02. ´Aqiydah ya kundi lililonusuriwa na kuokoka mpaka siku ya Qiyaamah

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) amesema:

Hii ni I´tiqaad ya kundi lililookoka na kunusuriwa mpaka kisimame Qiyaamah, Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah, nayo ni:

MAELEZO

Maneno yake:

“Hii ni I´tiqaad… “

Bi maana ninasema kuwa hii nitakayoitaja huko mbele ndio I´tiqaad.

Maneno yake:

“Kundi lililookoka na kunusuriwa mpaka kisimame Qiyaamah… ”

Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameeleza kuwa ummah utagawanyika mapote sabini na tatu na kwamba yote yataingia Motoni isipokuwa moja tu. Kukasemwa: “Ni lipi hilo, ewe Mtume wa Allaah?” Akasema: “Ni mkusanyiko, al-Jamaa´ah.”[1]

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Ni lile linalofuata yale ninayofuata mimi hii leo na Maswahabah zangu.”[2]

Hawa ndio Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah. Wanaitwa pia “kundi lililookoka” na “kundi lililonusuriwa” mpaka Qiyaamah kisimame. Hizo zote ni sifa za pote moja. Linaitwa kuwa ni kundi lililonusuriwa mpaka siku ya Qiyaamah, kundi lililookoka, Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah na Ahl-us-Sunnah. Nao ni Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) na wale watakaofuata uongofu wao. Hawa ndio Ahl-us-Sunnah. Hawa ndio kundi lililonusuriwa. Ni Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wale wenye kufuata mfumo wao, uongofu wao na wakawaiga. Hawa ndio Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah.

Nje ya hao kunatoka Jahymiyyah, Mu´tazilah, Murji-ah, Qadariyyah na kila mwenye kwenda kinyume na Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum). Kila mwenye kwenda kinyume na Maswahabah anakuwa katika mapote sabini na mbili.

Ambaye yuko katika kundi lililonusuriwa ni yule anayefuata uongofu wa Maswahabah katika kumpwekesha Allaah, kumtakasia Yeye ´ibaadah, kufuata Shari´ah Yake na kuadhimisha amri Zake na kujiepusha na makatazo Yake kama ilivyokuja katika Kitabu Chake na Sunnah za Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Watu hawa ndio kundi lililonusuriwa.

[1] Ibn Maajah (3992), Abuu Daawuud (3597) na al-Haakim (443) ambaye ameisahihisha na adh-Dhahabiy akawafikiana naye (01/218).

[2] at-Tirmidhiy (2641), al-Haakim (444) ambaye ameisahihishya na adh-Dhahabiy ameafikiana naye (01/128).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-´Aqiydah al-Waasitwiyyah, uk. 10-11
  • Imechapishwa: 31/05/2023