Miongoni mwa kampeni mbaya zinazofanywa kuhusu Hijaab, kuikemea na juu ya zile dalili zilizokuja kuhusu Hijaab. Bidii zao zingeenda patupu iwapo wangelijaribu kuzidhoofisha. Walipoona hawana njia nyingine ya kuzidhoofisha ndipo wakaanza kuzipindisha maana na kuzifasiri kinyume na tafsiri zake halisi na kinyume na makusudio ya Allaah na Mtume Wake. Je, huku si kuchukia yale aliyoteremsha Allaah na Mtume Wake? Haya ni katika mambo ambayo yamejitokeza hii leo katika jamii na yameonekana wazi katika maneno yao, mijadala yao na mahojiano yao. Hawataki atofautishwe mwanamke na mwanaume. Allaah (Ta´ala) katofautisha kati ya waislamu na makafiri, katofautisha kati ya waumini, mayahudi na manaswara. Wao wanasema kwamba hakuna tofauti kati ya waumini, myahudi na mnaswara. Wanasema kuwa wote ni waumini.

Ni kweli kwamba mayahudi na manaswara ni Ahl-ul-Kitaab ambao wana hukumu ambazo ni maalum. Lakini hata hivyo hawafanywi kuwa sawa na waumini na wala dini ya kiyahudi na dini ya kinaswara hazisawazishwi na dini ya Uislamu. Dini ya Uislamu ndio ya haki pekee. Hivyo haisawazishwi na dini ya uyahudi na unaswara. Haijalishi kitu japokuwa wana hukumu maalum zinzowapambanua na makafiri wengine. Lakini hii haina maana kwamba wanasawazishwa na dini ya Uislamu.

Mwenye kufanya dini ya kiyahudi na ya kinaswara kuwa sawa na Uislamu ni kafiri. Hawataki utaje Aayah kuhusu kuwapenda waislamu na kuwachukia makafiri ambazo Allaah kateremsha katika Qur-aan. Hawataki utaje Aayah ambazo zinawakaripia mayahudi na manaswara ambapo zimewasema vibaya, kuwalaani, kubainisha upotofu na fedheha zao. Hawataki utaje Aayah zinazoamrisha kuwachukia mayahudi na manaswara na kutojenga nao urafiki na kuwapenda. Wala hawataki kuzisikia. Je, huku si kuyachukia aliyoteremsha Allaah kwa Mtume wake? Hili ni jambo khatari sana. Allaah (Ta´ala) amesema:

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمُ اتَّبَعُوا مَا أَسْخَطَ اللَّـهَ وَكَرِهُوا رِضْوَانَهُ فَأَحْبَطَ أَعْمَالَهُمْ

”Hivyo kwa kuwa wao wamefuata yale yanayomghadhibisha Allaah na wakachukia radhi Zake. Hivyo akayaporomosha matendo yao.” (Muhammad 47:28)

Kwa hivyo ni wajibu kwa muislamu amche Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) na wala asiwapake mafuta makafiri wakiwemo mayahudi na mayahudi. Asiwapake mafuta katika dini ya Allaah (´Azza wa Jall):

وَدُّوا لَوْ تُدْهِنُ فَيُدْهِنُونَ

”Wanatamani lau kama ungelilainisha nao pia walainishe.” (al-Qalam 68:09)

أَفَبِهَـٰذَا الْحَدِيثِ أَنتُم مُّدْهِنُونَ

”Je, kwa hadithi hii nyinyi ni wenye kuibeza?” (al-Waaqi´ah 56:81)

Haijuzu kupakana mafuta katika dini ya Allaah. Ama kuhusu sisi kuamiliana na mayahudi, manaswara na makafiri wengine kwa mujibu wa ilivyokuja katika Qur-aan na Sunnah, hili ni haki. Ama kuwafanya wao kuwa ni sawa na waislamu ni batili. Amesema (Ta´ala):

لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ ۚأَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ

”Hawalingani sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi, watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.” (al-Hashr 59:20)

أَمْ حَسِبَ الَّذِينَ اجْتَرَحُوا السَّيِّئَاتِ أَن نَّجْعَلَهُمْ كَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ سَوَاءً مَّحْيَاهُمْ وَمَمَاتُهُمْ ۚ سَاءَ مَا يَحْكُمُونَ

”Je, wanadhania wale waliochuma mabaya Tuwafanye wawe sawa na wale walioamini na wakatenda mema na pia sawasawa uhai wao na kufa kwao? – uovu ulioje wanaouhukumu!” (al-Jaathiyah 45:21)

أَمْ نَجْعَلُ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ كَالْمُفْسِدِينَ فِي الْأَرْضِ أَمْ نَجْعَلُ الْمُتَّقِينَ كَالْفُجَّارِ

“Je, Tuwafanye wale walioamini na wakatenda mema kama mafisadi katika ardhi au tuwafanye wachaji kama waovu?” (Swaad 38:28)

Hili halijuzu kabisa. Allaah (Ta´ala) ameteremsha Qur-aan na Sunnah hali ya kupambanua kati ya muumini na kafiri. Ni mamoja kafiri huyu ni mwabudu sanamu, mpagani, mnaswara na myahudi. Ni wajibu kwetu kuwateremsha watu nafasi zao na wala tusichelee kwa ajili ya Allaah lawama za wenye kulaumu. Hapana shaka kwamba kuipenda Qur-aan na Sunnah ndio imani.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 117-119
  • Imechapishwa: 29/11/2018