´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Kuna sampuli tatu za subira; subira juu ya misiba, subira juu ya utiifu na subira juu ya maasi. Mwenye kusubiri juu ya msiba mpaka akaurudisha kwa uzuri analipwa daraja mia tatu. Mwenye kusubiri juu ya utiifu analipwa daraja mia sita. Anayesubiri juu ya maasi analipwa daraja mia tisa.”

Maymuun bin Mahraan amesema:

“Kuna aina mbili za subira; kuwa na subira juu ya misiba – na ni jambo zuri – na lililo bora zaidi ya hilo ni kuwa na subira juu ya maasi.”

al-Junayd (Rahimahu Allaah) aliulizwa kuhusu maana ya subira. Akajibu:

“Ni kumeza yale machungu bila ya kukunja uso.”

al-Fudhwayl bin ´Iyaadhw amesema kuhusu maneno ya Allaah (Ta´ala):

سَلَامٌ عَلَيْكُم بِمَا صَبَرْتُمْ ۚ فَنِعْمَ عُقْبَى الدَّارِ

“Amani! [Haya ni malipo] kwa yale mliyosubiri na kustahamili!” Uzuri ulioje hatima ya nyumba hizi za milele!” 13:24

“Walisubiri juu ya yale waliyoamrishwa na yale waliyokatazwa.”

Ina maana kuwa anaonelea misiba inaingia katika yale yaliyoamrishwa.

Abus-Safar amesema:

“Pindi Abu Bakr alipokuwa mgonjwa alitembelewa na watu. Wakamwambia: “Tusikuitie daktari?” Akasema: “Nimeshapata daktari.” Wakasema: “Amekwambia nini sasa?” Akasema: “Amesema: “Mimi nafanya Nitakacho.”

´Aliy bin Abiy Twaalib amesema:

“Subira inapokuja katika imani ni kama kichwa kwenye mwili. Kichwa kikikatwa mwili unasimama.” Halafu akapaza sauti na kusema:

“Asiyekuwa na subira hana imani.”

al-Hasan al-Baswriy amesema:

“Subira ni hazina miongoni mwa hazina za kheri na Allaah hampi yeyote isipokuwa mja Wake mtukufu.”

´Umar bin ´Abdil-`Aziyz amesema:

“Allaah hajamneemesha mja neema kisha akaiondosha kwake na akaweka mahala pake subira isipokuwa kile alichokiweka mahala pake ni bora kuliko kile alichokiondosha.”

´Amr bin Qays amesema kuhusu maneno ya Allaah:

فَصَبْرٌ جَمِيلٌ

“Subira ni njema… ” 12:83

“Kuridhia na kujisalimisha juu ya msiba.”

Hassaan amesema:

“Subira isiyokuwa na malalamiko.”

Qataadah amesema kuhusu maneno ya Allaah juu ya Ya´quub:

وَتَوَلَّىٰ عَنْهُمْ وَقَالَ يَا أَسَفَىٰ عَلَىٰ يُوسُفَ وَابْيَضَّتْ عَيْنَاهُ مِنَ الْحُزْنِ فَهُوَ كَظِيمٌ

“Na akajitenga nao na akasema: “Ee majonzi yangu juu ya Yuusuf!” na macho yake yakageuka meupe [kwa kulia] kutokana na huzuni naye huku akiwa amezuia ghaidhi.” 12:84

“Huzuni wake daima ulikuwa ndani pasi na kutoa neno hata moja. Hakusema lolote isipokuwa kheri.”

al-Hasan amesema:

“Ina maana kwamba alikuwa mvumilivu.”

Yuunus bin Zayd amesema:

“Nilimuuliza Rabiy´ah bin Abiy ´Abdir-Rahmaan kuhusu subira kipeo chake cha juu kabisa. Akasema:

“Aione siku yake ile msiba umemfika ni sawa tu na siku kabla yake.”

Qays bin al-Hajjaaj amesema kuhusu maneno ya Allaah:

فَاصْبِرْ صَبْرًا جَمِيلًا

“Subiri subira njema!” 70:05

“Ina maana kwamba yule mwenye msiba anapokuwa kati ya watu asijulikane ni nani.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Muhammad al-Hanbaliy al-Manbajiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Tasliyatu Ahl-il-Maswaa-ib, uk. 140-142
  • Imechapishwa: 30/10/2016