Vivyo ndivo ilivyokuwa wakati wa ´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anh) na wale waliokuja baada yake. Wanawaua waislamu na hawawapigi vita makafiri. Hii ndio sifa yao; wanawakufurisha waislamu, wanaonelea kufaa kuuliwa na kufaa kuichukua mali yao, wanafarikisha na kuyaasi maneno Yake Allaah (´Azza wa Jall):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَطِيعُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُوا الرَّسُولَ وَأُولِي الْأَمْرِ مِنكُمْ

”Enyi mlioamini! Mtiini Allaah na mtiini Mtume na wenye madaraka katika nyinyi.”[1]

Wanawakufurisha watenda madhambi, licha ya kuwa madhambi yao ni chini ya shirki na kufuru. Mtu akizini, akaiba au akanywa pombe, basi wanamuona kuwa ni kafiri. Ambaye anafanya madhambi kama hayo wanaona kuwa ni kafiri. Hii ndio natija ya ujinga. Ni kweli wanafanya ´ibaadah na hamasa, lakini hawana elimu. Ujinga ni ugonjwa. Kufanya ´ibaadah pasi na elimu ni upotofu. Kufanya bidii pasi na uelewa ni upotofu. Ni lazima ipatikane elimu na uelewa. Kwa ajili hii Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) amesema juu yao:

Wanayo maandiko ambayo hawakujaaliwa kuyafahamu

matokeo yake wakafikwa na upungufu katika uelewa[2]

Wanafuata yale maandiko yasiyokuwa wazi na wanaacha yale maandiko yaliyo wazi. Wanajenga hoja kwa Aayah za Qur-aan na Hadiyth zisizokuwa wazi na wala hawarejei katika zile Aayah na Hadiyth zinazozifasiri na kuzibainisha. Hawarejeshi zile Aayah zisizokuwa wazi kwenda katika zile ambazo ziko wazi. Allaah (Ta´ala) amesema:

فَأَمَّا الَّذِينَ فِي قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ ابْتِغَاءَ الْفِتْنَةِ وَابْتِغَاءَ تَأْوِيلِهِ

”Basi wale ambao katika nyoyo zao mna upotevu hufuata zile zisizokuwa wazi ili kutafuta fitina na kutafuta kuzipotosha.”[3]

Ni wajibu kurejesha zile Aayah zisizokuwa wazi kwenda katika zile ambazo ziko wazi, baadhi ya maandiko ya Qur-aan yanafasiri mengine, kufasiri yale maandiko ambayo hayakufungamanishwa kwa yale yaliyofungamanishwa, yale maandiko yaliyotajwa kwa njia ya kuenea kwa yale maandiko maalum na kufanyia kazi yale maandiko yaliyofuta na kuachana na yale yaliyofutwa. Vivyo hivyo kuhusu Sunnah. Ama kutendea kazi yale maandiko yasiyokuwa wazi na kuyaacha yale yaliyo wazi si jengine isipokuwa upotofu. Khawaarij wanafanya namna hii.

Kinacholengwa ni sentesi:

“Hivi kweli hamniamini ilihali naaminiwa na Yule aliye mbinguni?”

Ambaye yuko juu ya mbingu ni Allaah (´Azza wa Jall). Amemweleza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba yuko mbinguni, bi maana juu. Hiki ndicho kinachokusudiwa katika Hadiyth. Vivyo hivyo sentesi:

“Najiwa na khabari za mbinguni asubuhi na jioni.”

Bi maana khabari inayoshuka kutoka Kwake ambaye yuko juu ya mbingu. Kwa maana nyingine kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala).

[1] 4:59

[2] an-Nuuniyyah (2/62).

[3] 3:7

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaa al-Hamawiyyah, uk. 120-122