92. Muislamu wa kweli anatanguliza Qur-aan na Sunnah juu ya kila kitu

Alikuwepo mtu wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akiwaswalisha marafiki zake na alikuwa anasoma katika kila Rak´ah Suurah “al-Ikhlaasw.” Wakamweleza hayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambapo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamuuliza juu ya hilo:

Akajibu: “Kwa sababu naipenda; kwa kuwa ni sifa za Mwingi wa huruma na mimi naipenda.” Ndipo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamwambia: “Hakika kuipenda kwako kumekuingiza Peponi.”[1]

Yule anayeipenda Qur-aan na Sunnah ni dalili juu ya imani yake na hili litamuingiza Peponi. Upande mwingine yule mwenye kuchukia kitu katika Qur-aan au kitu katika Sunnah  kwa sababu inakwenda kinyume na matamanio yake, huyu sio katika waumini na matendo yake yanaharibika. Haijalishi kitu hata kama hakuongea. Vipi basi ikiwa ataongea na kupinga? Mambo yanakuwa khatari zaidi.

Kadhalika anaweza kuichukia Qur-aan na Sunnah kwa sababu inakwenda kinyume na madhehebu yake au madhehebu ya yule anayemuiga na kumfuata. Hivyo akawa anachukia kumtajia dalili kutoka katika Qur-aan na Sunnah. Kwa sababu haya yanakwenda kinyume na madhehebu yake ilihali mtu huyu anayapenda madhehebu yake zaidi ya anavyoipenda Qur-aan na Sunnah. Ikifikia mpaka katika kiwango hichi akayachukia ndani ya moyo wake yaliyotajwa katika Qur-aan an Sunnah, hii ni dalili inayofahamisha juu ya kutokuwa na imani na kitendo hichi kinayaharibu matendo yake. Muumini hatangulizi mbele ya Qur-aan na Sunnah chochote kile. Hatangulizi matamanio ya nafsi yake, madhehebu yake na madhehebu ya mwalimu wake. Kinyume chake Qur-aan na Sunnah anavitangulizi mbele ya kila kitu japokuwa yatakwenda kinyume na shahawa yake, matamanio yake, madhehebu yake au madhehebu ya yule anayemfuata. Muislamu halinganishi chochote na Qur-aan na Sunnah.

[1] al-Bukhaariy (7375) na Muslim (813).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 119-120
  • Imechapishwa: 29/11/2018