Ni ipi hukumu ya kutoa mawaidha makaburini, masherehe na kwenye mialiko?

Swali: Ni ipi hukumu ya mawaidha makaburini, kwenye masherehe na na kwenye karamu?

Jibu: Mawaidha makaburini inajuzu vile ilivyokuja katika Sunnah. Katika hali hiyo mtu asisimame na kuanza kuwakhutubia watu. Hilo halikuthibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na khaswa ikiwa kama atafanya ndio mazowea. Mawaidha makaburini yanatakiwa kuwa vile alivyofanya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Aliwawaidhi pindi aliposimama karibu na kaburi na kusema:

“Hakuna yeyote katika nyinyi isipokuwa ameshaandikiwa makazi yake Peponi na makazi yake Motoni.”[1]

Siku nyingine alifika makaburini wakati wamesimama wakisubiri kutengenezwe mwanandani. Akakaa na watu wakaa pembezoni naye. Akaanza kuchimba kwenye ardhi na kijiti na akataja hali ya mwanadamu wakati anapokata roho na baada ya kufa. Akawapa mawaidha ya kihakika. Kitendo kama hichi hakina neno. Ama mtu kusimama na kuanza kuwakhutubia watu ni jambo halikupokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Harusini pia haikuthibiti ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wala Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) walikuwa wakiwakhutubia watu kutokana na ninavyojua. Alipopata khabari (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amempa mwanamke mwanaume mmoja wa Answaar alisema:

“´Aaishah! Hamkuwa na burudani? Answaar wanapendezwa na budurani.”[2]

Inathibitisha kuwa kila kitu kina mahala pake. Watu wanaweza kuchukizwa mtu akisimama kukhutubu harusini. Si kila mtu anayakubali. Baadhi hawakutani na ndugu na marafiki zao isipokuwa katika masherehe haya. Hivyo wanataka kuzungumza, kuulizana na kufurahi ambapo wanaudhika na mawaidha kama haya. Sipendi watu waudhike kwa mawaidha. Watachukia mawaidha yenye kuudhi na yule mtowaji. Lakini lau watu watamuomba mtu azungumze basi azungumze na khaswa ikiwa ni mtu ambaye watu wanakubali maneno yake. Vilevile azungumze endapo ataona maovu anayotaka kuyakemea na kuyatahadharisha. Katika hali hii aseme:

“Ima msimamishe hayo au mimi natoka.”

Kila kitu kina mahapa pake. Hata hivyo ni bora ikiwa wanayapokea mawaidha kwa furaha. Kwa ajili hii Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiwawaidhi Maswahabah wake wakati muafaka bila ya kuwachosha.

[1] al-Bukhaariy (1362) na Muslim (2647).

[2] al-Bukhaariy (5162)

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (17/230-231)
  • Imechapishwa: 02/09/2021