Swali: Ni zipi sampuli za nafsi?

Jibu: Kuna aina tatu za nafsi:

 Ya kwanza: Nafsi yenye shari. Kwa jina lingine inaitwa nafsi yenye kuamrisha sana maovu.

Ya pili: Nafsi yenye kheri. Kwa jina lingine inaitwa nafsi iliyotulizana inayoamrisha kheri.

Ya tatu: Nafsi yenye kujilaumu sana.

Aina zote hizi zimetajwa katika Qur-aan. Nafsi yenye shari inayoamrisha sana maovu imetajwa katika Suurah ”Yuusuf”:

وَمَا أُبَرِّئُ نَفْسِي ۚ إِنَّ النَّفْسَ لَأَمَّارَةٌ بِالسُّوءِ

”Nami sijitakasi nafsi yangu. Hakika nafsi ni yenye kuamrisha sana maovu… ” (12:53)

Nafsi yenye kheri ambayo inaamrisha kheri imetajwa katika Suurah ”al-Fajr”:

يَا أَيَّتُهَا النَّفْسُ الْمُطْمَئِنَّةُ ارْجِعِي إِلَىٰ رَبِّكِ رَاضِيَةً مَّرْضِيَّةً  فَادْخُلِي فِي عِبَادِي وَادْخُلِي جَنَّتِي

“Ee nafsi iliyotua. Rejea kwa Mola wako hali ya kuwa umeridhika na mwenye kuridhiwa. Hivyo basi ingia miongoni mwa waja Wangu na ingia Pepo Yangu.” (89:27-30)

Nafsi yenye kujilaumu sana imetajwa katika Suurah ”al-Qiyaamah”:

لَا أُقْسِمُ بِيَوْمِ الْقِيَامَةِ وَلَا أُقْسِمُ بِالنَّفْسِ اللَّوَّامَةِ

”Naapa kwa siku ya Qiyaamah na naapa kwa nafsi inayojilaumu sana.” (75:01-02)

Nafsi yenye kujilaumu sana sio hiyo yenye kheri na yenye ovu au ni nafsi mbili? Wako wanachuoni waliosema kwamba ni aina ya tatu ya nafsi. Wako wengine waliosema ni wasifu wa nafsi mbili zilizotangulia. Kwa mfano nafsi yenye kheri inakulaumu wakati gani? Inakulaumu pale utapofanya maovu au pale utapozembea juu ya wajibu. Katika hali hiyo inakulaumu. Nafsi yenye shari inakulaumu wakati gani? Inakulaumu pale utapofanya kheri au pale utapojiepusha na jambo la haramu. Katika hali hiyo inakulaumu na kukunong´oneza ni kwa nini hukufanya yale yote unayotaka. Hii ni ile nafsi inayoamrisha sana maovu. Kuhusu nafsi yenye kheri inakulaumu pindi unapofanya shari na kuacha kufanya kheri. Kuhusu nafsi yenye shari inafanya kinyume chake.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://fatwa.islamweb.net/fatwa/index.php?page=showfatwa&Option=FatwaId&Id=140529
  • Imechapishwa: 13/09/2018