79. Uchambuzi wa Ibn Taymiyyah juu ya kulipwa kwa yule aliyefikwa na msiba

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) amesema:

“Kuhusu ile misiba Allaah anafanya itokee, wakati fulani pasi na athari ya viumbe, kama maradhi, na wakati mwingine kwa athari ya viumbe. Kwa kufupisha ni kwamba mja analipwa kwa ile misiba ambayo ni matunda ya matendo mema kama vile Jihaad, kuamrisha mema, kukataza maovu na mfano wa hayo. Allaah anamlipa mja kwa matendo yake mema na yale ambayo yanatokamana na yeye ikiwa atakuwa na ustahamilivu. Mujaahid anayetoka kwenda katika Jihaad anajua kuwa ataudhiwa kwa ajili ya Allaah (´Azza wa Jall) na pengine akafikwa na madhara, farasi wake akafa, mali yake akapokonywa, atapigwa, akatukanywa na kadhalika. Allaah (Ta´ala) amesema:

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ لَا يُصِيبُهُمْ ظَمَأٌ وَلَا نَصَبٌ وَلَا مَخْمَصَةٌ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَلَا يَطَئُونَ مَوْطِئًا يَغِيظُ الْكُفَّارَ وَلَا يَنَالُونَ مِنْ عَدُوٍّ نَّيْلًا إِلَّا كُتِبَ لَهُم بِهِ عَمَلٌ صَالِحٌ ۚ إِنَّ اللَّـهَ لَا يُضِيعُ أَجْرَ الْمُحْسِنِينَ

“Hivyo ni kwa kuwa wao haiwasibu kiu, wala machofu, wala njaa kali katika njia ya Allaah, na wala hawakanyagi njia yoyote inayowaghadhibisha makafiri, na wala hawawasibu maadui msiba wowote isipokuwa [yote haya] wanaadikiwa kwayo matendo mema. Hakika Allaah hapotezi ujira wa wafanyao wema.” 09:120

Allaah (Ta´ala) ameeleza kuwa wanalipwa thawabu kwa kile kiu, kuchoka, njaa na mambo mengine wanayokutana nayo kwa sababu ya Jihaad katika njia ya Allaah. Allaah anasamehe madhambi kwa mambo haya na vilevile anawalipa thawabu kwa yale majanga kwa sababu yamewafika kwa sababu ya Jihaad. Majanga haya yanatokamana na kitendo hichi. Yale majanga ambayo yanatokamana na tendo jema kunalipwa thawabu juu yake.

Kuhusiana na njaa, kiu na kuchoka ambako hakutokamani na hilo, mtu analipwa kwa kule kuwa na subira juu yavyo. Matatizo haya yaliyotajwa hayatokamani na kitendo cha mja na wala sio matunda yanayotokamana na tendo jema. Katika hali hii matendo ya mja ndio yanayopatwa kufutwa.

Kuhusu kufiwa na mtoto, baba analipwa kwa kule kufiwa na mtoto pamoja vilevile na kumfutia dhambi zake ikiwa mtoto huyo anatokamana na jimaa ya kujikinga na uzinzi, kuukuza Ummah wa Kiislamu na kushusha macho chini kutokamana na ya haramu kwa sababu yamepitika kutokamana na matunda ya kitendo chake.

Ama maradhi na magonjwa, yanafuta madhambi. Imepokelewa ya kwamba watu walimwambia Abu ´Ubaydah bin al-Jarraah pindi walipomtembelea kwa sababu ya kuuguwa kwake: “Unapata ujira.” Ndipo akasema: “Sipewi ujira kwa haya. Ni maradhi ambayo Allaah hufuta madhambi kwayo.”

Haya niliyoyataja ndio tofauti kati ya yule msibiwaji anayelipwa thawabu kwa sababu ya msiba wake na yule msibiwaji asiyelipwa kwa sababu ya msiba wake. Baadhi ya wanachuoni wanasema kuwa yule aliyepatwa na msiba analipwa kwa hali zote na wengine wanasema sivyo hivyo isipokuwa analipwa kwa ile subira yake juu ya msiba huo.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 173-174
  • Imechapishwa: 19/11/2016