73- Imamu atasimama nyuma ya kichwa cha mwanamme na katikati ya mwanamke. Zipo Hadiyth mbili juu ya hilo:

Ya kwanza: Abu Ghaalib al-Khayyaatw ameeleza:

“Nilimwona Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh) akiswalia jeneza la mtu mmoja ambapo akasimama usawa wa kichwa chake. [Katika upokezi mwingine imekuja: “Usawa wa kile kichwa cha kitanda]. Alipoinuliwa, kukaletwa jeneza la mwanamke mmoja wa Quraysh – au wa Answaar – akaulizwa: “Ee Abu Hamzah! Hili ni jeneza la mwanamke fulani bint fulani. Mswalie! Akamswalia ambapo akasimama usawa wa katikati yake [Katika upokezi mwingine imekuja: “Usawa wa kiuno chake na mwanamke yule akiwa na shuka la kijani].  Katika sisi alikuweko al-´Alaa´ bin Ziyaad al-´Adawiy[1]. Pindi alipoona tofauti ya kule kusimama juu ya mwanamme na juu ya mwanamke akasema: “Ee Abu Hamzah! Namna hii ndivo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akisimama ulivyosimama na juu ya mwanamke ulivosimama? Akajibu: “Ndio.” al-´Alaa´ akatugeukia akasema: “Hifadhini!”

Ameipokea Abu Daawuud (02/66-67), at-Tirmidhiy (02/146) ambaye ameifanya kuwa nzuri. Pia ameipokea Ibn Maajah, at-Twahaawiy (01/283), al-Bayhaqiy (04/32), at-Twayaalisiy (nambari. 2149), Ahmad (03/118, 204) na mtiririko ni wake. Wote wameitoa kupitia njia ya Hammaam bin Yahyaa kutoka kwa Abu Ghaalib mbali na Abu Daawuud ambaye yeye ameitoa kupitia kwa njia ya ´Abdul-Waarith, ambaye ni Ibn Sa´iyd, kutoka kwake. Kadhalika ameipokea at-Twahaawiy katika moja ya mapokezi yake kwa mukhtasari.

Cheni ya wapokezi wake kutoka katika njia zote mbili ni Swahiyh. Wapokezi wa njia mbili hizo ni wapokezi wa al-Bukhaariy na Muslim pasi na Abu Ghaalib, licha ya kuwa ni mwaminifu, kama ilivyotajwa katika “at-Taqriyb” ya al-Haafidhw Ibn Hajar. Ajabu kutoka kwake vipi ametaja katika maelezo ya Hadiyth ifuatayo kutoka kwa Samurah katika “al-Fath” (03/157) kwamba al-Bukhaariy ameashiria kuidhoofisha Hadiyth hii halafu akanyamazia jambo hilo na wala hakumkosoa kwa chochote.

Upokezi wa pili ni wa at-Twayaalisiy na al-Bayhaqiy kupitia kwa njia ya Ahmad.

Upokezi wa tatu ni wa Abu Daawuud. Uko kwa wale waliotajwa kwa mfano wake pasi na tamko “kijani”[2].

Ya pili: Samurah bin Jundub ameeleza:

“Nilikuwa nyuma ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akimswalia Umm Ka´b ambaye alifariki akiwa na damu ya uzazi. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasimama katikati yake.”

Ameipokea ´Abdur-Razzaaq (93/468), al-Bukhaariy (03/156-157), Muslim (03/60) na mtririko ni wake, Abu Daawuud (02/67), an-Nasaa´iy (01/280), at-Tirmidhiy (02/147) ambaye ameisahihisha, Ibn Maajah (01/455), Ibn-ul-Jaaruud (267), at-Twahaawiy (01/283), al-Bayhaqiy (04/34), at-Twayaalisiy (902) na Ahmad (1914).

Hadiyth inatoa ushahidi wa wazi kwamba Sunnah ni imamu kusimama usawa na katikati kwa mwanamke. Nayo imekuja kwa maana ya Hadiyth ya Anas:

“…. usawa wa kiuno chake.”

Bali  hili ni katika yale yanayozidi kuliweka wazi zaidi. Kwani iko wazi katika ushahidi kuliko makusudio ya Hadiyth ya Samurah.

[1] Kun-ya yake alikuwa akiitwa Abu Naswr. Ni katika waaminifu wa Taabi´uun. Alikuwa ni katika wachaji wa watu wa Baswhrah na wasomaji wao. Alifariki mwaka wa 94.

[2] Kwa Abu Daawuud kuna ziada nyingine ambayo ni lazima tuitaje na kubainisha hali yake. Nayo ni kama ifuatavyo:

“Abu Ghaalib amesema: “Niliuliza kuhusu kitendo cha Anas juu ya kusimama kwake usawa wa kiuno cha mwanamke. Wakanihadithia kwamba ilikuwa hivo kwa sababu kipindi hicho hapakuwa na majeneza yaliyofunikwa kwa ajili ya wanawake. Hivyo imamu akawa anasimama usawa wa kiuno chake kwa lengo la kumsitiri kutokamana na watu [waliyoko nyuma].”

Sababu hii ni yenye kurudishwa kwa njia nyingi:

Ya kwanza: Ni yenye kutoka kwa mtu asiyejulikana. Jambo linapokuwa hivo basi halina maana yoyote.

Ya pili: Ni kinyume na yale aliyofanya mpokezi wa Hadiyth mwenyewe, ambaye ni Anas. Yeye mwenyewe alisimama katikati yake ingawa mwanamke huyo alikuwa kwenye jeneza. Hivyo inalengesha juu ya kubatilika kwa sababu hiyo, jambo ambalo linatiliwa nguvu na njia inayofuata:

Ya tatu: Ni kinyume na yale waliyofahamu wahudhuriaji wa swalah ya Anas. Miongoni mwao ni al-´Alaa´ bin Ziyaad. Kwani wakati alipotaka kuelewa kutoka kwa Anas juu ya Sunnah hii aliwageukia wenzake na kuwaambia:

“Hifadhini!”

Jambo lingekuwa linatokana na sababu hiyo ambayo inarejea kuibatilisha Sunnah, basi al-´Alaa´ asingelitilia umuhimu huu mkubwa na kuwaamrisha wenzake walihifadhi, jambo ambalo liko dhahiri – na himdi zote anastahiki Allaah.

Kwa ajili hiyo wanachuoni wengi hawakuzingatia sababu hii. Wakaenda katika yale yaliyofahamishwa na Hadiyth juu ya kusimama usawa na kichwa cha mwanamme na usawa wa katikati na mwanamke. Miongoni mwao ni Imaam ash-Shaafi´iy, Ahmad na Ishaaq kama ilivyo katika “al-Majmuu´” (05/225). ash-Shawkaaniy amesema:

“Na ndio jambo la haki.”

Limechaguliwa na baadhi ya Hanafiyyah, bali ni maoni ya Abu Haniyfah mwenyewe, kama ilivyo katika “al-Hidaayah” (01/462) na Abu Yuusuf pia katika “Sharh-ul-Ma´aaniy” (01/284) ya Imaam at-Twahaawiy na akaipa nguvu juu ya rai zao zile zengine:

“Asimame  [wakati wa kumswalia] kwa mwanamme na mwanamke usawa wa kifua.”

Na ndio maoni ya Imaam Muhammad pia na waliyomo Hanafiyyah. Akawatolea hoja katika “al-Hidaayah” kwa kusema:

“Kwa sababu ndio mahala penye moyo na ndio kwenye nuru ya imani. Kwa hiyo kusimama usawa na hapo inakuwa ni ishara ya uombezi wa imani yake.”

Kisha akataja maoni ya Abu Haniyfah ya kwanza na kwamba alijengea hoja kwa maneno ya Anas aliposema:

“Ndio Sunnah.”

 ambapo mtunzi wa “al-Hidaayah” akaijibu kwa kusema:

“Tafsiri yake ni kwamba jeneza la mwanamke yule halikuwa limesitiriwa akaziba kati yake yeye na wale.”

Umekwishatambua kutokana na yaliyotangulia ubatilifu wa tafsiri hii. Lau watakubaliwa kwamba ni hivo, ni vipi hoja yao katika kwenda kwao kinyume na Hadiyth katika ile nusu yake ya kwanza ambayo ni kule kusimama kwake usawa na kichwa cha mwanamme. Wao wakasema: “Bali asimame usawa wake.” Laiti ningelikuwa najua ni kipi kimewafanya kuonyesha waziwazi kwenda kinyume na Sunnah kwa mfano wa tafsiri kama hizi ambazo ni batili na kule kusema kwao kwamba:

“… kwa sababu ndio mahala penye moyo… “

na maimamu wao wamesema hivo katika moja ya kauli zao. Kwa nini wasiichukue kama alivofanya at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) ambapo wakawa wamepatia Sunnah na pia wakawa wamechukua maoni ya maimamu wakati mmoja? Pamoja na mukhalafa huu wa wazi juu ya Sunnah hii na nyenginezo katika yale ambayo kutakuja uzinduzi juu yake wanawanasibishia wale wanaowatuhumu kwamba wanatanguliza maoni kabla ya Sunnah kutokana na uhafidhina wao!

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 139-141
  • Imechapishwa: 14/10/2020