2 – Miongoni mwa sababu ya kuhifadhi tupu ni kujiepusha na kusikiliza nyimbo na zumari. ´Allaamah Ibn-ul-Qayyim amesema katika “Ighaathat-ul-Lahfaan”:

“Miongoni mwa mbinu za shaytwaan ambazo amewaingiza wale wenye elimu, akili na dini chache na ameziwinda nyoyo za watu wajinga na watu wa batili ni kusikiliza miruzi, kupiga makofi, kuimba kwa nyenzo za haramu ambazo zinazuia mioyo mbali na Qur-aan na zinaifanya kudumu juu ya ufuska na maasi. Nyimbo ni Qur-aan ya shaytwaan, kizuizi kizito kinachomzuia mtu kwa Allaah, ndio ngazi ya liwati na uzinzi na kupitia kwazo ndipo anapopata yule mpenzi mwisho wa matarajio na matumaini yake.” Mpaka aliposema: “Ama kusikiliza kutoka kwa mwanamke au wavulana waliopendeza ni katika haramu na ufisadi uliomkubwa zaidi juu ya dini.” Mpaka aliposema: “Hapana shaka kwamba kila mwenye wivu anawaepusha familia yake kusikiliza nyimbo kama anavyowaepusha na sababu za mashaka.” Amesema vilevile: “Ni jambo linalojulikana kwa watu kwamba mwanamke akiwa na uzito wa kumpata mwanaume basi mwanamume anajitahidi kumsikilizisha sauti ya nyimbo na hapo ndipo inampa ulaini. Hili ni kwa sababu mwanamke ni mwepesi zaidi kuathirika kwa sauti. Sauti ikiwa ni kwa nyimbo basi mwanamke anaathirika kwa njia mbili; kwa njia ya sauti na kwa njia ya maana yake.” Akasema tena: “Ama ngazi hii ikikusanyika na dufu, ujana, kucheza na kujivunjavunja, lau mwanamke angelikuwa anapata mimba kwa nyimbo basi angelipata mimba kwa nyimbo hizi. Naapa kwa Allaah ni wanawake wangapi waungwana wamekuwa wamalaya kwa nyimbo hizi?”[1]

Ee dada wa Kiislamu! Mche Allaah na tahadhari kutokamana na magonjwa haya khatari ambayo ni kusikiliza nyimbo zinafanyiwa propaganda kati ya waislamu kwa aina na njia zake mbalimbali. Jambo hilo limewafanya wasichana wengi wajinga wanazitafuta kutoka katika vyanzo vyake na wanapeana zawadi kati yao.

[1] (01/242, 248, 264, 265).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tanbiyhaat, uk. 121
  • Imechapishwa: 12/09/2019