Allaah (Ta´ala) amesema tena:

وَالسَّابِقُونَ الْأَوَّلُونَ مِنَ الْمُهَاجِرِينَ وَالْأَنصَارِ وَالَّذِينَ اتَّبَعُوهُم بِإِحْسَانٍ

“Wale waliotangulia mwanzoni ambao ni Muhaajiruun na Answaar na wale waliowafuata kwa wema… ”

Wamewafuata kwa wema, pasi na kuchupa mipaka wala kuzembea. Hawakuwa na msimamo mkali wala hawakulegeza; bali wamewafuata kati na kati:

رَّضِيَ اللَّـهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ وَأَعَدَّ لَهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي تَحْتَهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَدًا ۚ ذَٰلِكَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ

”… Allaah ameridhika nao nao wameridhika Naye na amewaandalia mabustani yapitayo chini yake mito – ni wenye kudumu humo milele. Huko ndiko kufuzu kukubwa.”[1]

Hii ni fadhilah kubwa inayopelekea mtu kufuata uongofu wa Salaf na kuwafuata. Kama alivosema Allaah (Ta´ala):

وَالَّذِينَ جَاءُوا مِن بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا اغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَانِنَا الَّذِينَ سَبَقُونَا بِالْإِيمَانِ وَلَا تَجْعَلْ فِي قُلُوبِنَا غِلًّا لِّلَّذِينَ آمَنُوا

”Na wale waliokuja baada yao wanasema: ”Ee Mola wetu! Tusamehe na ndugu zetu ambao wametutangulia kwa imani na wala Usijaalie katika nyoyo zetu mafundo ya chuki kwa wale walioamini!”

Hapa inawahusu wale wote waliokuja baada yao mpaka siku ya Qiyaamah. Kila ambaye atafuata mwenendo huu na akafuata nyayo zao anajumuishwa na Aayah:

وَالَّذِينَ اتَّبَعُوهُم بِإِحْسَانٍ

”… na wale waliowafuata kwa wema… ”

na:

وَالَّذِينَ جَاءُوا مِن بَعْدِهِمْ

”Na wale waliokuja baada yao… ”

Hawapati kwa Salaf isipokuwa mapenzi, matukuzo na heshima. Wanafaidika na elimu yao. Wanaitakidi kuwa wao ndio watu bora, watu waliotangulia na watu wanaomtambua zaidi Allaah (´Azza wa Jall).

Ni kweli kwamba vile vizazi vya wale waliokuja nyuma wameyajua mambo ya kidunia na uvumbuzi, lakini haifahamishi juu ya ubora wao. Kwa sababu elimu yao haihusiani na mambo ya Shari´ah. Hii ni elimu ya kimazingira. Elimu, fakhari na utukufu inapatikana katika ile elimu aliyokuja nayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hii ndio elimu inayomfaa mtu ulimwenguni na Aakhirah. Hata kama elimu ya mazingira inaweza kunufaisha, inaweza vilevile kumdhuru mtu. Inaweza kumpelekea mtu kuwa na kiburi, dhuluma na unyanyasaji. Ulimwengu umefaidika nini juu ya silaha hizi zinazoangamiza na mabomu ya atomiki? Hakuna zaidi ya uharibifu. Hali imekuwa kwamba wale waliozivumbua wenyewe wanaziogopa kwelikweli. Hata hivyo  ni vyema ikiwa elimu za mazingira zinamsaidia mtu juu ya matendo ya Aakhirah.

[1] 9:100

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 96-97
  • Imechapishwa: 13/08/2024