Njia ni daraja itayowekwa juu ya Moto. Ina makali zaidi kuliko upanga na ni nyembamba zaidi kuliko unywele. Tunamuomba Allaah atuthibitishe sisi na nyinyi wakati wa kupita juu yake.

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Hurayrah na Hudhayfah (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) atawakusanya watu na Pepo itawasogelea waumini. Watu watamwendea Aadam na kusema: “Ee baba yetu! Tuombee kwa Allaah tufunguliwe Pepo.” Aseme: “Kuna jengine kilichowafanya kutolewa Peponi kama sio kwa sababu ya dhambi ya baba yenu Aadam?” Sio mimi nitayefanya hivo. Nendeni kwa mwanangu Ibraahiym ambaye ni kipenzi wa karibu wa Allaah.” Waende kwa Ibraahiym (´alayhis-Salaam) ambaye atawaambia: “Sio mimi nitayefanya hivo. Nilikuwa kipenzi wa karibu kupitia mkati kati. Nendeni kwa Muusa aliyezungumzishwa na Allaah.” Waende kwa Muusa ambaye atasema: “Sio mimi nitayefanya hivo. Nendeni kwa ´Iysaa ambaye ni neno na roho ya Allaah.” Waende kwa ´Iysaa atayesema: “Sio mimi nitayefanya hivo. Nendeni kwa Muhammad.” Waende kwa Muhammad na atapewa idhini. Amana na kukata udugu vitatumwa na vitakuwa pembezoni mwa Njia ya kila mmoja. Mtu wa kwanza wenu atapita kama umeme na atapita na kurudi kwa [muda wa] kupepesa macho, kisha kama upepo, halafu kama ndege na kama kipando – watapita kwa matendo yao. Mtume wenu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) atasimama pembezoni mwa Njia na kusema: “Ee Mola! Salimisha! Ee Mola salimisha!” mpaka yaishe matendo ya waja na mpaka apite mtu na asiweze kupita isipokuwa kwa kutambaa. Karibu na Njia kutakuwa ndoano zilizotundikwa zilizoamrishwa kumchukua kila aliyehukumiwa. Mwenye kuchanywa-chanywa ameokoka na mwenye kukamatwa anatumbukia Motoni. Ninaapa kwa yule ambaye nafsi ya Abu Hurayrah iko mkononi Mwake kufika chini kabisa ya Moto ni miaka elfu sabini.”

Abu Sa´iyd al-Khudriy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitaja Njia na watu kupita juu yake na kusema:

“Waumini watapita kama mpepeso wa macho, umeme, upepo, ndege na kama ngamia na mpandaji anayeenda mbio. Mwenye kuokoka na kusalimika ameumia na mwenye kukamatwa anatupwa Motoni.”

Ameipokea Muslim.

al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kutoka kwa Abu Hurayrah aliyeeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema:

“Njia itawekwa juu ya Moto. Mimi na Ummah wangu ndio tutakuwa wa kwanza kupita juu yake. Siku hiyo hakuna wataozungumza isipokuwa tu Mitume na watasema: “Ee Allaah! Salimisha! Salimish!” Kwenye Moto kuna ndoano kama miba ya Sa´daan[1]. Mmeshaona miba ya Sa´daan?” Wakasema: “Ndo, ee Mtume wa Allaah!” Akasema: “Ni kama miba ya Sa´daan japokuwa hakuna anayejua ukubwa wake isipokuwa Allaah (´Azza wa Jall) peke yake. Itawashika watu kutokana na matendo yao. Baadhi wataenda chini kwa matendo yao na wengine wataenda juu mpaka waokoke.”

[1] Tazama http://www.ahlalhdeeth.com/vb/showthread.php?t=277841

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 232-133
  • Imechapishwa: 24/12/2016