68. Kutumia makadirio ya Allaah kama hoja?

Kuna masuala mengine yaliyotajwa na wanachuoni. Masuala yanayohusiana na kutumia makadirio kama hoja. Hilo ni kwa sababu Muusa (´alayhis-Salaam) alipokutana na baba wa watu, ambaye ni Aadam (´alayhis-Salaam) kwa Ummah wake, alimwambia:

“Ni kwa nini ulisababisha sisi na wewe tukatolewa Peponi?” Akasema: “Wewe ni Muusa msemezwa wa Allaah. Ni kwa muda kiasi gani ulikutana haya yameandikwa kwangu kwenye Ubao uliohifadhiwa?” Muusa akasema maneno yakiwa na maana ifuatayo: “Allaah aliyaandika hayo kwenye Ubao uliohifadhiwa.”

Jabriyyah wamelichukua hili na wakalitumia kama hoja ya kwamba Aadam ametumia kama hoja dhidi ya Muusa ya kwamba yaliyompitikia sio kwa khiyari yake. Wanasema kuwa ni kitendo cha Allaah (Jalla wa ´Alaa). Hawakufahamu Hadiyth. Muusa hakumlaumu Aadam juu ya mipango na makadirio. Alimlaumu kwa ajili ya kutolewa Peponi pindi aliposema:

“Ni kwa nini ulisababisha sisi na wewe tukatolewa Peponi?” Aadam akatumia hoja dhidi yake kwa mipango na makadirio. Kutumia hoja mipango na makadirio katika misiba ni jambo linajuzu. Ni jambo linamsahilishia mtu na anakuwa sio mwenye kuvunjika moyo wala kukasirika. Muusa hakumuuliza kuhusu mipango na makadirio. Hakumwambia:

“Ni kwa nini Allaah alikukadiria hivi?”

Bali alisema:

“Ni kwa nini ulisababisha tukatolewa?”

Alimuuliza kutokana na msiba uliopelekea katika yale yaliyomtokea Aadam kula kwenye mti. Muusa hakumlaumu juu ya dhambi. Hakumwambia:

“Ni kwa nini ulikula kwenye mti?”

Kwa sababu alitubu kutokana na dhambi yake na Allaah akamsamehe. Mwenye kutubia halaumiwi kwa yaliyomtokea baada ya kutubia. Alimlaumu kwa sababu ya kutolewa Peponi. Huu ni msiba uliowafika dhuriya ya Aadam. Aadam alitumia hoja dhidi ya Muusa (´alayhimaas-Salaam) kwa mipango na makadirio. Kutumia hoja kwa mipango na makadirio katika misiba ni jambo linakubalika kwa mujibu wa Shari´ah. Kwa ajili hii ndio maana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Utapofikwa na jambo usisemi “lau ningefanya kadhaa ingelikuwa kadhaa na kadhaa” badala yake sema “amekadiria Allaah  na alitakalo huwa.”

Mipango na makadirio inatumiwa kama hoja katika misiba. Kwa sababu wewe huna khiyari katika hayo. Allaah ndiye amefanya hivo. Kuhusu maasi ni dhambi yako wewe. Hivyo usitumie hoja kwa mipango na makadirio. Kwa ajili hii wanachuoni wamesema:

“Mipango na makadirio inatumiwa kama hoja katika misiba na haitumiwi kama hoja katika mambo ya aibu.”[1]

Huu ndio upambanuzi katika masuala haya makubwa.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Yakinisha makadirio yaliyopangwa… “

Kwamba ni kutoka kwa Allaah (Jalla wa ´Alaa).

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Yakinisha… ”

Bi maana itakidi.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… hakika ndio nguzo ya dini… “

Ni nguzo. Kuiamini ni nguzo ya sita katika nguzo za imani.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… nguzo ya dini… “

Kwa sababu dini imegawanyika katika daraja tatu:

1 – Daraja ya nguzo za Uislamu tano.

2 – Daraja ya imani kwa nguzo zake sita.

3 – Daraja ya Ihsaan kwa nguzo yake moja.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na dini ni pana.”

Ni sehemu pana. Dini ni pana na ni yenye kuenea.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (08/454)

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Mandhuumat-ul-Haaiyyah fiy ´Aqiydati Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 155-157
  • Imechapishwa: 07/02/2024