Ibn Baaz kubeba msahafu katika swalah za faradhi

Swali: Je, inafaa kwa imamu katika zile swalah tano akasoma ndani ya msahafu na khaswa swalah ya Fajr? Kwa sababu kurefusha kisomo ni jambo linalotakikana na anachelea asikosee au asisahau?

Jibu: Inafaa kufanya hivo haja ikipelekea kufanya hivo kama ambavo inafaa kusoma ndani ya msahafu katika Tarawiyh kwa ambaye hajahifadhi Qur-aan. Dhakwaan, ambaye ni mtumwa wa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) aliyemwacha huru, alikuwa akimswalisha ndani ya msahafu katika Ramadhaan. Hayo yametajwa na al-Bukhaariy katika “as-Swahiyh” yake hali ya kuyawekea taaliki na kwa njia ya kukata. Kurefusha kisomo katika swalah ya Fajr ni kitu kimependekezwa. Ikiwa imamu hakuhifadhi zile Suurah za kati na kati wala nyenginezo kutoka katika Qur-aan tukufu basi itafaa kwake kusoma ndani ya msahafu. Imewekwa katika Shari´ah kwake kujishughulisha na kuhifadhi Qur-aan na ajitahidi katika jambo hilo. Au angalau kwa uchache ahifadhi zile Suurah za kati na kati ili asihitajie kusoma ndani ya msahafu. Suurah za kati na kati ni kuanzia katika Qaaf mpaka mwishoni mwa Qur-aan. Atakayejipinda katika kuhifadhi basi Allaah atamfanyia wepesi jambo lake. Amesema (Subhaanah):

وَمَن يَتَّقِ اللَّـهَ يَجْعَل لَّهُ مَخْرَجًا وَيَرْزُقْهُ مِنْ حَيْثُ لَا يَحْتَسِبُ

“Na yule anayemcha Allaah humjaalia njia [ya kutokea] na atamruzuku kutoka njia ambayo hatizamii.”[1]

وَلَقَدْ يَسَّرْنَا الْقُرْآنَ لِلذِّكْرِ فَهَلْ مِن مُّدَّكِرٍ

“Kwa hakika Tumeiwepesisha Qur-aan kwa kuikumbuka, je, yuko yeyote mwenye kuwaidhika?”[2]

[1] 65:02-03

[2] 54:17

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (11/117)
  • Imechapishwa: 18/10/2021