

Maneno yake (Rahimahu Allaah):

“Nashuhudia ya kwamba hakuna mungu mwenye kuabudiwa kwa haki ispokuwa Allaah pekee… “

Kukiri ya kwamba Yeye ndiye wa pekee na Mwenye kustahiki ´ibaadah, Yeye ndiye wa pekee katika dhati Yake, Yeye ndiye wa pekee katika sifa za majina Yake. Hana mshirika, mwenza na anayelingana Naye. Yeye ni wa pekee katika uola Wake na katika kuwaumba Kwake viumbe. Hakuna mwingine aliyewaumba asiyekuwa Yeye. Yeye ndiye Muumbaji na Mruzukaji. Yeye ni wa pekee katika kuabudiwa Kwake. Hakuna mwengine anayestahiki ´ibaadah asiyekuwa Yeye (Jalla wa ´Alaa).

Maneno yake:

“Kwa kukiri hilo… ”

Bi maana kwa Tawhiyd hii.

Maneno yake:

“Kumpwekesha Yeye… “

Kumuabudu Allaah peke Yake (Subhaanahu wa Ta´ala).

Baada ya hapo akamsalia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kama ilivyokuja katika Hadiyth. Amemuelekeza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mwenye kuomba du´aa aanze kwa kumhimidi kwanza Allaah kisha baada ya hapo amswalie (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Inapendeza mtu anapoanza kuomba du´aa au kuandika vitabu mtu aanze kwa kumhimidi Allaah, kumsifu, kumshuhudia ustahiki Wake wa ´ibaadah na kumshuhudia Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) utume. Kufanya hivi ni miongoni mwa sababu za kukubaliwa du´aa na ni miongoni vilevile mwa sababu za mafanikio. Kwa ajili hii amesema katika Hadiyth iliyopokea Fadhwaalah bin ´Ubayd (Radhiya Allaahu ´anh):

“Anapoomba mmoja wenu basi aanze kwa kumhimidi na kumsifu Allaah. Halafu amswalie Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kisha baada ya hapo aombe akitakacho.”[1]

Maneno yake:

“Ama baada ya hayo;”

Ni neno linaloletwa ili kutenganisha maneno ya kabla na yanayokuja baada yake. Malengo ni kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Kwa msemo mwingine ama baada ya maneno yaliyotangulia.

[1] Abuu Daawuud (1481) na at-Tirmidhiy (3477) ambaye amesema kuwa Hadiyth ni nzuri na Swahiyh. al-Haakim ameisahihisha katika ”al-Mustadrak” (840) na adh-Dhahabiy akaafikiana naye.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-´Aqiydah al-Waasitwiyyah, uk. 9-10
  • Imechapishwa: 31/05/2023