Swali 72: Je, katika medani na khaswa Saudi Arabia kuna mifumo inayopingana na mfumo wa Salaf? Ni vipi mtu atatangamana na mifumo hii na walinganizi wake?

Jibu: Katika nchi hii ya Saudi Arabia hakuna mifumo inayooenda kinyume na mfumo wa Salaf. Nchi nzima ni kwa mujibu wa Salafiyyah. Hata hivyo ndani ya nchi wanaweza kuwepo watu wa nje ambao wamebeba fikira zilizopinda[1]. Baadhi ya wakazi wa nchi hii wanaweza kuathirika nao kwa sababu ya ujinga wa kuwadhania dhana njema. Kwa ajili hiyo tunawashauri wakazi wa nchi yetu wajihadhari na watu hawa na watu mfano wao na wasimuamini kila mmoja. Hawazijui ´Aqiydah na mielekeo yao. Hawajui viwango vyao vya elimu na ni wapi wamejifunza elimu. Kwa sababu asiye na kitu hakuna pia anachoweza kutoa.

Hapo kale Najd ilikuwa imegawanyika. Kila kijiji kinajitawala na kinapiga vita kijiji kingine. Wakati Allaah alipoineemesha nchi hii kwa kujitokeza kwa Shaykh-ul-Islaam Muhamamd bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) ambapo akawalingania watu katika Tawhiyd na dini ya Allaah ambayo alikuja nayo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Akapambana na shirki, Bid´ah na mambo ya ukhurafi na kurejea katika dini sahihi. Allaah akaitunuku familia ya Su´uud kuwapa utawala ambao hapo kabla walikuwa wakihukumu kijiji kimoja peke yake. Lakini Allaah akawatunuku mababu zao ambao wakanusuru ulinganizi wa Shaykh Muhamamd bin ´Abdil-Wahhaab na wakapambana bega kwa bega pamoja naye. Hivyo kukakusanyika jihaad ya elimu na jihaad ya upanga. Hatimaye nchi nzima ikazungukwa na elimu na utulivu. Desturi za kipindi kabla ya kuja Uislamu na ada batili zikaondoka. Bid´ah, mambo ya ukhurafi na ya shirki yakapotea. Nchi ikakusanyika chini ya bendera ya shahaadah. Amani ikapatikana. Watu wakajenga udugu kati yao. Vijiji na miji ikakusanyika kuwa nchi moja.

Lakini msisahau kuwa maadui daima ni wenye wanajificha na wanataka kutenganisha umoja huu. Wanasababisha mifarakano hii kati ya ummah huu katika nchi hii. Wanaichafua kwa misingi ya kigeni na mifumo inayotia shaka inayokubaliwa na baadhi ya vijana. Hakuna wanachotutakia isipokuwa shari. Vinginevyo ni kipi wanachofanya? Je, sisi si kundi moja? Je, sisi si tuko katika Tawhiyd na ´Aqiydah? Je, sisi si tunaishi juu ya imani na utulivu? Ni kipi kingine tunachotaka zaidi ya haya? Ni kwa nini tunazikubali fikira ngeni, mifumo yenye kutoka nje na maoni ya watu ambao haitambuliki dini, elimu, masomo na ´Aqiydah yao? Kisha baadaye tunachukua maoni yao na tunaiacha ile dini sahihi na ´Aqiydah sahihi na mfumo uliosalimika? Tahadharini na mapote haya; watahadharisheni ndugu na watoto wenu.

Sisi ni kundi moja, ummah mmoja. Tunafuata mfumo mmoja na ´Aqiydah moja. Nchi yetu ni ya Kiislamu. Hukumu yetu ni kwa Shari´ah ya Allaah. Sisemi kuwa ni wakamilifu. Bali tuna mapungufu. Tunahukumu kwa Qur-aan na Sunnah. Nchi nzima ni ya Kiislamu na inahukumu kwa Shari´ah ya Allaah. Ina ´Aqiydah na mfumo mmoja ambayo imefunzwa na kupokelewa kizazi baada ya kingine.

Ni kwa nini tunakubali misingi hii, fikira hizi na mifumo hii iliyopinda kutokana na ´Aqiydah ambapo kila kipote kinashika mfumo wake na kila kipote kinajenga uadui dhidi ya kipote kingine na tunaacha mfumo sahihi na uliosalimika ambao walikuwa nao mababa na mababu zetu na wakaishi juu yake vizazi vyetu na nchi yetu? Je, huku si ni kuikufuru neema? Ni kwa nini hatukumbuki neema ya Allaah juu yetu:

وَاذْكُرُوا نِعْمَتَ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ إِذْ كُنتُمْ أَعْدَاءً فَأَلَّفَ بَيْنَ قُلُوبِكُمْ فَأَصْبَحْتُم بِنِعْمَتِهِ إِخْوَانًا َ

”Kumbukeni neema ya Allaah juu yenu, pale mlipokuwa maadui, kisha akaunganisha nyoyo zenu, mkawa kwa neema Yake ndugu.”[2]

Historia inajirudia. Ni lazima kwetu kufikiria tulipotoka na kusoma historia, kujua ni wapi tulipo, ni wapi tulikuwa na ni wapi tupo sasa.

[1] Kwa mfano wa Muhammad Suruur bin Nayaif Zayn-ul-´Aabidiyn aliyekuwa akiishi Qaswim, al-Ghazaaliy, ´Abdur-Rahiym at-Twahhaan  aliyekuwa akiishi ´Asiyr, Muhammad Qutuwb na wengineo. Wananadharia wao kutoka katika uongozi wa al-Ikhwaan al-Muslimuun na wajumbe wao wapo. Saudi Arabia iliwafanyia wema na wakaishukuru kwa fikira zao, ´Aqiydah na fataawaa zao zilizowashawishi vijana wetu. Tunamuomba Allaah atuongoze sisi na wao katika mfumo wa Salaf. Aamiyn!

[2] 3:103

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Ajwibah al-Mufiydah ´an As-ilat-il-Manaahij al-Jadiydah, uk. 179-183
  • Imechapishwa: 05/07/2024
  • taaliki: Shaykh Jamaal bin Furahyaan al-Haarithiy